Monday, October 9, 2017

MWILI WA SHABAN YOHANA 'WANTED' WAPOKELEWA TANZANIA MAZISHI KUWA MICHUNGWANI JUMATANO

Sanduku lenye mwili wa Shaban Yohana Wanted lilipokelewa na wanamuziki wa Tanzania jana asubuhi katika ofisi za Swissport Dar es Salaam. Mwili wa mwanamuziki huyo ambaye aliefia Gaberone Botswana tarehe 14/9/2017 ulifanikiwa kufika Tanzania kutokana na juhudi za wanamuziki wenzake na wadau wa muziki walioko huko Botswana. Walioupokea mwili huo walikuwa ni John Kitime, Rashid pembe, Hassan Msumari na mwanamuziki wa kike Sholinder Mwezimpya. Maiti ilipelekwa hospitali ya Muhimbili kuhifadhiwa. Baada ya hapo wanamuziki walikutana Vijana Social Hall kupanga mikakati ya jinsi ya kufikisha mwili kijijini kwao Shaban. Wanamuziki, wadau wa muziki, Baraza la Sanaa la Taifa, Umoja wa Vijana, Mheshimiwa William Ngeleja Mbunge wa Sengerema, Dekula Kahanga Vumbi vikundi vya Whatsap vya Zamazile  na Kavasha ni kati ya walioweza kuchangia ili kufanikisha taratibu za kukamilisha safari ya Shaban Yohana Wanted.
Shabani atazikwa kesho Jumatano 11/10/2017, Michungwani Muheza. Safari ya kwenda huko itaanzia Muhimbili saa kumi na mbili asubuhi. wanamuziki kadhaa watamsindikiza mwenzao katika safari yake ya mwisho.

Wanamuziki waakiwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana Shaka Hamdu Shaka wakipanga kukamilisha safari ya mwisho ya Shaban Yohana. Shaban alikuwa kiongozi wa bendi ya Vijana Jazz  kuanzia mwaka 1990 hadi 1995.




No comments: