Saturday, June 3, 2017

NIDHAMU NA MAENDELEO YA MUZIKI KATIKA BENDI ZETU


Miezi michache iliyopita rafiki yangu mmoja alinambia ameamua kuunda bendi mpya kabisa, alikuwa na lengo la kuleta muziki mpya kabisa katika anga ya muziki Tanzania. Aliongea kwa furaha na ni wazi alikuwa ana nia ya kufanya kitu kikubwa, maana alikuwa amegharamia fedha nyingi kununua vifaa vipya kabisa vya kuanzisha bendi. Mwezi mmoja baada ya mazoezi kuanza alinitafuta na kunambia ameamua kuvunja bendi na vyombo anauza. Nilipomuuliza kwanini kabadili mawazo katika kipindi kifupi vile, hata onyesho moja halijafanyika? Akanijibu. ’Wanamuziki wamenishinda, wana matatizo makubwa ya ndhamu’. Kiukweli sikushangaa sana kwani jambo hili si geni kabisa kwenye tasnia ya muziki kwa siku hizi. Mfumo wa uendeshaji bendi siku hizi ni tofauti sana na miaka ya nyuma.

Nichukue mfano wa bendi Vijana jazz Band, bendi ambayo nilijiunga mwaka 1989. Kujiunga na bendi hii kulitokana na mwaliko niliyoupata kupitia kwa muimbaji rafiki yangu Marehemu Mohamed Shaweji. Shaweji tulikuwa wote Tancut Almasi Orchestra kisha yeye akaniacha kule na na kujiunga na Vijana Jazz Band, yeye na muimbaji mwingine Marehemu Gota gota wakiwa wamemfuata mpiga gitaa Shaaban ‘Wanted’ Yohana, aliyetoka Tancut pia na kuhamia Vijana Jazz Band miezi michache kabla. Hivyo siku moja nikiwa na bendi ya Tancut Almasi kwenye onyesho kwenye ukumbi wa CCM kata ya 14 Temeke, Shaweji alikuja na kunambia kuwa Hemed Maneti, kiongozi wa Vijana Jazz Band alikuwa anataka nijiunge na bendi yake. Nilikubali na mwezi Oktoba 1989 nilijiunga na Vijana Jazz. Kufikia mwezi wa Desemba mwaka huohuo nikawa nimepewa wadhifa wa kuwa Band Master, kazi za Band Master ni kuangalia nidhamu ya jumla ya wanamuziki, ikiwemo mahudhurio mazoezini na kazini, uchelewaji, ulevi, usafi binafsi wa mwanamuziki na pia kupanga ratiba ya nyimbo ambazo zinatakiwa kupigwa katika onyesho.  Kwa mfumo uliokuweko, Band Master aliweza kumsimamisha mwanamuziki yoyote aliyekiuka sheria za bendi, au kutoa adhabu ya kukatwa fedha kutoka kwenye mafao yake ya kila wiki ikiwa ni adhabu kwa makosa mbalimbali. Nguvu hizi zilifanya wanamuziki kuwa na nidhamu wakati wote wawapo kwenye shughuli za bendi. Ikumbukwe kuwa katika bendi kulikuweko na kiongozi mkuu Band Leader. Huyu alikuwa na mamlaka ya kufukuza mtu kazi na pia kuajiri na ndie anaepanga hata ukubwa wa mshahara, lakini alikuwa haingilii madaraka ya Stage Master. Kwa kawaida wanamuziki waliona ni heri matatizo yao yaishie kwa Band Master kwani yakifika kwa Band Leader yanakuwa ndio yamefika hatua ya mwisho isiyo na rufaa na inaweza kuwa hasara kubwa. Ili kuonyesha Band Master alivyokuwa na nafasi ya pekee, siku moja wakati niko Vijana jazz band, ilikuwa twende kwenye moja ya maonesho na kuna gari ilikuwa inatupitia wote majumbani kwetu, tulipofika nyumbani kwa Band Leader Hemed Maneti, alitoka nje akiwa na karatasi kutoka hospitali akaja kunitaarifu kama Band Master, kuwa hataweza kuja kazini kwani anaumwa, Maneti alikuwa Band Leader lakini alikuwa akiheshimu nafasi ya Band Master, tena nilikuwa bado mgeni katika bendi. Hii ilikuwa ni ishara wazi kwa wanamuziki wengine kuwa Band Master lazima aheshimiwe na wote.

Hali si hivi katika bendi nyingi siku hizi. Ngumu kujua nani mwenye madaraka gani kwani bendi zinakuwa na mwenye bendi, mkurugenzi wa bendi, meneja, maseneta, kiongozi wa bendi, wadau wa bendi. Wote hawa wana mamlaka zisizo na mipaka, wanaweza kuamua wimbo gani upigwe, wanaweza kuamua nani atimuliwe au nani aingizwe kwenye bendi, mmoja akimsimamisha mwanamuziki kwa utovu wa nidhamu mwingine anaweza akamrudisha, hakuna mtu mwenye amri ya mwisho kuhusu lolote lile, hivyo nidhamu imeshuka sana, na pasipo na nidhamu si rahisi kuweko na maendeleo yoyote yenye tija.

Sasa nizungumzie kosa la rafiki yangu aliyetaka kuanzisha bendi na ikamshinda, kwanza baada ya kununua vyombo, aliaanza kutafuta wanamuziki akisaidiana na watu wake wa karibu, kisha akamteua kiongozi wa bendi, ambae kimsingi kilikuwa kilemba cha ukoka kwani rafiki yangu ndie aliyekuwa na amri ya mwisho kuhusu lolote katika bendi. Na kwa kuwa hakuwa na muda wa kushinda kila mahala na bendi, kundi likawa halina kiongozi mwenye mamalaka  na mwisho kila mtu akawa anafanya lake, walevi wakalewa sana, wachelewaji wakendelea na uchelewaji wao, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo wa kutoa mwelekeo wa bendi kinidhamu wala kimuziki. Muziki wa bendi kwa ujumla umekumbwa na tatizo hili la kukosa uongozi, maamuzi mengi yanafanyika kwa vikao, hata maamuzi yale ambayo ni ya kitaaluma yanangoja makubaliano ya wengi, na kwa mtindo huu bendi zitachelewa sana kujikwamua kwenye tope ambalo zimenasa.  Ushauri kwa wanaotaka kufungua bendi, ni bora kumtafuta mwanamuziki mmoja ambaye unaamini anaweza kutengeneza muziki unaoutaka au unaodhani utakuletea biashara kisha umwachie aijege hiyo bendi na wanamuziki anaoona yeye wanafaa, hapa tayari utakuwa umejenga utawala unaoeleweka. Mwenye vyombo usiingilie moja kwa moja mambo ya bendi, wanamuziki wakishajua kuwa kiongozi wa bendi hana mamlaka kamili, nidhamu inavunjika.

Friday, June 2, 2017

HALILA TONGOLANGA AMELAZWA MUHIMBILI WODI YA KIBASILA


HALILA TONGOLANGA ALIWASILI DAR JANA USIKU NA KUFIKIA REGENCY HOSPITAL AMBAKO WALISHAURI KUWA AHAMISHIWE MUHIMBILI. KWA SASA AMEPEWA KITANDA. AMELAZWA KIBASILA NO 10. KWA MAWASILIANO UNAWEZA KUPATA TAARIFA ZAIDI KWA KUPIGA NAMBA YA MDOGO WAKE UWESU TONGOLANGA NI 0789800656

HABARI NJEMA, HALILA TONGOLANGA AMEPATA USAFIRI WA KUJA DAR ES SALAAM NA YUKO NJIANI, ANATEGEMEA KUFIKIA HOSPITALI TA REGENCY

MWANAMUZIKI HALILA TONGOLANGA AMEWEZA KUPATA BAHATI YA KUPATA USAFIRI UTAKAOMLETA KWENYE MATIBABU DAR ES SALAAM. TONGOLANGA ANATEGEMEWA KUFIKIA HOSPITALI YA REGENCY. ANASINDIKIZWA NA WADOGO ZAKE WAWILI. TUZIDI KUMUOMBEA NDUGU YETU

Thursday, June 1, 2017

HALILA TONGOLANGA ANAUMWA ANAHITAJI MSAADA WA HARAKA SANA


MWANAMUZIKI HALILA TONGOLANGA MTUNZI WA WIMBO MAARUFU WA KILA MUNU AVE NA KWAO, AMEUGUA GHAFLA AKIWA KATIKA ZIARA YA MUZIKI MIKOA YA KUSINI. ANATAKIWA KURUDISHWA DAR ES SALAAM MAPEMA APATE MATIBABU YA HARAKA MUHIMBILI. KWA SASA AMELAZWA KATIKA HOSPITALI YA NDANDA. ANAE ONA AMEGUSWA NA ANAWEZA KUTOA USAFIRI AU MSAADA WOWOTE  APIGE SIMU 0713644439 ILI KUWASILIANA NA KATIBU MTENDAJI WA BARAZA LA SANAA LA TAIFA.

NI MIAKA 27 TOKA KIFO CHA HEMEDI MANETI

Picha niliyoipiga tukiwa chumba cha maiti Muhimbili, mbele yetu ulikuwa mwili wa Hemedi Maneti. Kati ya waliopo kwenye picha ni marehemu Mzee jacob John, mwenye shati jeusi na marehemu Salum Faya mwenye jaketi jekundu
Mara ya kwanza kukutana uso kwa uso na Hemedi Maneti ilikuwa ni wakati Vijana Jazz band ilipita Iringa  ikielekea Songea mwaka 1989. Wakti huo nilikuwa mwanamuziki wa Tancut Almasi Orchestra, na kama ilivyokuwa ada miaka ile, bendi ikipita katika mji ambao kuna bendi wanamuziki walikuwa wakipiga muziki pamoja. Tuliongea nae machache lakini aliongea kuhusu kufurahishwa na setting ya vyombo vyetu, alisema inafanya vyombo vyote visikike. Wakati huo hatukujua lakini kumbe alikuwa kishaongea na Shaaban Wanted, Mohamed Gotagota na Mohamed Shaweji ili wajiunge na Vijana Jazz band, na hakika walihamia bendi hiyo wiki chache zilizofuata.
Katika mlolongo huohuo nilijikuta nikiitwa kujiunga na Vijana Jazz Band mwezi wa September mwaka huohuo na kufikia Oktober 1989 niliwasili Dar es Salaam kujiunga na Vijana Jazz Band. Siku ya kwanza nilipofika Vijana maneti alinipa shilingi 300 za kuanza maisha. Nitafute guest house ya kuishi na chakula kwa wiki moja. Hiyo ndiyo kumbukumbu yangu ya kwanza ya Maneti ambaye miezi michache baadae, tarehe 31 May 1990 siku ya Alhamisi majira ya saa kumi na moja jioni, Hemed Maneti alifariki katika hospitali ya Mwananyamala.  Alikuwa ameanza kuwa na matatizo ya afya miezi kadhaa kabla ya hapo na  hatimae kupelekwa Tanga kwa ajili ya matibabu. Hali yake ilipozidi kuwa mbaya alirudishwa kwa ndege  kuwasili Dar Jumatano 30 May na kupelekwa moja kwa moja hospitali ya Mwananyamala ambapo alilala na kufariki kesho yake. Marehemu alisafirishwa kwenda kuzikwa Tanga siku moja baadae.
Wimbo wa mwisho kurekodi ulikuwa wimbo Nelson Mandela uliotungwa nami, ukiwa wimbo uliokuwa matayarisho ya ziara ya Nelson Mandela.

Friday, May 26, 2017

URAFIKI WA MUZIKI NA SIASA ULIANZA ENZI ZA UKOLONI



 
Miaka michache baada ya Tanganyika kupata Uhuru, nchi yetu ikabadili mfumo wa siasa na kuwa na siasa ya chama kimoja. Hivyo chama cha TANU kikawa ndicho chama pekee cha siasa nchini. Katika mtiririko huo wa siasa ya chama kimoja,  vyama vingine mbalimbali vilivyokuwa si vya kisiasa, vikaunganishwa ili kuwa kwa namna moja au nyingine chini ya TANU, hivyo kukaweko na muungano kama National Union of Tanganyika Workers (NUTA) kwa ajili ya vyama vya wafanyakazi, Cooperative Union of Tanganyika (CUT), muungano wa vyama vya  ushirika, TANU Youth League (TYL) chama cha vijana,  na kadhalika. Pia jeshi likaundwa upya na kukaundwa Tanzania Peoples Defence Force (TPDF) baada ya vurugu ya jeshi la awali la lililorithiwa kutoka kwa wakoloni lililoitwaTanganyika Rifles, na baadae jeshi jingine la kujitolea lililoitwa National Service likaanzishwa. Hakika mabadiliko yalikuwa mengi sana katika miaka saba ya kwanza baada ya Uhuru wa Tanganyika, likiwemo pia tukio kubwa la muungano wa Tanganyika na Zanzibar, na kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.  Mabadiliko haya mengi na ya muda mfupi yaligusa kila sekta ikiwemo sekta ya muziki. Katika miaka hii, kulikuwa na aina mbalimbali za muziki uliokuwa ukipendwa , ukiwemo muziki wa dansi, taarab, kwaya na ngoma za asili. Muziki wa dansi  ulikuwa umejikita hasa mijini, bendi zikiwa mali za watu binafsi au taasisi binafsi. Lakini baada ya mabadiliko hayo niliyo yataja hapo juu, vyombo vya umma vikaanza kuzindua vikundi vyao vya muziki. Kati ya bendi za kwanza kuanzishwa kupitia mfumo hu, zilikuwa ni NUTA Jazz Band ikijitambulisha kwa mtindo wa msondo, Polisi Jazz Band na mtindo wa Vangavanga, National Service Jazz Band na mtindo wa Kimbunga, baadaye bendi hii ikaja kuitwa Kimbunga Stereo, baada ya bendi nyingine ya National Service kuanzishwa katika kambi ya jeshi hilo huko Mafinga Iringa, ambayo iliitwa National Service Kimulimuli. Jeshi la wananchi nalo likaanzisha bendi Mwenge Jazz Band wana Paselepa, na hivyo hivyo Jeshi la Magereza wakawa na Magereza Jazz Band waliokuja kuwa namtindo wa Super Mnyanyuo na hata idara ya Uhamiaji nayo ilianzisha bendi maarufu ya Uhamiaji Jazz Band iliyokuwa na mtindo wao wa Hamahama. Vijana wa chama cha Tanu, walianzisha TANU Youth League Jazz Band, iliyokuja kupata jina la Vijana  Jazz Band baadae. TYL ilianzisha pia bendi nyingi katika wilaya mbalimbali nchini, kama vile Mbeya lringa, Mwanza, Moshi, Lindi, Songea, Bagamoyo, Tunduru, Biharamulo, Nachingwea, Njombe, Same na kadhalika. Muungano wa vyama vya Ushirika nayo pia ikaja kuwa na bendi iliyokuja kuwa maarufu sana, Washirika Tanzania Stars. Mashirika ya umma nayo yakaanzisha bendi, Urafiki Jazz Band, ilikuwa mali ya kiwanda cha nguo cha Friendship Textile Mills, shirika la State Trading Corporation likaja na STC Jazz Band ambayo baadae ilikuja kuitwa Biashara Jazz band. Kampuni ya mabasi ya Usafiri Dar es Salaam ikazindua bendi yao ya UDA Jazz Band,
National Insurance Corporation, shirika la bima nalo likaanzisha Bima Jazz Band ambayo wanamuziki wake awali wengi walikuwa wanamuziki wa BAT Jazz Band mali ya  kampuni ya sigara ya British American Tobacco (BAT), kampuni iliyokufa na kuzaliwa kampuni ya Tanzania Cigarette Company (TCC). Mwaka 1978. Tanzania Taxi and Transport Service (TTTS) wakaanzisha bendi yao waliyoiita Mlimani Park Orchestra, jina la Mlimani lilitokana na bendi kuanzia Mlalakuwa jirani na chuo kikuu cha Dar es Salaam maarufu kwa jina la Mlimani, bendi hii ilikuja kubadili jina baada ya kuchukuliwa na Dar es Salaam Development Corporation (DDC) na kuitwa DDC Mlimani Park Orchestra mwaka 1982. Mashirika ya umma na idara za serikali zilianzisha bendi hizi hasa kwa ajili ya kuburudisha  wafanyakazi wake, lakini pia na kutambua uwezo wa muziki katika kusambaza ujumbe ambao mashirika haya yalitaka uwafikie wananchi, na mwisho bendi hizi zilikuwa ni vitega uchumi. Bendi za mashirika kama Urafiki Jazz Band, Biashara Jazz Band, na Bima Lee, kwa mfano zilifanya kazi za kutangaza biashara za kampuni zao na bendi zilizunguka kila wilaya nchini, na hata kwenye vitongoji vidogo kabisa. Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), lilikuwa na bendi tatu ikiwemo Kimbunga Stereo ikiwa kambi ya Mgulani, Kimulimuli katika kambi ya Mafinga, na kambi ya Makutopora nayo pia ikawa na bendi yake. Kulikuwa na bendi za Polisi maarufu kama Usalama jazz Band  huko Bukoba na Moshi, wakati Polisi Jazz band ilikuwa Dar es Salaam. Kuna hata Kurugenzi za mikoa zilizoanzisha bendi zilizokuja kuwa maarufu, bendi za Kurugenzi Arusha na Kurugenzi Dodoma ni kati ya bendi hizo. Kwa kuwa chama cha siasa kilikuwa kimoja tu, bendi zote hizi, pamoja na bendi zilizokuwa za watu au vikundi binafsi zilishiriki kikamilifu katika kutangaza mambo yote ya siasa wakati ule. Kimsingi hakukuwa na mabadiliko sana kwa jambo hili, kwani mahusiano kati ya wanamuziki na siasa yalianza toka wakati wa kupigania Uhuru, wazee kama marehemu Mzee Nnauye walitumia sana muziki kuhamasisha wananchi kuunga mkono juhudi za kumuondoa mkoloni. Uhusiano huu uliongezeka sana mara baada ya Uhuru kwa bendi kutunga nyimbo nyingi za uzalendo na kuhamasisha ujenzi wa Taifa jipya. Mpaka kufikia mwishoni mwa miaka ya 1980, kila wakati wa kurekodi nyimbo mpya bendi zilikuwa japo na wimbo mmoja wa siasa katika kila nyimbo sita. Radio ya Taifa ilizipiga sana nyimbo hizi na zikafahamika nchini kote.RTD wakati huo ilikuwa ni ngazi moja kubwa ya kutangaza nyimbo za bendi za hapa nchini. Takwimu moja iliyofanywa July 1968, ilionyesha kuwa asilimia  84% ya nyimbo zilizoombwa na wasikilizaji katika vipindi vitatu vya Idhaa ya Kiswahili ya RTD, zilikuwa ni nyimbo za Kiswahili, kutoka Tanzania, na nyingi zikiwa nyimbo za siasa. Bendi hazikuongelea tu siasa za ndani ya nchi bali ziliongea pia kuhusu siasa zilizokuwa zikiendelea ulimwenguni na hasa kuhusiana kupigania uhuru wa nchi zilizokuwa bado zinatawaliwa Afrika. Vijana Jazz Band ndio ilikuwa bendi kubwa ya kuelezea mipango, sera na maanuzi ya chama tawala, bendi ilikuwa mstari wa mbele kwenye kampeni za uchaguzi na kutunga nyimbo nyingi za kupigia debe mgombea wa chama tawala. Bila kusahau bendi zilifanya kazi kubwa ya kuwahamasisha askari na wananchi wakati wa vita ya Kagera, baada ya vita vikundi vya muziki vya JKT, JWTZ na Magereza, vilizunguka sehemu mbalimbali nchini Uganda kupiga muziki kuwahamasisha watu kurudi kutoka mafichoni.
Mwisho lazima nitoe mfano wa bendi binafsi zilivyokuwa zinashiriki katika siasa. Bendi kama Kilwa Jazz band ilikuwa moja ya bendi iliyotumika sana na wanasiasa wa TANU kuhamasisha watu juhudhuria mikutano ya kisiasa, na hata katika mikutano ya kuchangia chama. Kilwa Jazz ndio ilikuwa bendi rasmi iliyopiga muziki siku ya sherehe za mwaka wa pili wa Uhuru 1962, na ndio bendi iliyopelekwa na serikali kwenye sherehe za Uhuru wa Malawi mwaka July 6, 1964.

Monday, May 1, 2017

MSONDO KUTENGENEZA HISTORIA?

HABARI ambazo hazijathibitishwa zimesema kuwa bendi ya Msongo Ngoma Music imechukuliwa tena na Chama cha Wafanyakazi, na itaitwa TUCTA Jazz Band 'Msondo Ngoma'.  Hii itakuwa historia ya mambo mengi, kwanza kurudi kwa uhusiano kati ya bendi hii na vyama vya wafanyakazi. Bendi hii ilianzishwa na chama cha wafanya kazi cha NUTA mwaka 1964 na kuitwa NUTA Jazz Band, na kubadilika kuwa JUWATA Jazz Band baada ya mabadiliko yaliyozaa Jumuiya ya Wafanya kazi Tanzania (JUWATA). Baada ya mabadiliko mengine yaliyoleta chombo kilichoitwa Organization of Tanzania Trade Unions (OTTU), bendi ikabadili jina na kuitwa Ottu Jazz band, kwa muda mfupi kulikuweko mabadiliko mengine yaliyoleta Tanzania Federation of Free Trade Unions (TFTU), na bendi ikachukuliwa na TFTU. Hatimae bendi ikajikuta iko huru ikiendeshwa na wanamuziki wenyewe na ndipo ilipojipa jima la Msondo Ngoma Music Band, na kama inavyosikika inaweza sasa tena ikaitwa TUCTA Jazz Band.hakika itakuwa moja ya bendi ambazo zimewahi kubadili jina mara nyingi kuliko bendi nyingine duniani.