Harrison Siwale (Satchmo) mpiga rythm, Mbaraka Mwinyishehe mpiga solo, Abdul Mketema mpuliza saksafoni |
Lakini katika makala ya leo tuzungumzie gitaa la rythm. Chombo hiki bado kinapigwa katika bendi nyingi lakini umuhimu wake umeshuka sana. Katika kipindi cha miaka ya 60 na 70, gitaa hili lilikuwa na umuhimu mkubwa na wapigaji wake waliweza kubuni staili zao wenyewe. N kujijengea sifa kubwa. Kati ya wapiga rythm maarufu alikuweko Satchmo, hilo ndio lilikuwa jina la kisanii la Harrison Siwale, huyu alikuwa Mzambia aliyekuja weka masikani yake katika mji wa Tanga. Alipitia bendi kubwa za Tanga ikiwemo Atomic Jazz Band na hatimae Jamhuri Jazz Band. Satchmo alikuwa na staili peke yake ya kupiga rythm, sikumbuki kusikia mtu mwingine akipiga rythm ya aina yake kabla ya hapo, lakini hakika wapiga rythm wengi walichukua mtindo wake na kubuni vionjo vya aina yao. Rythm yake ilitawala nyimbo za Jamhuri Jazz Band wakati huo. Ufundi wake unaonekana sana katika nyimbo kama Mganga no 1 na 2, au Blandina. Kule Tabora Mzee Kasim Kaluwona nae alikuwa na staili tofauti ya upigaji wa gitaa la rythm uliyoifanya Tabora Jazz kuwa na staili yake peke yake, kumbuka gitaa lake katika wimbo Asha, au Dada Lemmy. Charles Kazembe akiwa na Morogoro Jazz anakumbukwa katika upigaji wa rythm kwenye nyimbo kama Wajomba Wamechacha. Hao ni wachache tu kulikoweko na wengi marufu. Katika kipindi hiki huko Zaire kulikuwa na mipigo mbalimbali ya gitaa la rythm, ila kitu kipya kikaanzishwa ambapo katika ufungaji wa nyuzi ,wapiga rythm wakauondoa uzi namba nne katika gitaa hilo na kuweka uzi namba moja, hivyo kukawa na nyuzi namba moja 2 katika gitaa moja, hapo ndipo akina Vata Mombasa wakaweza kuleta utamu mpya katika upigaji wa rythm, ufungaji wa aina hii wa nyuzi za gitaa ulifahamika kama 'double string'. Wakati huo Orchestra Kiam wakawa wanajivunia kupiga rythm kwa spidi kali sana,vibao kama Kamiki, Bomoto ni ushahidi wa kazi hizo. Utamu wa ufungaji wa nyuzi kwa staili hii uliweza kusikika vizuri katika gitaa lililopigwa mwanzo kabisa wa wimbo Andoya. Umuhimu wa gitaa la rythm ulikuwa ukionekana kwa bendi nyingi kuwa na mtindo wa 'kuachia rythm', huo ulikuwa ni mpangilio ambapo gitaa la rythm liliachwa lipige peke yake wakati magitaa mengine yakiwa kimya. Hapo mpiga rythm aliachiwa kucheza na gitaa alivyotaka na kuonyesha umahiri wake wote. Mtindo huu ulipendwa sana na wapenzi wa muziki. Utaratibu huu umerudi kwa njia ya ajabu sana, bendi nyingi za taarab vimeanza 'kuachia rythm' lakini kwa kuwa bendi hizo hazitumii tena gitaa la rythm , jukumu hili linafanywa na mpiga solo, tena vipande vingi vinavyopigwa ni vile vilivyopigwa na bendi za zamani!! matokeo ni yaleyale, wapenzi wa muziki hupanda mzuka na kucheza sana wakati wa kipindi hicho.
Kwa ujumla bendi nyingi za dansi hazitilii umuhimu tena gitaa la rythm. Kinanda kimechukua nafasi ya gitaa hili. Kuna bendi ambazo zinalo gitaa la rythm lakini kwa mfumo wa sasa wa muimbaji kuchukua nafasi kubwa ya wimbo gitaa hilo limerudishwa nyuma sana. Lakini kwenye muziki kila kitu kina utamu wake kamwe chombo kimoja hakiwezi kuziba pengo la chombo kingine.
No comments: