Saturday, July 1, 2017

MSICHANA NDOTONI MWANGU.....1 TO 11


GENEVIEVE aliwaangalia watoto wake mapacha na kujikuta akitabasamu, ujio wao duniani ulifuta machozi yake na kumuondolea aibu ya kuitwa mwanamke tasa kila alikokwenda. Alipoikumbuka safari ndefu aliyosafiri kuwatafuta watoto hao ghafla huzuni ikamuingia na kujikuta akilengwalengwa na machozi.

Kabla hajaendelea sana na mawazo hayo mlango wa chumba ulifunguliwa, mume wake Phillip akatokeza nje akiwa amevaa shati lake jeupe, tai ya rangi ya kahawia na suruali iliyonyoshwa vizuri pamoja na viatu vilivyong’arishwa vyema, begani mwake alikuwa na begi la kompyuta yake ndogo.

“Nini tena?”
“Basi tu.”
“Basi tu nini?”
“Yaani kila siku ninapowaangalia Dorice na Dorica siamini kama hatimaye na mimi nina watoto tena wazuri kiasi hiki, badala ya kufurahi huwa naishia kuingiwa na huzuni.”

“Mwaaa!” Phillip alimbusu mkewe kwenye paji la uso huku akitabasamu.
“Asante.”
“Usijali darling, ni jambo la kumshukuru Mungu. Usiiangalie sana historia, wewe furahia kwamba hatimaye sasa tuna watoto na leo wanakwenda kuanza darasa la kwanza kwa mara ya kwanza.”

Phillip aliongea kwa sauti ya upole huku wote wawili wakiwaangalia watoto wao wazuri wa kike mapacha wakiwa wamekaa kwenye meza wakinywa chai, tayari walikuwa na miaka mitano, walikuwa na hamu kubwa ya kufika shuleni kuanza darasa la kwanza baada ya kusoma chekechea kwa miaka miwili.

“Daddy!” Dorice alimuita baba yake.
“Yes, darling.”
“Guess what?” (Hebu buni kuna nini?)
“What is it my sweetie!” (Nini mpenzi wangu?)
“Today we are going to school!” (Leo tunakwenda shule.)

“I know darling, make sure you do good in writing, reading and counting, okay?” (Najua mpenzi wangu, hakikisheni mnafanya vizuri kwenye kuandika, kusoma na kuhesabu, sawa?)
“Yes daddy, I am going to be the first and Dorica the second.” (Sawa baba, mimi nitakuwa wa kwanza na Dorica wa pili.)

“No! I will be the first and you the second.” (Hapana! Nitakuwa wa kwanza halafu wewe wa pili.) Dorica alijibu.
Genevieve na Phillip wakacheka kwa sauti kisha kunyanyuka kwa pamoja mahali walipoketi kwenda kuwakumbatia watoto wao, wakawabusu na hapohapo kuanza kusali wakiwaombea wafanye vizuri shuleni.

Zoezi hilo lilipomalizika, Phillip aliwaaga wote na kuwatakia siku njema kisha kutoka hadi nje ambapo aliingia ndani ya gari lake na kuondoka akiamini saa mbili kamili ikifika mke wake angewachukua watoto hadi barabarani ambako basi la shule lingepita na kuwabeba.

Waliishi Upanga karibu kabisa na eneo la katikati la jiji la Dar es Salaam, lakini ofisini kwa Phillip ilikuwa ni maeneo ya Victoria kilomita kama ishirini hivi kutoka katikati ya jiji. Wakati watu wengi waliteseka kwenye msongamano wa magari asubuhi kwenda kazini sababu ofisi nyingi zilikuwa katikati ya jiji, yeye hakuelewa hata kama kulikuwa na msongamano, alipishana nao asubuhi akielekea kazini nje ya jiji.

Baada ya kuingia tu ndani ya gari lake aliendesha kwa kasi ya kawaida akiwahurumia watu wa upande wa pili wa barabara ambao magari yao yalikuwa yamesimama bila hata kusogea mbele, kichwani mwake aliwaza sana juu ya watoto wake wa pekee Dorice na Dorica, wao ndiyo waliomfanya afanye kazi kwa nguvu sana kwa sababu hakutaka wapate shida maishani mwao.

Katika umri wa miaka mitano tu tayari kila mmoja kwenye akauti yake ya Jumbo kwenye Benki ya CRDB alikuwa na kiasi cha milioni nane ambazo Phillip na mke wake walipanga kuendelea kuziongeza wakiwa wamedhamiria zifike milioni mia moja kwenye kila akaunti ya kila mtoto watakapokuwa na umri wa miaka kumi na minane.

Mawazo hayo aliendelea nayo mpaka alipokuwa anakata kona kuingia ofisini kwake ambako aliegesha na kushuka, kabla hajaondoka simu yake ya mkononi ikalia, akifunga mlango aliibana kwa bega sikioni na kuanza kusikiliza taratibu akiwa bado hajaelewa ni nani aliyempigia kwani namba haikuonyesha jina bali maandishi “Call” peke yake ndiyo yaliyoonekana, ishara kuwa simu hiyo ilitoka nje ya nchi.

“Naongea na Phillip?”
“Ndiyo, nani mwenzangu?”
“Huhitaji sana kufahamu jina langu, ila nimekupigia kukutaarifu kuwa kama kuna uwezekano naomba usiwapandishe watoto wako kwenye basi la shule, kuna bomu limetegwa ndani yake litalipuka muda mfupi tu wakishapanda, watakufa hapo hapo! Nimekupigia kwa sababu najua ni kiasi gani unawapenda watoto wako.” simu ikakatwa.

Mwanzoni Phillip alidhani labda siku hiyo ilikuwa ni tarehe moja mwezi wa Nne, Siku ya Wajinga Duniani lakini alipoangalia saa yake mkononi alikuta ilikuwa ni tarehe tofauti. Upande mmoja wa moyo wake ukamwambia apuuze maneno hayo lakini upande mwingine ukamtaka ampigie simu mkewe haraka iwezekanavyo na kumsimulia habari hiyo ya kuogofya.

Simu iliita sana lakini haikupokelewa, akaendelea kupiga tena na tena lakini hali ilikuwa hiyo hiyo. Akathibitisha haikuwa tabia ya Genevieve kutopokea simu yake hasa alipopigiwa na mume wake maana hawakuwa na tabia ya kupigiana simu zisizo na maana, hii ilimfanya Phillip aingie ndani ya gari lake haraka na kugeuza akiwa amepuuza hata muda wa kuwahi kazini, kwake familia kilikuwa kitu cha kwanza.

Haraka akaanza kuendesha kuelekea mjini, hakwenda umbali mrefu akakutana na msongamano wa magari ambao wala ulikuwa hausongi mbele. Kwa mkono wa kuume akiwa ameshika usukani na kwa mkono wa kushoto simu ikiwa sikioni akiendelea kuwasiliana na Genevieve bila mafanikio, bado simu ilikuwa haipokelewi.

Alipofika maeneo ya Morocco aliamua kuiingiza gari yake kwenye kituo cha mafuta cha Bonjour, kando tu mwa kibanda ambacho hutumika kuuza baga, akashuka haraka na kukimbia upande wa pili ambako alimkodisha mtu wa Bajaj aliyekuwa akipita na kumtaka amwahishe haraka sana mjini.

Akiwa ndani ya Bajaj aliendelea kupiga simu huku wasiwasi wake ukiendelea kuongezeka, isingewezekana mke wake muda wote huo awe mbali na simu. Hakumpata Genevieve na Bajaj ilikuwa ikienda kwa mwendo mdogo sana, alipofika eneo liitwalo Mbuyuni alilazimika kumlipa dereva wa Bajaj ujira wake, akashuka na kukodisha pikipiki hiyo ndiyo ilimpeleka moja kwa moja hadi nyumbani kwake.

“Genevieve! Genevieve!” Aliita akigonga mlangoni lakini hakuitikiwa na mlango ulikuwa umefungwa.
Akaendelea kupiga simu, alipousikia mlio kutoka ndani tena sebuleni, alielewa mke wake alikuwa ameisahau simu ndani na kupeleka watoto barabarani. Haraka akarukia juu ya pikipiki na kumwamuru dereva aondoke kwenda barabarani mahali ambapo basi la shule hupita kuchukua wanafunzi.

Walipokaribia eneo hilo aliliona gari la mke wake likiwa limeegeshwa kando ya barabara, yeye mwenyewe akiwa amesimama nje akiliangalia gari la shule likiondoka mwendo wa taratibu, tayari Phillip akawa amefika na kuruka kwenye pikipiki. Genevieve alipomuona alishituka sana.

“Nini tena?”
“Watoto wako wapi?”
“Wako kwenye gari la shule.”
“Mungu wangu!”
“Nini?”

Phillip akadandia tena pikipiki na kumwamuru dereva aanze kulifuata basi la shule wakimwacha Genevieve mahali alipokuwa, hawakwenda mbali sana, gari likiwa umbali wa kama mita hamsini kabla hawajalifikia, walisikia kishindo cha ajabu “Puuuuuu”. Wakaanguka chini, gari la wanafunzi lilikuwa limelipuliwa na bomu.

Je, nini kitaendelea? Nani amefanya unyama huu? Dorice na Dorica wamekufa?

MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.2.


Ilikuwa ni familia yenye furaha, Genevieve na mume wake Phillip wakiwa na watoto wao mapacha Dorice na Dorica, watoto wa kike wenye sura za kuvutia ambao walifanana kupita kiasi. Ilikuwa ni kazi ngumu hata kwa wazazi wao kuwatofautisha.

Watoto hawa ndiyo walikuwa mzizi wa furaha ndani ya nyumba ya Genevieve na Phillip. Waliwapata kwa taabu mno, ndiyo sababu waliwapenda kupita kiasi. Asubuhi hii ya leo, Dorice na Dorica wakiwa na umri wa miaka mitano ndiyo wanapelekwa kwa mara ya kwanza shuleni kuanza darasa la kwanza baada ya kusoma chekechea kwa muda wa miaka miwili.

Phillip ameamka asubuhi na kujiandaa kwa ajili ya kwenda kazini huku mke wake ambaye tangu ajifungue watoto hawa alikuwa mama wa nyumbani, aliwaandaa Dorice na Dorica tayari kwa shule. Phillip akampiga mke wake busu, vivyo hivyo watoto na kuwaaga akifahamu mke wake angewapeleka barabarani ambako wangechukuliwa na gari la shule muda ukifika, akaondoka zake kuelekea kazini.

Waliishi Upanga lakini kazini kwa Phillip ilikuwa ni maeneo ya Victoria, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam hivyo yeye hakuwa na msongamano wa magari kuelekea kazini kwani wengi walielekea mjini kila asubuhi.

Akiwa nje ya jengo la ofisi yake, simu yake ililia, akaipokea na kuongea na mtu aliyekuwa akipiga kutoka nje ya nchi. Hakuwa tayari kutaja jina lake, akampa taarifa kuwa ikiwezekana wasiwapakie watoto wao ndani ya gari la shule kwani lingelipuliwa kwa bomu.

Mwanzoni Phillip alidhani ni utani lakini alipoamua kumpigia simu mke wake, ikawa inaita bila kupokelewa, moyoni akaingiwa na wasiwasi hivyo kuamua kugeuza kuelekea nyumbani ili amuwahi kabla hajawapeleka watoto barabarani kupanda basi la shule.

Haikuwa rahisi, kwani pamoja na kuliacha gari lake na kukodisha Bajaj ambayo pia aliiacha na kukodisha pikipiki, alifika nyumbani na kumkosa mke wake, aliamua kumfuata barabarani ambako alikuta basi ndiyo kwanza limeondoka. Akamwamuru mwenye pikipiki alifuatilie kwani halikuwa mbali, lengo likiwa ni kuwashusha watoto.

Walipolikaribia basi hilo, ikiwa ni mita chache tu walisikia mlipuko mkubwa, basi lilikuwa limelipuliwa na bomu.
Je, nini kitaendelea? Nani kafanya unyama huu? Kwa nini? SONGA NAYO…

Mlipuko huo uliwafanya Phillip na mwendesha pikipiki waanguke kando ya barabara, fahamu za Phillip zikapotea. Alipozinduka alijikuta kitandani, mkononi akiwa na dripu iliyodondosha matone kwa haraka kuingiza kwenye mishipa yake. Awali hakuelewa ni kwa nini alikuwa pale lakini alipotulia ndipo akakumbuka picha nzima ya tukio la kulipuka kwa basi lililobeba wanafunzi, wakiwemo watoto wake Dorice na Dorica.

“Mamaaaaa! Watoto wanguuu! Nani amefanya kitendo hiki? Nitamjua,” aliongea kwa sauti ya juu huku akilia, wauguzi wakafika haraka na kuanza kumtuliza.

Faraja zao hazikusaidia, alitaka aoneshwe mahali mke wake Genevieve alipokuwa. Wauguzi hawakuwa tayari, moyoni akaingiwa na wasiwasi kuwa huenda hata yeye alikuwa marehemu. Phillip akiwa kama mtu aliyechanganyikiwa, alinyanyuka kitandani na kusimama wima, dripu ikachomoka.

Hakutaka kuongea kitu kingine zaidi, akatoka kuanza kukimbia kuelekea barabara ya Umoja wa Mataifa, karibu kabisa na Shule ya Al-Muntazir, ambako basi lililobeba wanafunzi lililipukia. Mbele kidogo alisimamisha gari ambalo kwa juu liliandikwa “Taxi”, likaegesha pembeni naye akaingia na kuketi kiti cha mbele kando ya dereva aliyemwangalia kwa jicho la wasiwasi.

“Wapi braza?”
“Pale chini.”
“Wapi?”
“Wewe twende.”

“Nipe kabisa changu,” dereva alisema baada ya kuhisi abiria wake asingemlipa kwani alionekana ni mtu aliyechanganyikiwa.
“Shilingi ngapi?”
“Niambie kwanza unakwenda wapi.”

“Kwenye basi lililolipukiwa na bomu.”
“Ahaa! Shilingi elfu moja.”
Phillip akaingiza mkono mfukoni na kukuta bahati nzuri pochi yake ilikuwepo, akaitoa na kuchomoa noti ya shilingi elfu kumi na kumkabidhi dereva wa teksi. Safari ikaanza kuelekea Al-Muntazir, mbele kidogo walikuta msongamano wa magari, barabara ilikuwa imefungwa kwa sababu ya ajali hiyo.

Phillip akashuka bila hata kudai chenji yake na kuanza kukimbia kwenda mbele. Mtu yeyote aliyemwona lazima alijua akili yake haikuwa sawa, hakujali, akazidi kukimbia akimfikiria mke wake na pia watoto wake. Kila kitu kilichotokea kwake kilikuwa ni ndoto, isingewezekana hata kidogo watoto wake wazuri, tena mapacha, waliofanana kila kitu kwa sura kuwa wamekufa ghafla kiasi hicho?

Alijiuliza bila kupata majibu akiamini muda si mrefu angezinduka ili amsimulie mke wake Genevieve ndoto hiyo, lakini ukweli haukubadilika. Alifika eneo la tukio na kukuta magari ya zimamoto na mamia ya watu wakiwa wamekusanyika kushuhudia kilichotokea. Lilikuwa tukio baya na polisi walikuwa kila mahali wakizuia watu kupita.

Hawakuweza kumzuia Phillip ambaye alipenya mpaka mbele na kuanguka chini akilia baada ya kuyaona mabaki ya watoto wazuri waliokufa kinyama, kiatu kimoja cha Dorica alikitambua, pia chupa ya chai ya Dorice aliyowekewa maziwa na mama yake ilikuwa juu ya lami.

Miili ya watoto wote ilikuwa imelazwa juu ya ardhi ikiwa imefunikwa na mashuka meupe, haikuwa rahisi hata kidogo kuitambua kwani iliharibika kupita kiasi. Phillip akanyanyuka na kuanza kuzunguka kwenye miili hiyo akifunua ili angalau aweze kuwaona watoto wake. Hapakuonekana mwili wa Dorice au Dorica, miili iliyokuwepo ilikuwa imesambaratishwa na kubaki kiungo kimoja kimoja.

“Nani amefanya unyama huu? Nitamjua, sitarudi kazini mpaka siku nitakapomtia mikononi mwangu,” alijisemea Phillip akilia, kisha akakaa chini na kuanza kuiangalia miili hiyo huku akimfikiria mke wake Genevieve ambaye mpaka wakati huo alikuwa hajamwona.

Siku iliyoanza vizuri hatimaye ilikuwa imeharibika, watu walikuwa wakilia kwa uchungu mkubwa, lilikuwa ni tukio baya kuliko jingine lolote kutokea. Phillip hakuwa tayari kuongea na waandishi wa habari walipomfuata. Tayari wazazi wa watoto wote waliokufa walikuwa eneo hilo, vilio vilienea.

Baadaye miili ilianza kubebwa na kuingizwa kwenye gari tayari kupelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Muhimbili. Phillip aliamua kutangulia huko ili akaone mahali ambapo watoto wake wangelazwa. Alifika wakati magari yameshawasili, watu wengi wakiwa wamekusanyika na wafanyakazi wenzake ambao tayari walishapata habari walikuwepo kumfariji lakini alikuwa hafarijiki.

“Jamani nisaidieni kujua mahali mke wangu alipo,” aliwaomba.
Badala ya kumjibu au kusema chochote, wafanyakazi wenzake walikaa kimya, jambo lililoonesha kabisa walikuwa na kitu moyoni. Wasiwasi wa Phillip ukaongezeka, hakuelewa maisha yake yangeendeleaje bila kuwa na familia. Alikitamani kifo kama ingethibitika kuwa, watu wote aliowapenda hawakuwepo duniani.

“Jamani niwaulize kama mnaweza kuwa mnafahamu mahali aliko Genevieve.”
“Tunajua lakini...”
“Lakini nini jamani, hebu nielezeni tu mahali aliko mke wangu, amekufa? Kwa mshtuko huu ukizingatia ana shinikizo la damu, anaweza kuwa amenitoka.

Nitafanyaje mimi? Nitaishije mimi? Eee Mungu, ni kwa nini umeruhusu nipite kwenye jambo hili wakati unaelewa moyo wangu ni mdogo?” Aliuliza maswali mengi akiwa ameshikiliwa na wafanyakazi wenzake walioonekana kuwa na siri nzito mioyoni mwao.
 MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.3.

Familia yenye furaha, ya Phillip na mke wake Genevieve pamoja na watoto wao mapacha, Dorice na Dorica inapatwa na balaa ambalo hawakuwahi kulitegemea maishani mwao.

Watoto hawa wawili waliokuwa mzizi wa furaha yao, baada ya kuhangaika kwa muda mrefu kuwapata wanasindikizwa na mama yao kwenda stendi ya basi ambako wanapanda basi la kuwapeleka shule; ni siku ya kwanza shuleni wakiwa darasa la kwanza baada ya kusoma chekechea na kumaliza.

Phillip aliamka asubuhi na kuwapiga busu watoto wake wote wawili pamoja na mkewe, kisha kuondoka kuelekea kazini. Alipoegesha tu gari lake nje ya jengo la ofisi yao, simu yake ililia, akaangalia kwenye kioo na kukuta pameandikwa neno “Call” bila kuonyesha namba, akajua namba hiyo ilitoka nje ya nchi. Haraka akaipokea.

Sauti aliyokutana nayo ilikuwa ya kukwaruza, ikimtaarifu kuwa kama kuna uwezekano asiwapandishe watoto wao kwenye gari la shule kwani kulikuwa na bomu lililotegwa ndani yake ambako lingelipuka wakati wowote na kuua watu wote waliokuwa ndani yake.

Awali alizichukulia taarifa hizo kama utani, lakini baadaye akaamua kumpigia simu mke wake ili ampe taarifa hiyo asiwapeleke watoto kwenye gari la shule. Simu iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa, akaendelea tena na tena, hali ikawa ileile. Mwisho akafikia uamuzi wa kuendesha gari kurejea nyumbani.

Hakwenda mbali sana kabla hajakutana na msongamano mrefu wa magari, akaamua kuliegesha la kwake pembeni na kuchukua Bajaj ambayo nayo ilishindwa, akalipa kisha kushuka na kuchukua pikipiki iliyomfikisha hadi nyumbani ambako hakumkuta mke wake ingawa simu iliiita kutoka chumbani.

Akalazimika kumwamuru mwendesha pikipiki ampeleke hadi stendi ambako walimkuta mke wake akiliangalia gari lilivyoondoka, akashituka kumwona Phillip pale wakati alishaondoka kwenda kazini. Akawaulizia watoto, jibu alilopewa ni kwamba wameondoka na gari lililokuwa mita kama hamsini hivi kutoka waliposimama, Phillip akamwamuru mwendesha pikipiki alifuate.

Kabla hawajalifikia gari hilo lililipuka vibaya, Phillip akazimia, alipozinduka alikuwa hospitali na kuondoka kurejea eneo la tukio ambako alikuta polisi wamekwishafika na magari ya zimamoto. Miili ya watoto iliyosambaratishwa kiasi cha kutokutambulika ilikuwa ikiondolewa kwenye gari lililowaka moto na kupelekwa chumba cha kuhifadhia maiti.

Phillip akalia kwa uchungu na kuamua kufuatilia hospitalini, huko aliendelea kulia akiuliza ni wapi mke wake alipokuwa. Lilikuwa tukio la kusikitisha, siku iliyoanza vizuri sasa ilibadilika na kuwa mkosi.
Je, nini kitaendelea? Nani amefanya unyama huu? Yuko wapi mke wa Phillip? SONGA NAYO…

Wafanyakazi wenzake waliomzunguka wakiwa wamemwekea mikono mabegani na kumbembeleza ili asimame imara kama mwanaume katika kipindi hicho kigumu, hawakuwa na la kufanya aliposisitiza aonyeshwe mke wake. Wote walimuonea huruma, mmoja wao akaondoka hadi ofisini kwa daktari aliyempokea Genevieve alipofikishwa hospitali kutoka eneo la ajali.

“Hakuna shida mpelekeni tu.” Alijibu Dk. Anorld Mapunjo.
“Asante daktari, sisi tulikuwa tunaogopa kwa kudhani pengine tunaweza kumsababishia matatizo yale yale pia.”

“Haina tatizo, kama ameweza kustahimili mshituko uliompata baada ya kuona gari linalipuka, hakuna kinachoweza kumletea matatizo tena. Si alikuwa amelazwa wodi ya Mwaisela?”
“Ni kweli lakini aliporejewa na fahamu, aliondoka hospitalini hadi eneo la tukio, huko ndiko tulikokutana naye.”

“Mpelekeni tu.”
Reginald, rafiki mkubwa wa Phillip waliyefanya naye kazi kitengo cha uhasibu alirejea mahali alipowaacha wenzake na kuwapa taarifa ya daktari, wakaondoka pamoja hadi kwenye jengo lililoandikwa mlangoni Muhimbili Intensive Care Unit, kando kukiwa na maneno ya Kiswahili; Kitengo cha Wagonjwa Mahututi. Wakagonga mlangoni, muuguzi akafungua mlango.

“Sista samahani.”
“Bila samahani.”
“Tumemleta huyu kaka ni mume wa Genevieve.”
“Karibuni.”

Huku akibubujikwa machozi na mwili wake kutetemeka, Phillip aliongozwa na rafiki zake akiwa ameshikiliwa kila upande na kuingizwa ndani ya jengo hilo na kuongozwa hadi kwenye chumba kilichokuwa kando, mlango ukafunguliwa tena na wote wakaingia ndani. Macho yake yakaenda moja kwa moja kitandani; Genevieve alikuwa amelala hapo akiwa hajitambui.

Uso wake ukiwa umefunikwa na tabasamu kama vile alikuwa amelala macho yake yakiwa yamefungwa akikoroma na kuhangaika kuhema ingawa alikuwa akitumia mashine.

Uchungu mkali ukauchoma moyo wa Phillip na machozi mengi yakamtoka, nguvu zikamwishia miguuni na kujikuta anaketi chini moyoni mwake akiilaani siku hiyo, kwamba haikustahili kabisa kuwemo katika orodha ya siku za dunia, ilikuwa mbaya na asingeisahau maisha yake yote.

Nusu saa baadaye alijikakamua na kusimama wima, akasogelea kitanda na kuinamisha kichwa chake mpaka karibu kabisa na shavu la Genevieve, matone ya machozi yakadondoka kutoka kwenye ncha ya pua yake na kutua shavuni kwa mkewe. Mdomo wake ukamgusa shavuni, bila kuchelewa akampiga busu na Genevieve akatoa tabasamu la siku zote.

Phillip alikuwa bado haamini kilichotokea, isingewezekana hiyo iwe kweli, alihisi labda alikuwa akiota ndoto au kuangalia sinema fulani ya kutisha iliyochukua kabisa hisia zake. Huo uliendelea kubaki ukweli akimwangalia Genevieve kitandani na kuwafikiria watoto wake waliosambaratishwa na mabomu, hasira ikapanda, akamchukia mtu aliyefanya hivyo na kutamani kukutana naye ana kwa ana.

“Mke wangu, naomba usife, baki hai ili tumtafute pamoja mtu aliyefanya unyama huu wa kuwateketeza watoto wetu tuliowapenda kuliko kitu kingine chochote. Kama utakufa, basi tangulia ili mimi niikamilishe hii kazi.
Nakupenda Genevieve.” Phillip aliongea kwa sauti ya upole, watu wote waliokuwemo chumbani wakajikuta wanachukua vitambaa vyao na kujifuta machozi, ilikuwa ni taswira mbaya mno kuishuhudia.

Genevieve alikuwa amelala kitandani akiwa hajitambui, mashine ndiyo zilimsaidia kuhema na hata moyo wake kupiga. Pamoja na hali hiyo bado urembo wake ulionekana wazi, hakika alikuwa msichana mzuri kupindukia. Hakuna mwanaume angemuona akaacha kutamani kuwa naye maishani, wengi walikuja kwake kabla, lakini aliyekuwa na bahati hiyo ni Phillip peke yake.

Kichwani mwa Phillip kuliendelea mawazo mengi, aliikumbuka tangu siku waliyokutana mara ya kwanza maeneo ya Posta jijini Dar es Salaam na kushangaa kama kweli msichana ambaye siku zote alimuota katika ndoto kumbe alikuwepo katika ulimwengu halisi, kabla hajaendelea sana na mawazo hayo mlango ukafunguliwa, akaingia Dk. Mapunjo akiongozana na mwanaume mrefu aliyenyoa mtindo wa panki.

“Karibu baba, pole sana, tumepata tatizo kubwa, watoto wetu wote wamekufa na mke wangu yuko taabani hapa kitandani.” Phillip aliongea akikumbatiana na mwanaume huyo.
“Usijali mwanangu, ndiyo dunia!”

Alikuwa ni mzee Mpangal Anthony, mzazi wa Genevieve. Taarifa za kulipuka kwa bomu, vifo vya watoto na kuanguka kwa mwanaye na kupoteza fahamu alizipata akiwa nyumbani kwake maeneo ya Mbezi Beach na kuamua kwenda hospitalini kushuhudia mwenyewe. Pamoja na utu uzima wake, akiwa ameshuhudia mambo mengi duniani, kitendo cha kumwona amelala kitandani akiwa taabani, kilimfanya ashindwe kujizuia; machozi yakamtoka.

“Mzee Mpangal, jikaze, tunakutegemea wewe ututie nguvu.” Ilikuwa ni sauti ya Dk. Mapunjo.
“Inauma daktari.”
“Pole sana.”

Phillip alihisi kuchanganyikiwa, alishindwa kuelewa aumizwe na kipi; kufa kwa watoto wake ama hali mbaya ya mke wake kitandani. Alijisikia kama vile amesimama katikati ya mawe mawili makubwa yote yakitaka kumgandamiza yeye. Ilikuwa ni lazima asimame imara; vinginevyo angeweza kukatisha uhai wake. Hili liliwafanya ndugu wakae naye karibu muda wote.

Hakuondoka wodini tangu alipoingia, muda wote alikuwa pembeni ya kitanda cha mke wake, hakupata hata lepe la usingizi au kufumba jicho kwa siku tatu mfululizo akiangalia kama Genevieve angefumbua macho yake, hilo ndilo jambo alilolisubiri kwa hamu kubwa.

Baadaye alipata taarifa za ndugu zake wakiongozwa na Mzee Mpangala kukabidhiwa mabaki ya watoto wake kwa ajili ya mazishi, lakini habari zikasambaa kwamba ndugu waligawiwa vipande vilivyopatikana ili wakazike majumbani kwao bila uhakika kama kweli waliomchukua ni ndugu yao. Haukuwepo uwezekano wa kupima vinasaba vya DNA.

“Baba naomba msizike mpaka mke wangu azinduke, najua Genevieve atazinduka ili aweze kushuhudia mazishi ya watoto wake.” Phillip aliongea kwa simu na mzee Mpangal huku akibubujikwa na machozi.

“Lakini hali ni mbaya. Nashauri tuzike, Genevieve akirejewa na fahamu tutamwambia kilichotokea, bila shaka ataelewa.”
“Hapana baba, nataka mke wangu ashuhudie watoto wake wakizikwa.”


MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.4.

Juhudi zote za Mzee Mpangal kuhakikisha mabaki ya watoto yanazikwa ziligonga mwamba, Phillip aliendelea kusisitiza mke wake ni lazima azinduke na kuwashuhudia wapendwa wake Dorice na Dorica wakizikwa.
Mzee Mpangal alishindwa tu kumueleza ukweli kuwa hata mabaki waliyopewa hakuwa na uhakika kama kweli walikuwa ni wajukuu zake, maana alikabidhiwa viwiliwili vya watoto bila kichwa wala miguu.
Hakutaka kabisa mwanaye ashuhudie picha hiyo lakini Phillip alipong’ang’ania ilibidi mzee atulie na kusikiliza maamuzi ya mzazi, mabaki yakarejeshwa tena chumba cha kuhifadhia maiti kusubiri Genevieve azinduke ndipo mazishi yafanyike.

Phillip aliendelea kubaki wodini, karibu kila siku akilia, ulikuwa ni msiba mkubwa mno kwake. Juhudi za marafiki kumfariji zilikuwa zimeshindikana, alikuwa kando ya kitanda cha mke wake akiangalia kila kilichoendelea, ndani ya masaa ishirini na sita tu tangu mlipuko utokee alikuwa amepoteza uzito mkubwa sana wa mwili wake.

Kichwani mwake yaliendelea maswali mengi yasiyo na majibu, nani alilipua basi? Kwa nini aliua watoto wasio na hatia? Je, kama kilikuwa ni kisasi mkosaji alikuwa ni yeye au wazazi wa watoto wengine? Moyoni akatamani kukutana na mtu aliyefanya ukatili huo bila kujali alikuwa analipa kisasi kwa nani. Ilikuwa ni lazima afahamu ukweli siku moja hata kama gharama ingekuwa ni uhai wake mwenyewe.

“Tatizo Genevieve, angekuwa mzima hivi sasa ningekuwa nimeshapanga namna ya kumtafuta mtu huyo mbaya… hata hivyo ipo siku ataingia mikononi mwangu.” Alisema akijifuta machozi.
Usiku na mchana alikuwa macho, mara nyingi akimwangalia Genevieve aliyekuwa akipumua kwa msaada wa mashine huku akikoroma, madaktari walisema shinikizo lake la damu lilikuwa juu sana na lilikuwa limegoma kabisa kushuka, mshituko alioupata ndiyo uliosababisha hali hiyo.

Alfajiri ya siku ya nne ndipo alipoliona tabasamu la mke wake lililokuwa limepotea, hakuamini kama kweli macho yake yalikuwa yakimpa usahihi wa alichokiona. Ikabidi asogee karibu na kuthibitisha, moyo wake ukajaa furaha, akapiga magoti chini na kusali akimshukuru Mungu. Ghafla Genevieve akafumbua macho na kuangalia kila upande kama mtu aliyekuwa akijaribu kutambua mahali alipokuwa.

“Genevieve! Genevieve!” Akaita lakini hakuitikia.
Haraka akatoka akikimbia mpaka kwenye chumba cha wauguzi ambao aliwapa taarifa ya kilichotokea, nao katika hali ya kutokuamini wakaungana naye kukimbia hadi chumbani. Wakamkuta Genevieve amekaa kitandani kama vile hakuwa taabani muda mfupi tu uliopita, Phillip akaingiwa na furaha ambayo maelezo yake hayakuwepo, hali iliyosababisha machozi zaidi kumbubujika kwani kilichotokea kilikuwa ni muujiza.

“Genevieve! Genevieve mke wangu, mimi ni Phillip, unanisikia?” Aliuliza lakini mke wake aliendelea kuwa kimya.
“Mpigie simu Dk. Mapunjo umpe taarifa hii, mmoja wa wauguzi alisema.
“Sawa acha nikampigie,” alijibu na kuondoka akikimbia, ingawa alivaa raba zilisikika vizuri sakafuni wakati akitimua mbio kuelekea ofisini.

Baada ya muuguzi kuondoka, Phillip aliendelea kumwita mke wake lakini hali ilikuwa ni ile ile, hakuitika na aliendelea kuangaza huku na kule kama vile wafanyavyo watu wenye ulemavu wa kuona. Dakika ishirini baadaye muuguzi alirejea akiongozana na Dk. Mapunjo, alipomtazama Genevieve alifurahi na kuanza kumfanyia vipimo mbalimbali, akathibitisha kabisa kwamba shinikizo lake la damu lilikuwa limeshuka kufikia kiwango cha kawaida.

“Sasa kwa nini namwita haitiki na hata nikimsogezea kidole machoni ingawa amefumbua macho hapigi kope?”
“Hilo ndilo tatizo ambalo nimeligundua, mkeo amepatwa na tatizo jingine ambalo limetokana na shinikizo la damu kupanda sana, hivyo kuharibu vituo kwenye ubongo vinavyohusika na kuona pia kusikia, ni habari ya kusikitisha lakini ni bora nikwambie ukweli kwamba mkeo hataweza kuona wala kusikia tena maishani mwake.”
“Mungu wangu!” Phillip alisema kwa huzuni.

Hakuweza hata kusimama, akasogea pembeni kwenye kiti na kuketi kisha kuinamisha kichwa chake katikati ya magoti. Machozi yakaanza kudondoka taratibu na kulowanisha sakafu huku akiupitia mchakato mzima wa maisha yake, tangu alipozaliwa mpaka siku hiyo akiwa amefiwa na watoto wake wote kwenye mlipuko wa bomu ambao miili yao ilikuwa bado imehifadhiwa chumba cha maiti na sasa alikuwa amepokea taarifa kuwa, mke wake angekuwa kipofu na kiziwi maisha yote.

Zilikuwa habari mbaya za kutosha kabisa mtu mwingine kufikiria kukatisha uhai wake. Phillip hakuuona huo kama uamuzi wa busara, asingeweza kujiua na kumwacha mke wake akiteseka, isitoshe alikuwa na kazi nzito ya kumtafuta mtu aliyetega bomu ndani ya basi na kuwaua pamoja na watoto wa wazazi wengine.

Huyo ndiye aliyekuwa adui yake mkubwa, hakutaka kumwacha duniani akila starehe wakati aliwasababishia watu wengine uchungu, akaapa kumsaka kwa udi na uvumba kila kona ya dunia mpaka amtie mkononi. Ni kweli hakuwa mpelelezi lakini sasa ilimlazimu kuifahamu kazi hiyo ili aweze kukamilisha kazi yake kwa heshima ya watoto na mke wake.

“Dorice! Dorica! Leteni viatu vyenu niwavalishe ili niwapeleke shule, leo ni siku ya kwanza ya darasa la kwanza, hamjafurahi? ” Genevieve alitamka maneno yaliyoonesha kabisa hakuwa na taarifa hata ya mahali alipokuwa na hakujua kilichotokea maishani mwake, moyo wa Phillip ukaumia zaidi.

***
Militon Lukinda alipandisha kwa kasi, alikuwa hatarini kuchelewa kikao cha asubuhi hiyo ambako yeye na wenzake Jacob Mkonyi na Albert Shitugugu walikuwa na kazi ya kuwakilisha taarifa walizozipata kwenye eneo la tukio ambako bomu lililipuka.Vijana hawa watatu ndiyo walikuwa na mwezi mmoja tangu warejee kutoka Houston, Texas, Marekani walikokwenda kuchukua kozi ya uchunguzi wa eneo ilipofanyika jinai, kwa lugha ya Kiingereza iliitwa Crime Scene Investigation.

Serikali ya Tanzania iliamua kuwapeleka vijana hao kusomea elimu hiyo ili waweze kusaidia kwenye matukio mbalimbali ya ulipuaji wa mabomu yaliyojitokeza kwa sababu ya ugaidi. Hii ilikuwa ni baada ya Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania kulipuliwa na mtandao wa kigaidi wa Al Qaeda.

Kazi yao ya kwanza tangu waingie nchini wakiwa na elimu ya kutosha ilikuwa ni mlipuko wa basi la wanafunzi, lililoteketeza jumla ya watoto kumi na nane waliokuwa wakipelekwa shuleni. Muda mfupi tu baada ya mlipuko huo, Milton na wenzake walifika na kulizungushia eneo hilo kamba maalum ili watu wasivuruge ushahidi kisha wao wakaanza kupiga picha na kuchukua vitu mbalimbali ambavyo vingewasaidia katika uchunguzi wao.

Walichukua vipande vya bomu, nywele za watoto, mabaki ya nguo na hata damu iliyotapakaa katika baadhi ya sehemu na kwenda nazo moja kwa moja maabara ambako walimkabidhi Mzee John Simba, bingwa wa uchunguzi wa matukio kama hayo aliyepata elimu yake pia nchini Marekani na kufuzu kwa kiwango cha kuitwa Forensic Scientist.

Asubuhi hiyo ndiyo siku ambayo ripoti ilikuwa inatolewa ili kuweza kujua ni aina gani ya bomu lilitegwa, pengine mtegaji alikuwa nani kama aliacha alama yoyote kwenye gari na kufahamu idadi ya watoto waliokufa ili umma uweze kutangaziwa.

Aliufikia mlango ulioandikwa Crime Scene Investigation Bureau na kuufungua, kisha kunyoosha moja kwa moja hadi kwenye chumba cha mikutano. Alikuta watu wote wamekwishaketi ingawa kikao kilikuwa hakijaanza, naye akachukua nafasi yake na kutulia.

Haukupita muda mrefu sana mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai, Kamishna Pius Kalinga aliingia na kuketi kwenye kiti chake kisha kukifungua kikao na kuomba Mzee Simba aanze kutoa taarifa ya uchunguzi alioufanya maabara ili kazi ya kumtafuta muuaji ianze mara moja.

“Asante sana kamishna, kwanza kabisa nianze kwa kusema watoto waliokufa katika mlipuko huo si kumi na nane kama inavyodaiwa, vipimo vya damu na alama za vidole nilivyovifanya kwa kutumia sampuli nilizoletewa na wapelelezi, zinaonesha watoto waliokuwa ndani ya gari hilo wakati linalipuliwa ni kumi na sita!”
“Mh!” Watu wote wakaguna.

Je, nini kitaendelea? Kama watoto walikuwa kumi na nane kwa nini Mzee Simba anadai waliokufa ndani ya gari walikuwa kumi na sita? Wengine wawili wako wapi? Je, muuaji ni nani na kwa nini aliwaua? Nini kitaendelea katika maisha ya Phillip na mke wake Genevieve ambaye hivi sasa amepata upofu na uziwi?


MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.5.


“UNA hakika walikuwa watoto kumi na sita tu?” Kamishna wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai alisema.
“Kabisa, hivyo ndivyo nilivyogundua, ipo sababu ya kuzungumza na wazazi kuona kama kuna watoto hawakupandishwa, huenda watoto wengine hawakwenda shuleni siku hiyo lakini viongozi wa shule wakaendelea kuelewa basi lilibeba watoto kumi na nane,” Mzee Simba aliongea kwa kujiamini.

“Tutahitaji kwenda shuleni kuongea na wazazi ili tuone idadi ya wazazi waliofiwa na watoto wao, hapo ndio tutapata jibu la uhakika… endelea...”

“Bomu lililotumika ni la kutengeneza nyumbani na limetumia mtungi wa gesi aina ya compressed gas, madini ya Uranium 235 na Plutonium 239, pia kemikali ya Nitroglycerine. Cha muhimu hapa kama tunataka kumpata mtu aliyetega hili bomu ni lazima tufahamu mahali aliponunua Uranium na Plutonium.”

“Kuna alama zozote za vidole?”
“Hakuna, watu waliofanya kazi ya kutega bomu hili ni wataalam haswa kwani hawakuacha alama yoyote inayoweza kufanya wakakamatwa.”

“Duh! Tuachie sisi kazi ya upelelezi, ninachotaka kifanyike mara moja ni kwenda shuleni kuthibitisha kama watoto waliokufa ni kumi na sita au kumi na nane, haiwezekani watoto wawili wakawa hawajulikani walipo na pia tupate kufahamu bomu lilitegwaje ndani ya gari, muelewe mahali ambako huwa linalazwa ili kama kuna mlinzi katika eneo hilo basi ahojiwe, lazima atakuwa anahusika,”
Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai aliongea na watu wote wakaitikia.

Huo ukawa ndiyo mwisho wa kikao, watu wote wakasambaa wakiwa na nakala za taarifa iliyotolewa na watu wa Uchunguzi wa Vielelezo.
Hakuna aliyekuwa na picha kamili kichwani mwake juu ya nani hasa alikuwa mhusika wa kutega bomu hilo, sababu ilikuwa ni ipi iliyopelekea watoto kumi na nane au kumi na sita wasio na hatia kuuawa kikatili kiasi hicho.

Shule ya Kimataifa ya Holy Ghost ambako watoto Dorice na Dorica walitakiwa kuanza darasa la kwanza ilikuwa imegubikwa na msiba mkubwa mno, watu wengi walimiminika shuleni hapo kuomboleza.Eneo maalum lilitengwa kwa ajili ya watu kuweka maua na kadi za rambirambi, maelfu ya kadi na maua yalitupwa hapo yakiwa na ujumbe wa kuhuzunisha.

Vilio vilitawala kila kona, haikuwezekana tena kuendelea na masomo. Ikabidi kila kitu kiahirishwe, vyombo vyote vya habari vilikuwepo, ilibidi rais na viongozi mbalimbali wa serikali wafike kutoa pole kwa msiba huo mkubwa uliolipata taifa. Katika hotuba yake, rais aliahidi kuwasaka magaidi waliofanya kitendo hicho kwa udi na uvumba mpaka wapatikane.

Baadaye maaskari walifika na kuanza kuzungumza na walimu juu ya idadi ya watoto, wakakutanishwa na wazazi wote kumi na sita, familia kumi na saba yenye watoto wawili ilikuwa ni ya Phillip na mke wake Genevieve, askari walitaka pia kuwaona wazazi hao ili kuthibitisha kama kweli watoto walioteketea walikuwa ni kumi na nane kama walivyoagizwa na mkuu wao wa kazi.

“Wapo Hospitali ya Taifa Muhimbili wakiendelea na matibabu, labda mnaweza mkawafuata huko kuthibitisha kama kweli watoto wao walikuwemo.”

“Tutakwenda huko hospitali tuone kama tunaweza kuzungumza nao.”
Pilikapilika zilizofuata hapo zikawa ni mazishi, wazazi walikataa kabisa watoto wao kuzikwa kwenye kaburi la pamoja, ikabidi wapewe mabaki ya miili ya watoto wao ili wakazike wenyewe. Kila mtu alipewa alichopewa, ilikuwa ni kama kuwagawia watu kilichopatikana, hatimaye wote kumi na saba wakapata kitu cha kwenda nacho nyumbani bila kujali ulikuwa mwili halali wa mtoto wao au lah.

Mzee Mpangal ndiye aliyepokea mabaki ya Dorice na Dorica, alipowasiliana na Phillip kuhusu mazishi alikataa kabisa akitaka yahifadhiwe chumba cha maiti mpaka mke wake atakapozinduka ili ashuhudie mazishi ya watoto wake hata kama ingekuwa ni baada ya mwaka mmoja.

Angekuwa na mamlaka ya kuzika Mzee Mpangal angefanya hivyo, lakini kisheria mzazi ndiye alikuwa na uamuzi hivyo alilazimika kukubaliana na uamuzi wa Phillip. Mabaki yakahifadhiwa chumba cha maiti kusubiri fahamu za Genevieve zirejee.

Kila siku kwa Phillip ilikuwa ni machozi, akiwalilia watoto wake na kumsikitikia Genevieve ambaye aliendelea kulala kitandani bila fahamu mpaka zilipomrejea siku nne baadaye akiwa haelewi kilichoendelea, cha kusikitisha zaidi daktari akaweka bayana kuwa Genevieve alikuwa amepoteza uwezo wa kuona na kusikia na hata kumbukumbu zake hazikuwa sawa.

“Daktari ni kwanini anaendelea kuwaita watoto eti awapeleke shule?”
“Hana kumbukumbu, kilichompata ni hali fulani ambayo kitaalam inaitwa Concusion, yaani ubongo ulitikisika sana alipoanguka na kupiga kichwa chini, kumbukumbu zikafutika ni kama vile ambavyo hutokea katika kompyuta, vivyo hivyo kwenye ubongo wakati mwingine. Fahamu zake zitarejea baadaye lakini taratibu.”
“Kuona?”

“Vituo vyake vya kuona na kusikia kwenye ubongo vimeharibiwa sababu ya shinikizo la damu kupanda sana, hapo kwa kweli naomba tu niseme kwa uwazi kuwa, Genevieve hataweza kuona wala kusikia maisha yake yote.”

Haikuwa mara ya kwanza kwa Phillip kusikia taarifa hiyo, muda mfupi tu kabla daktari alikuwa amemweleza lakini hakutaka kulichukua hilo kama jibu akidhani labda baadaye daktari angebadilisha. Roho ikamuuama, akahisi kitu kama kisu cha moto kikimchoma. Alipomwangalia Geneviveve kitandani alikosa uwezo wa kuyazuia machozi.

“Genevieve awe kipofu? Watoto wangu wote wamekufa? Ni nani hasa aliyetega bomu kwenye basi la shule? Huyu ndiye adui yangu, nitamtafuta popote duniani mpaka nimtie mkononi, hata kama ni Osama bin Laden ambaye Marekani imeshindwa kumkamata, basi mimi nitamkamata, siwezi kumwacha mtu aliyeniharibia maisha kiasi hiki aendelee kutanua,” Philip aliwaza kichwani mwake.

Hiyo ndiyo ilikuwa dhamira yake, kikwazo pekee alichokiona ni Genevieve, alishindwa kabisa kuanza msako wa magaidi akimuacha mkewe hospitali, hilo ndilo lilikuwa jambo baya la mwisho angeweza kulifanya maishani mwake kabla ya kufa.

Aliendelea kuomba Genevieve apate nafuu na baadaye kutoka hospitali ili ajipange kwa kazi, hakutaka tena kurejea ofisini kwake, uhasibu haukuwa na maana tena, alichokihitaji maishani mwake kwa wakati huo ambacho kingemtuliza na kumpa faraja hakikuwa kingine isipokuwa kuwapata wauaji wake.

Wiki moja baadaye Genevieve aliruhusiwa kutoka wodini kwani asingeweza kukaa hospitalini siku zote wakati alikuwa na nafuu, madaktari walitaka akaugulie nyumbani. Mpaka anaondolewa hospitalini bado hakuwa na uwezo wa kuona wala kusikia, kumbukumbu zake pia zilikuwa hazijarejea, hakujua kama watoto wake walishakufa, mara tatu kwa siku aliwaita huku akilia na kudai kwanini walikuwa wakiwekwa mbali naye.

Jambo pekee lililokuwa limebaki likawa ni mazishi, Phillip hakuwa na ubishi tena juu ya watoto wake kuhifadhiwa kwani Genevieve hakuwa na fahamu ya chochote kilichoendelea. Maandalizi yakafanyika ndipo Dorice na Dorica wakazikwa bila Genevieve kuelewa kilichokuwa kikiendelea, baada ya hapo akarejeshwa nyumbani ambako maisha ya huzuni kwa Phillip yaliendelea.

Nyumba ilikuwa kubwa mno kwake kwani sasa waliishi watu watatu peke yao; yeye, mfanyakazi wa ndani na Genevieve. Hii ilizidisha huzuni yake, kila siku alikuwa na picha ya watoto wake mkononi, hizo ndizo zilimfanya alie zaidi. Marafiki walijitahidi kuja kumtembelea na kumfariji lakini hawakuweza kumrejesha tena katika hali ya zamani, tayari alikuwa mtumwa wa huzuni na mateso na hakujua furaha ingerejea vipi maishani mwake tena.

“Hodi...” alisikia sauti hiyo mlangoni akiwa amejilaza sakafuni sebuleni.
Tangu apate matatizo na kurejea nyumbani kwake alilala sebuleni kila siku, hakutaka kabisa kwenda chumbani ambako kungemkumbusha mke na watoto wake.

“Karibu...” akaitikia na kunyanyuka akijua ni wafariji walikuwa wamekuja kumtembelea asubuhi hiyo.
Alipofungua mlango, macho yake yaligongana na wanaume watatu, mmoja wao akaonesha kitambulisho cha polisi kisha kujitambulisha na kueleza nia ya safari yao kwamba walikuwa ni wapelelezi waliofika pale kuzungumza naye juu ya tukio lililotokea ili awaeleze alichokifahamu ambacho waliamini kingewasaidia kuwajua watu waliofanya kitendo hicho.

“Nasikia ulipokea simu ya mtu akikupa taarifa ya bomu kuwepo ndani ya gari la shule?”
“Ni kweli.”
“Unayo namba yake aliyekupigia?”
“Haikuandika namba, iliandika tu neno Call!”
“Tutaijua baadaye ni ya nani. Unadhani ni kisasi?”

“Sidhani kama ni kisasi, sina ugomvi na mtu, maisha yangu yalikuwa haya haya siku zote, sipendi kabisa kugombana na binadamu wenzangu. Huyo niliyemtenda ubaya mpaka akafikia hatua ya kuua watoto wangu ni nani?” Phillip alibubujikwa na machozi akijieleza.
“Hebu tueleze kidogo historia ya maisha yako.”
“Ni ndefu.”
“Tueleze tu hivyo hivyo.”

Je, nini kitaendelea? Wauaji watapatikana? Watoto waliokufa katika tukio hilo ni kumi na sita au kumi na nane? Kama ni kumi na sita wawili wako wapi? Fuatilia KESHOOO,
KUANZIA LEO EPISODE ZA HADITHI ZITAKUWA 5 TU KILA SIKU......USIKU MWEMA!!!!

MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.6


Polisi wameanza upelelezi wakijaribu kuchunguza ni nani hasa anayehusika na kutega bomu ndani ya gari la wanafunzi lililolipuka na kuua idadi ya watoto kumi na sita wasio na hatia.

Hii ni kwa mujibu wa polisi waliofanya uchunguzi. Kwa mujibu wa shule, idadi ya watoto wa shule waliokufa ni kumi nane, jambo ambalo limewashangaza watu wengi kiasi cha kushindwa kuelewa ni watoto wangapi hasa waliokufa kwenye mlipuko huo.

Uchunguzi umeanzia eneo la tukio ambako vitu mbalimbali vilichukuliwa ili kuangalia kama mtegaji wa bomu aliacha alama yoyote, matokeo yametoka na kuonesha hakuna alama iliyobakia, mtegaji alikuwa ni mtaalamu wa kazi hiyo.

Baada ya hapo polisi waliamua kumfuata Philip nyumbani kwake ambako tayari mke wake amekwisharuhusiwa kutoka hospitali akiwa hana kumbukumbu juu ya yaliyotokea, lengo ni kwenda kumuuliza juu ya simu aliyopokea ikimpa onyo asipakie watoto wake kwenye gari la shule sababu ndani yake kulitegwa bomu. Wapelelezi waliamini huo ungekuwa mwanzo mzuri wa kumpata muuaji.
Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO...

“Nasikia ulipokea simu ya mtu akikupa taarifa za bomu kuwemo ndani ya gari la shule?”
“Ni kweli!”
“Unayo namba ya aliyekupigia?”

“Haikuandika namba, iliandika tu neno ‘Call’!”
“Tutajua baadaye ni nani! Unadhani ni kisasi?”
“Sidhani kama ni kisasi, sina ugomvi na mtu, maisha yangu yalikuwa haya haya siku zote, sipendi kabisa kugombana na binadamu wenzangu. Huyu niliyemtendea ubaya mpaka akafikia hatua ya kuua watoto wangu ni nani?” Philip alibubujikwa machozi akijieleza.

“Hebu tueleze kidogo historia ya maisha yako.”
“Ni ndefu!”
“Tueleze tu hivyo hivyo.”
“Subirini kwanza nije,” Philip aliongea kisha kunyanyuka kwenda chumbani. Aliporejea dakika chache baadaye alikuwa na kitabu cheusi mkononi.

Taratibu akaanza kukifungua huku askari wakimuangalia kwa mshangao, mioyoni mwao waliamini ndani ya kitabu hicho ndimo historia yake ilimokuwa. Wote wakakaa kimya kusubiri wakati wa kusisimua uanze.

“Historia yangu ni ya kusikitisha, sijui kama itawasaidia chochote kwenye upelelezi wenu.”
“Itasaidia sana.”
“Kivipi?”

“Tunaweza tukajua ni nani hasa amefanya ukatili huu.”
“Lakini niliyepoteza watoto kwenye ajali si mimi peke yangu. Je, kama aliyefanya hivyo alikuwa akilipa kisasi kwa mzazi mwingine? Ikatokea tu kwamba watoto wangu wamo?” Philip aliuliza maswali ya mfululizo.

“Tutaongea na wazazi wengine wote, kilichotufanya tukufuate wewe kwanza ni ile taarifa kwamba ulipigiwa simu ya onyo.”

“This is my sad diary!” (Hiki ni kitabu changu cha kusikitisha cha kumbukumbu za matukio). Alianza kukisoma juu huku askari wakimsikiliza kwa makini, walijua lazima wangepata jambo la kuwawezesha hatimaye kumpata waliyekuwa wakimtafuta.

“Why sad?” (Kwa nini yakusikitisha?)
“They are memories I don’t want to remember!” (Ni kumbukumbu ambazo sitaki kuzikumbuka).

***
Juni 6, 1990, Sengerema Sekondari, Mwanza
Namshukuru Mungu niko hapa sekondari, hii ni ndoto na ni jambo ambalo hakuna mtu anayeweza kuliamini. Bila shaka baba na mama yangu wangekuwa hai, wangefurahi sana kumuona mtoto wao amefikia kiwango hiki cha elimu, tena peke yangu kutoka kijijini kwetu.
Acha nilale nikiamka asubuhi kabla ya kwenda darasani nitaendelea kuandika tena. Kumbukumbu hizi zitakuja kusomwa na watu siku moja hata kama nitakuwa nimekwisha kufa.

Juni 7, 1990
Usingizi ulikuwa mnono, nimeota ndoto moja tu leo, ya yule yule msichana mrembo ambaye kwa miaka mingi nimekuwa nikimuota, sura ile ile, sauti ile ile, umbile lile lile. Hakika msichana huyu ni mrembo, sijawahi kuona kama yeye hapa duniani. Leo aliniomba tuoane lakini nikakataa na kumwambia mimi bado mwanafunzi, lakini kwa nini ndoto hii kwa miaka yote? Hapa kuna jambo, iko siku nitakuja kulifahamu.

Juni 8, 1990
Bado watu wananitenga shuleni, eti kwa sababu wazazi wangu walikuwa wagonjwa wa Ukoma. Lakini tumekwisha fundishwa kwamba Ukoma sio ugonjwa wa kurithi, kwa kipindi kirefu nimenyanyapaliwa na kufanywa nijisikie sina amani ingawa mimi mwenyewe ugonjwa huo sina. Baadhi ya wasichana hata huniambia sitapata msichana wa kuoa. Sijali, msichana wa kwenye ndoto zangu ananitosha.

Kila ninapokumbuka maisha yangu ya utotoni, kijijini nilipozaliwa na mateso niliyoyapata moyo wangu unauma sana. Hata hivyo namshukuru Mungu nimefika hapa nilipo. Ipo siku nitakuja kuwa na maisha bora. Hebu nijifute machozi…

Philip aliendelea kuwasomea askari kitabu chake huku wote wakiwa kimya na wakionekana kuvutiwa na kila kitu alichokuwa akikisoma ingawa bado hawakupata picha hasa ya maisha yake kwa undani kwani maandishi hayo yaliandikwa kwa ufupi mno.
“Unaweza kusimulia sasa vizuri ili tukuelewe?”

“Nilizaliwa kijiji cha Bukokwa, mwaka 1976, katika familia ya bwana na bibi Robert Mpina, yenye watoto wawili mapacha. Mimi na ndugu yangu ambaye hivi sasa ni marehemu. Baba yangu alikuwa ni mwalimu ingawa mama yetu alikuwa ni mama wa nyumbani. Tukiwa na umri wa miaka mitano, pacha wangu aligongwa na gari na kufa pale pale. Naikumbuka sana hiyo siku, sijawahi kulia kiasi hicho tangu nizaliwe…” Philip akakohoa kidogo kusafisha koo.

***
Genevieve alikuwa kimya akiendelea kumshuhudia mume wake akisimulia historia ya maisha yake kwa watu ambao hakuwafahamu. Bado kumbukumbu zake zilikuwa hazijakaa sawa, hakuelewa chochote juu ya kilichowapata watoto wake. Aliendelea kuwaita akidhani labda walikuwa wamekwenda shule, ghafla akiwa katika mawazo hayo kitu kama filamu fupi kikampita akilini mwake.

Alikuwa amesimama kando ya barabara, akilishuhudia gari lililobeba watoto wake likiondoka mahali alipokuwa. Muda huo huo akiendelea kushangaa, gari dogo aina ya Starlet lilisimama kando yake, msichana mmoja akachungulia kutoka ndani na kumsalimia akimuulizia barabara ya kwenda mjini. Kwa alivyoonekana msichana huyo hakuwa mtu wa kushindwa kufahamu barabara ya kumpeleka katikati ya jiji.

“Yaani wewe dada hujui barabara ya kwenda mjini?”
“Kwani kuna ajabu gani? Kama hutaki kunisaidia basi.” Dada huyo alijibu na kuanza kuondoka taratibu.

Macho ya Genevieve yakarejea tena kwenye basi la wanafunzi, akashangaa kuona likiwa limesimama na tayari lilikuwa linaondoka, pia kulikuwa na gari jingine dogo jeusi ambalo liliondoka kwa kasi ya ajabu. Muda huo huo pikipiki iliyombeba Philip ikafika akiulizia watoto na kumuonesha basi, bila kupoteza wakati akaanza kulifuata, mbele kidogo ndipo likalipuka.
Alipofikia hapo, kumbukumbu zikapotea tena.

MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.7.


Muda mfupi tu baada ya kifo cha pacha wangu, wazazi hawakuwa tena na sababu ya kuendelea kuishi kijijini Bukokwa, isitoshe unyanyapaa dhidi ya ugonjwa wao ulikuwa umeongezeka sana. Walitengwa mno na kijiji, hakuna mtu hata mmoja aliyetaka kushirikiana nao, hata mimi kila mahali nilikopita niliitwa mtoto mkoma. Mwanzoni sikuelewa kabisa hiyo ilikuwa na maana gani, lakini baadaye nilielewa kila kitu na kuanza kujiona sina maana.

Nilikuwa na umri wa miaka sita tu, huo ukiwa mwaka 1982, kwa umri wangu nilitakiwa kuwa nimekwishaanza darasa la kwanza lakini wazazi walishindwa kunipeleka shule ambako waliamini watoto wa watu wengine wangeendelea kunitenga. Niliumia kila nilipowaona watoto wenye umri kama wa kwangu wakienda shule kila siku asubuhi, ndani ya suruali za kaki na mashati meupe yaliyoitwa Shikibo.

Katika umri huo tayari nilishaanza kuota sana juu ya mtoto huyu wa kike mwenye ngozi laini ya maji ya kunde, nywele nyingi kichwani, macho makubwa ya kulegea, shingo ndefu, midomo minene ya duara, pua iliyochongoka na vishimo kwenye mashavu ambavyo watu wengi siku hizi wanaviita ‘dimpoz.’

Ninachoweza kusema tu ni kwamba ingawa mtoto huyu wa kike alikuwa mdogo sawa na umri wangu, sura yake ilivutia mno na katika umri wangu huohuo nilitamani kuwa naye. Nakumbuka katika ndoto yangu ya kwanza, nilikuwa ufukweni nikichezea maji, siku hiyo mimi na wazazi wangu tulikuwa tumekwenda huko kwa mapumziko.

Nilishituka tu akiibuka kutoka majini mbele yangu na sikujua alikotokea, akatabasamu nami nikafanya hivyo. Tabasamu lake lilikuwa zuri mno, hakuna mwanadamu angeweza kujizuia kulijibu kwa tabasamu. Akanisogelea na kunisalimia kisha kuniambia alivutiwa sana na mimi.

“Mimi bado mdogo mbona?”
“Tutakua tu, nitakusubiri.”
“Wewe ni nani?” Nilimuuliza.
Hakujibu swali langu, akanitega mgongo kama vile alikuwa akiona aibu, kisha kuzama tena majini, sikumuona alikopotelea lakini mbele kidogo kichwa chake kilionekana na kutabasamu, akapunga mkono hewani kisha kujibinua na kuzama kwa mara nyingine ndani ya maji, sikumuona tena na nikazinduka.

Sikumwambia mtu yeyote juu ya ndoto hiyo, sikuwa na mtu wa kumsimulia, niliichukulia kama ndoto ya kawaida na nisingeiota tena, haikuwa hivyo, niliendelea kumuota binti huyo karibu kila siku, akitokea eneo hilo hilo la baharini.

Safari zote zilizofuata aliongea na mimi bila kuniangalia usoni kama vile alikuwa akiona aibu ya kunitazama, katika maongezi yake aliendelea kusisitiza namna alivyonipenda na alitaka siku moja tuoane na kuwa mume na mke halafu tupate watoto wawili mapacha kufidia pacha wangu aliyepotea.

“Unajuaje kama nina pacha aliyepotea?”
“Ninaelewa Phillip, nakufahamu sana.”
“Wewe ni nani kwani?”
“Muda wa kulifahamu jina langu utakapofika utanifahamu, kwa hivi sasa bado.”
“Niangalie basi usoni.”

“Siwezi…” Alijibu binti huyo na kuzama majini kabla hajamaliza sentensi yake.
Kwa sababu ya manyanyaso yaliyokuwepo kijijini kwetu Bukokwa, baba na mama waliamua tuhame twende mjini Mwanza kutafuta maisha sehemu ambako hakuna mtu angeweza kuwanyanyapaa. Chaguo lao likawa ni kukimbilia mjini ambako wangejichanganya na watu wenye matatizo kama yao walioishi kwa kuombaomba.

Kihistoria wazazi wangu walikutana kwenye kambi ya wagonjwa wa ukoma iitwayo Kidugalo, iliyoko wilayani Sikonge mkoani Tabora ambako baada ya kugundulika wana ukoma, walipelekwa na ndugu zao na hawakutakiwa kurudi tena nyumbani kwa sababu ugonjwa wa ukoma ulitafsiriwa kama laana na jamii. Katika mazungumzo yao niligundua walikuwa ni watu wa Kakonko huko Kigoma na waliwasiliana kwa lugha ya Kiha si Kisukuma kama walivyofanya watu wengine.

Naikumbuka vyema siku tuliyopanda basi la African Bus Service kutoka Bukokwa kuelekea Mwanza mjini, mara tulipoingia tu ndani ya basi watu walianza kutukimbia wakiogopa kugusana na sisi, kondakta akatuchukua na kutupeleka kiti cha nyuma kabisa kilichokaliwa na watu sita, chote tukakikalia watu watatu, mimi na wazazi wangu.

Ilikuwa saa kumi ya alfajiri basi lilipoanza safari na kuendelea mpaka kuingia Mwanza mjini saa saba za mchana, ulikuwa umbali wa kilomita kama sitini hivi lakini kwa sababu ya ubovu wa barabara tulitumia muda mrefu sana kusafiri.

Wakati tunapita mitaani Mwanza, nilianza kuwaona watu wengine waliofanana kabisa na wazazi wangu kwa maumbile, hawakuwa na vidole na sura zao zilikuwa zimevimba nundu nyingi, wao pia walikuwa wakoma na waliketi kando ya barabara wakiwa na vikopo vidogo, kazi yao ikiwa ni kuomba kwa wapita njia.

Tulipofika mtaa maarufu wa Uhuru mjini Mwanza kwenye daraja kubwa la Mirongo, tuliona kundi kubwa la wagonjwa wa ukoma wakiwa wamelala kwenye vibanda vilivyotengenezwa kwa maturubai kando ya mto, baba akanishika mkono na kuanza kunivusha upande wa pili kwenye vibanda hivyo.

“Ng’wadila banamhala!” (Habari za leo wazee?) Baba aliwasalimia wanaume waliokuwa wameketi kando ya daraja kwa Kisukuma,
“Ng’wadila, ulimhola bhabha?” (Salama, habari zako mzee?)
“Nali mhola, kinehe ubing’we?” (Mimi sijambo, nyinyi je?)
“Tuli mhola duhu!” (Hatujambo tu)
“Niza nane, tugeme shihamo ukuchola sabo...” (Nami nimekuja, tujaribu kutafuta pamoja mali)

“Tuliho, bejaga kanumba lulu aha mhelo aho!” (Karibu, tengeneza kijumba basi pale kando.)
Wote walikuwa wagonjwa wa ukoma, wakipitia mateso na unyanyapaa wa aina moja, hawakuwa na la kufanya zaidi ya kupendana. Baba alisaidiwa kutengeneza kibanda kando kabisa ya mto, kibanda chake kikiwa cha mwisho.

Hiyo ndiyo ikawa nyumba yetu na hicho ndiyo kikawa kijiji chetu, tulitakiwa kuishi hapo maisha yetu yote. Hapakuwa na uwezekano wa kurudi tena kijijini Bukokwa, hivyo kazi ya wazazi wangu kila siku asubuhi ikawa ni kuondoka pamoja nami kwenda mitaani kuomba wakiwa na kopo, mimi nikiwa nimeketi kando yao nikiangalia wapita njia na roho kuniuma.

Sikupendezwa na maisha hayo na sikutaka kabisa na mimi nije kuishia hivyo, niliamini katika elimu na nilitamani kwenda shule, kila siku nilipowaona watoto wakipita mbele yangu kwenda shule roho iliniuma lakini sikuweza kuwaeleza wazazi wangu juu ya shule.

Jioni tuliporejea kambini, baba aliketi na rafiki yake mpendwa Masalu Nkwabi, mgonjwa wa ukoma kutoka Ukiriguru nje kidogo ya mji wa Mwanza, alikuwa ameishi hapo kando ya daraja kwa miaka kumi na mbili na alikuwa mwenyeji sana katika mji huo.

Kila siku mzee Masalu alitoka na baba yangu kwenda kutembea baada ya kurudi kutoka kuombaomba, mimi nikabaki na mama na waliporejea usiku walikuwa wamelewa kupita kiasi, mama alilalamika lakini baba hakusikia.

Hata katika mazingira kama hayo, ingawa nililala chini nikiumwa na papasi pamoja na mbu bado niliendelea kumuota msichana yule yule, alinijia mara nyingi mno katika ndoto zangu tukiwa hapo hapo kando ya bahari na kuniambia aliyafahamu matatizo yangu na siku moja angekuja kuyaondoa kabisa mara tukioana.

“Tutaoanaje wakati sote bado wadogo na sikufahamu?”
“Tutakua tu Phillip na utakuja kunifahamu!”
“Kwani wewe unaishi wapi?”
“Huwezi kujua ninapoishi, hata ukijua huwezi kwenda kwani wewe ni wa ulimwengu mwingine na mimi vivyo hivyo natoka ulimwengu mwingine.”

“Unamaanisha nini kusema hivyo?” Hakunijibu akapotelea majini.
Bado sikumsimulia mtu juu ya ndoto hiyo, nilishamzoea sana msichana huyu kiasi kwamba hata nilipotembea nilijaribu kuangaza watu ninaokutana nao ili kuona kama ningeweza kukutana naye mahali fulani. Hakika haikuwa ndoto ya kawaida, kila kitu kilionekana halisia mno aliponijia, alizidi kuwa mzuri na kupendeza kadri siku zilivyozidi kwenda.

“Shikamoo wazee!” Ilikuwa ni sauti ya mtu mmoja akipita kando ya njia, nikageuka kumwangalia, alikuwa Muasia mrefu mwembamba, nywele zake zikiwa zimefungwa kwa nyuma.
“Marahaba hujambo?” Baba na mama wakaitikia.

“Sijambo tu, naitwa Mustafa Kudret, natokea shirika linaloitwa Tujaliane, kazi yetu ni kuwasaidia watoto waishio katika mazingira magumu, nimemuona huyu mtoto hapa ni wenu?”
“Ndiyo ni wetu.”

“Anasoma?”
“Hapana.”
“Kwanini?”
“Gharama.”

“Eti wewe mtoto unaitwa nani?”
“Phillip.”
“Unapenda shule?”
“Ndiyo.”

Je, nini kitaendelea?, ni lazima ujue ni nani aliyetega bomu kwenye gari na kuwaua Dorice na Dorica pamoja na watoto wengine wasio na hatia.







MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.8.

Upelelezi wa polisi kuchunguza ukweli juu ya bomu lililolipuka umeanza. Pamoja na uchunguzi walioufanya eneo la tukio na kuongea na mashahidi walioshuhudia, polisi walihitaji kuongea na Phillip ambaye alidaiwa kupokea simu ya onyo kabla ya tukio hilo, hivyo wakamfuata nyumbani kwake.

Phillip aliyekuwa na masikitiko mengi aliamua kuwaeleza askari historia yote ya maisha yake akitumia kitabu alichotunza kumbukumbu zake tangu utotoni (diary). Lengo lilikuwa ni kutaka kuonesha ni kwa kiasi gani hakuwa na adui wa kuweza kuwaua watoto wake kinyama kiasi kile.

Ameeleza alivyozaliwa na wazazi wenye ugonjwa wa ukoma. Kwa sababu ya kunyanyapaliwa wakaamua kuhamia Mwanza mjini ambako waliishi mtaani pamoja na ombaomba wengine mpaka siku alipokuja mtu mmoja na kujitambulisha kama Mustafa Kudret, kutoka Shirika la Kusaidia Watoto liitwalo Tujaliane. Mustafa aliwauliza wazazi wa Phillip kama mtoto wao alikuwa akisoma shule mahali popote.

Wazazi wakaeleza ukweli kuwa Phillip alikuwa hasomi shule mahali popote sababu ya umaskini ingawa wangependa mtoto wao apate elimu ili asiishie kuwa ombaomba kama wao.

Mwisho wa mazungumzo hayo, Mustafa, Mtanzania mwenye asili ya Asia, alimgeukia Phillip na kuendelea kumuuliza maswali, akakiri kupenda shule na huo ndiyo ulikuwa ukweli kuhusu yeye.
Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO...

“Kweli unapenda shule?”
“Ndiyo.”
“Unataka kuwa nani ukikua?”
“Rubani.”
“Kabisa.”
“Ndiyo.”

“Basi kesho nitakuja kukuchukua ukapime nguo za shule, halafu Jumanne nitakupeleka shuleni ukaanze darasa la kwanza.”
“Sawa, asante!”

Mustafa aliaga na kuondoka akiniacha katika furaha ambayo sikuwahi kuwa nayo tangu kuzaliwa kwangu. Hakuna kitu nilichohitaji kama shule, nilijua ingawa katika umri mdogo kabisa hicho kingenisaidia maishani. Hatimaye ndoto sasa ilikuwa inatimia, nilishinda na furaha siku nzima nikiwashuhudia wazazi wangu wakiomba kwa wapita njia na kudondoshewa visenti kwenye kopo, tena wakati mwingine kwa dharau kubwa, jambo lililoniumiza sana moyoni na kutamani kuibadilisha hali hiyo.

Hiyo ilikuwa ni Jumapili jioni, tulirejea kambini kando ya mto ambako baba wala hakukaa sana, akaondoka na rafiki yake, Mzee Masalu kama ilivyokuwa kawaida yao kwenda kwenye vilabu vya pombe maeneo ya Mlango Mmoja. Mama alibaki nami akishughulikia chakula cha jioni.

Baada tu ya kupata chakula cha jioni, nilitandika mkeka wangu chini na kulala. Nilipozinduka baadaye katikati ya usiku, si baba wala mama aliyekuwepo ndani ya kibanda chetu, nilikuwa nimelala peke yangu jambo ambalo halikuwa kawaida kabisa. Nikarejea usingizini, safari hii msichana wa kwenye ndoto zangu alinijia, akiwa amependeza kupita kiasi na kuniambia ilikuwa ni lazima tufunge ndoa.

Tofauti na siku nyingine zote, nilijikuta nakubali bila kuhoji kuhusu umri wetu, akaniambia anichukue kwenda kunitambulisha kwa wazazi wake. Sikukataa, nikanyanyuka na kwa pamoja tukaanza kutembea tukipita kwenye mitaa yenye giza lakini macho yake yalimulika kama tochi kiasi cha kuonesha njia. Tukafika ufukweni mwa bahari na akaniambia nipande mgongoni, sikusita wala kuhoji swali lolote, moyo wangu pia haukuwa na woga ingawa sikumfahamu sana msichana huyo mdogo.

Nikamdandia na akaanza kuogelea nikiwa mgongoni mwake, sote tukazama majini bila mimi kuwa na matatizo ya kupumua, tofauti na siku nyingine zote nilizoogelea ambazo sikuwa na uwezo wa kubaki ndani ya maji bila pumzi hata kwa dakika moja. Kwa karibu saa nzima msichana huyo aliogelea, tukipita sehemu zenye mwanga mkali na majengo mazuri, huku tukipishana na samaki wengi, wakati mwingine nyangumi bila hata kudhuriwa.

“Tunakwenda wapi?” Nilimuuliza baada ya kuona hatufiki.
“Kwetu.”
“Kwenu wapi?”
“Utapaona tukifika.”

Safari ikazidi kusonga mpaka chini kabisa ya maji ambako tulikuta jumba kubwa la kifahari, tukaingia ndani yake na kupokelewa na sauti za shangwe ambazo sikuona zilitokea wapi kwani hapakuwa na mtu zaidi ya mimi na msichana huyo. Akanitoa hofu kwamba nisiogope na tukazidi kuingia ndani ya jumba hilo lililopambwa kwa vito vya thamani vyenye kung’ara ambavyo niliamini vilitengenezwa kwa almasi na dhahabu.

“Baba!” Aliita msichana huyo.
“Naam!”
“Nimemleta mwanao ninayempenda kuliko binadamu mwingine yeyote kwenye ulimwengu wao. Niko tayari kuolewa naye, nihame huku na kwenda kuishi kwenye ulimwengu wao kwani yeye hawezi kuja huku,” aliongea msichana huyo nikizidi kushangaa alimaanisha nini aliposema ulimwengu wao.

“Unampenda?”
“Ndiyo.”
“Uko tayari kuolewa naye?”
“Ndiyo.”
“Yeye anasemaje?”

“Labda umuulize wewe.”
“Uko tayari kumuoa binti yangu?”
“Ndiyo.”

Vigelegele vikasikika kila mahali ndani ya jumba hilo, lango kubwa likafunguka, wakaingia farasi wawili weupe nyuma wakiwa na tela lililopambwa vizuri kwa vitambaa vyeupe, likiwa na matairi ya rangi nyeupe. Farasi hao hawakuwa wa kawaida kwani walikuwa na mabawa, na ndimi zao zilitoa moto, macho yao yakiwaka kama tochi.

Kufumba na kufumbua tukawa tumebadilika nguo tulizovaa, msichana akawa amevaa gauni la kijani lililong’ara kupita kiasi, hakika alipendeza nami nikawa nimevaa suti nyeupe. Sote wawili tukapandishwa kwenye tela na mikono ya watu ambao sikuwaona huku vigelegele vikisikika.

“Tayari mmekwishafunga ndoa, nyie sasa ni mke na mume. Wewe kijana sasa hivi hutaitwa Phillip, bali Samir,” ilikuwa ni sauti ile ile ya baba wa msichana.

Huku akionesha tabasamu msichana huyo alinigeukia na kunikumbatia, kwa mara ya kwanza akanipiga busu shavuni, nikausikia mwili wangu kama umepigwa shoti ya umeme kwa msisimko nilioupata. Farasi wakaanza kuondoka huku wakipaa kwa kutumia mabawa yao.

Tukapitishwa kwenye jiji kubwa, maelfu ya watu wakiwa wamesimama kando ya njia wakitushangilia kwa ndoa hiyo, mikononi wakiwa wameshikilia matawi ya miti wakiyapeperusha hewani. Nilipowatazama vizuri niligundua hawakuwa binadamu wa kawaida, kwani usoni walikuwa na jicho moja tu kubwa katikati ya paji la uso.

“Sasa tumeoana, unaweza kuniambia unaitwa nani?”
“Mimi?”
“Naitwa Zamaradi.”
“Jina zuri.”

“Asante Samir, tangu sasa wewe ni mume wangu, nakupenda. Nasikitishwa tu na taabu zitakazokupata huko kwenye ulimwengu unaoishi, utateseka sana lakini usiwe na wasiwasi, nitakuwa pamoja nawe.”
“Unamaanisha nini Zamaradi?”

“Kuna taabu kubwa inakuja mbele yako, hata leo hii utalia sana machozi,” aliongea msichana huyo.
Ghafla niligutuka usingizini baada ya kusikia mlango wa bati kwenye kibanda chetu ukigongwa kwa nguvu, nikaketi kitako huku nikitetemeka.

Nilikuwa nimeota ndoto ya kutisha kuliko zote nilizowahi kuota juu ya msichana huyo. Nilipozungusha macho yangu chumbani nilimwona baba ameketi kando yangu akilia, sikuelewa ni kwa sababu gani alikuwa katika hali hiyo na pia sikufahamu ni muda gani alirejea, mama hakuwepo.

“Fungua, fungua mlango haraka.”
“Baba kuna nini?” Nilimuuliza baba yangu.
“Ni hasira mwanangu, nimefanya jambo ambalo sikutegemea kulifanya.’
“Jambo gani?”

“Nimewaua Mzee Masalu na mama yako.”
“Umewaua?”
“Ndiyo.”
“Kisa?”

“Nimewakuta wanafanya tendo la ndoa kwenye choo cha kilabu cha pombe tulichokwenda kunywa.”
Sikuwa na cha kusema zaidi ya kuanza kumlilia mama yangu. Haikuwa rahisi kukubaliana na maneno ya baba, ilifanana kama nimetoka kwenye ndoto moja ya kutisha na kuingia kwenye nyingine.

Mlango ukafunguliwa kwa nguvu, watu wawili wakaingia na kumvisha baba yangu pingu mikononi kisha kuondoka naye wakimsukuma. Sikubaki nyuma, nikaamua kufuatana nao nikilia hadi kituo kikuu cha polisi ambacho kipo karibu kabisa na bandari ya Mwanza.

Baba aliingizwa ndani na kutupwa mahabusu, watu wote wakimwita kwa jina la Mkoma Mkatili. Alikuwa amefanya kitendo cha kinyama ambacho sikuwa tayari kukiamini mpaka nilipozishuhudia maiti za mama na Mzee Masalu zikiwa zimechinjwa kwa kisu kama mbuzi. Sikuwahi hata siku moja kufikiri baba yangu mzazi angekuwa katili kiasi hicho.

Mustafa Kudret alikuwepo wakati wa mazishi ya mama yangu na Mzee Masalu kwenye makaburi ya Bugando ambako wafanyakazi wa Halmashauri ya Jiji walishughulikia kazi hiyo. Niliumia sana kumwona mama yangu akiingizwa ndani ya shimo na kufukiwa akiwa hana hata sanda. Hasira dhidi ya baba iliniingia ingawa bado nilikuwa na umri mdogo.

Sikuwa na mahali pa kwenda baada ya mazishi hayo, Mustafa akalazimika kunichukua hadi kwenye kituo chao cha kulelea watoto wa mitaani. Kulikuwa na watoto wengi kama mimi ambao hawakuwa na makazi, nikatambulishwa kwao na wakaelezwa kwamba tangu siku hiyo ningekuwa miongoni mwao.

Ingawa nililala ndani, kula chakula kizuri na Mustafa alininunulia sare za shule na kunipeleka Shule ya Msingi Nyakabungo wiki moja baadaye kuanza darasa la kwanza, sikuwa na furaha moyoni kwa sababu wazazi wangu hawakuwa pamoja nami kama nilivyozoea kuishi.

Muda mwingi nilikuwa mtoto mwenye huzuni na watoto wengi waliokuwepo kwenye kituo hicho walikuwa ni wakorofi na wapenda ugomvi, hivyo walinigeuza ngoma. Kila siku nilikuwa nikipigwa asubuhi, mchana na jioni kiasi kwamba mwili mwangu ulijaa nundu na makovu.

Hali hii ilinifanya nianze kubadilika, nikalazimika kuchukua hatua ya kujilinda na kujitetea pale nilipoonewa na silaha yangu kubwa ikawa ni wembe. Kila nilikokwenda wembe ulikuwa mfukoni na yeyote aliyenipiga, aliishia kuchanjwa. Nilikuwa na hasira kali sana dhidi ya mtu yeyote aliyenionea.

Sikuacha kumfikiria baba yangu pamoja na kuwa alitenda kosa, kila kesi yake ilipotajwa na yeye kufikishwa mahakamani, nilikuwepo kushuhudia kilichoendelea. Kila aliponiona alilia kwani hali yake ilikuwa imedhoofu na alijua angekufa na kuniacha duniani peke yangu nikiteseka.

“Nisamehe mwanangu, shetani ni mbaya.” Ndiyo maneno pekee aliyoyasema.
Miezi sita baadaye, baba yangu hakuletwa tena mahakamani, nilipojaribu kuuliza kwa askari hawakunificha, walinieleza wazi kuwa baba alikufa akiwa mahabusu kwa ugonjwa wa kuhara na kutapika uliolikumba Gereza la Butimba. Nililia kupita kiasi kwani sasa ilithibitika kabisa nilikuwa yatima kamili.

***
“Usilie Samir, niko pamoja nawe katika shida zote, wewe ni mume wangu katika ulimwengu ninaoishi mimi, vumilia tu yote yatakwisha!” Ilikuwa ni sauti ya Zamaradi nikiwa usingizini kwenye kituo cha kulelea watoto.
“Wazazi wangu wananiuma.”

“Najua mume wangu, lakini mimi nipo. Endelea tu na shule mpaka umalize chuo kikuu”
Hayo yalikuwa ndiyo maisha yangu ya kila siku, mchana niliishi maisha ya kawaida katika ulimwengu huu unaoonekana kwa macho lakini usiku niliishi maisha kwenye ulimwengu mwingine usioonekana kwa macho ya kawaida ambako nilikuwa mume wa msichana mrembo Zamaradi, huko ndiko nilipata furaha yangu tofauti na kwenye dunia hii ambako niliishi maisha ya kupambana na kupigana na watoto wenzangu.

Sikuwahi kumwambia mtu yeyote juu ya ndoto yangu na msichana niliyemuota, ilikuwa ni siri ambayo sikutakiwa kufumbua mdomo kuisema kwa yeyote. Majeraha ya kuondokewa na wazazi wangu yalishapona na nikaendelea na masomo kama kawaida mpaka kufika darasa la saba nikiongoza darasani, hakuna aliyeamini nilikuwa mtoto wa mtaani.

“Samir!”
“Naam.”
“Nina mimba.”
“Mimba?”
“Ndiyo.”

Zamaradi aliniambia maneno hayo mara tu nilipomaliza darasa la saba, kwanza sikuamini lakini baadaye nilipoona tumbo lake linaongezeka ukubwa nikakubaliana naye. Miezi tisa baadaye alijifungua mtoto wa kike aliyefanana sana na yeye, ilikuwa furaha kubwa mno kwa kila mtu aliyeishi chini ya bahari, hatimaye tukawa tumepata mtoto.

Katika ulimwengu ulioonekana kwa macho hakuna mtu hata mmoja aliyeelewa kwamba kwenye ulimwengu usioonekana kwa macho nilikuwa na mke na mtoto wa kike tuliyemwita jina la Mina. Hiyo ilikuwa ni siri ya kufa nayo moyoni mwangu. Kwa wanafunzi wenzangu nilionekana mtoto mwenzao, lakini nilikuwa mtu mzima kuliko mwanafunzi mwingine yeyote shuleni kwetu.







MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.9.


Tayari nilikuwa katika mapenzi mazito na Zamaradi, kwenye ulimwengu halisi ulioonekana kwa macho hakuna aliyeelewa jambo hili, ilikuwa ni siri kubwa, nisingethubutu kufungua mdomo wangu na kuongea mbele ya wanafunzi wenzangu au hata kwa Mustapha Kudret ambaye kwangu alikuwa ni mzazi.

Kwangu haikuwa ndoto tena, kila kitu kilikuwa ni halisi maana karibu kila siku Zamaradi alikuja nikiwa usingizini kuniletea mwanangu Mina, nikashuhudia akiendelea kukua na kufanana na mama yake kwa kila kitu. Kwa jinsi mambo yalivyotokea, hakuna binadamu awaye yote angeamini kwamba ilikuwa ni ndoto tu, ndoto ya kila siku? Swali hilo ndilo lilinifanya nikubali kwamba nilikuwa mume wa mtu lakini kwenye ulimwengu mwingine.

Hayo yakitokea niliendelea na shule kama kawaida, kila siku niliamka asubuhi nikiwa nimechoka sababu ya kukosa usingizi na kuelekea shuleni. Nguvu zangu zote zilielekezwa kwenye masomo, maumivu ya kufiwa na wazazi wangu tayari yalishaondoka moyoni, sasa nilitazama mbele ili niweze kujikomboa, nami nisiishie kuwa ombaomba kama ilivyokuwa kwa wazazi wangu.

Darasani nilikuwa mwanafunzi bora, sikumbuki kushika namba chini ya mbili katika masomo yote mpaka namaliza darasa la saba, hii ilimfurahisha sana mfadhili wangu Mustapha Kudret, kwani nilikuwa mwanafunzi bora kuliko mwingine yeyote kwenye kituo cha kulea watoto yatima na viongozi wote walijivuna kuwa na mtoto kama mimi kwenye kituo chao.

“Phillip!” Mmoja wa walezi aliniita.
“Naam.” Nikaitika.
“Wewe ni mfano wa kuigwa, ukiendelea hivi maisha yako baadaye yatakuwa mazuri, unaumwa macho?”

“Hapana.”
“Kwanini ni mekundu kiasi hicho?” Aliuliza Bibi Nyang’oma, mlezi wa watoto kwenye kituo akinisogelea kisha kuanza kunichunguza, jambo ambalo hakulifahamu ni kwamba usiku na mchana nilikuwa macho, kama nililala ni kwa saa moja au mbili nikicheza na mtoto wangu Mina katika ndoto.

“Hata sijui ni kwanini?”
“Au hupati usingizi wa kutosha usiku?”
“Hapana shangazi, nalala vizuri tu.” Nilidanganya.
Matokeo ya darasa la saba yalipotoka nilikuwa nimefaulu na kuchaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Mwanza kwa ajili ya kidato cha kwanza, ilikuwa ni furaha kubwa mno kwangu na hata nilipolala usingizi, Zamaradi alikuja na kunisifia.

Wote tukashangilia na akanichukua kunipeleka chini ya bahari ambako nilikutana na baba yake pamoja na watu wenye jicho moja, sherehe kubwa ikafanyika kunipongeza kwa ushindi wangu.

“Unakwenda sekondari sasa, utakutana na wasichana wazuri sana, kumbuka tu kwamba wewe ni mume wa mtu kwenye huu ulimwengu ninaoishi mimi, usijaribu kunisaliti, ukifanya hivyo nitakasirika na nikikasirika naweza kukuadhibu vibaya na unajua hasira ni hasara, sipendi kukuua Samir. Leo nataka nikueleze ukweli mimi ni jini mahaba, ninao uwezo wa kukunyonya damu!” Zamaradi aliongea akimwangalia kwa makini, alionekana ni mwenye wivu kupindukia.

“Siwezi kufanya hivyo.” Nilijibu huku nikitetemeka, hapo ndipo nikaelewa nilikuwa kwenye ulimwengu wa viumbe visivyoonekana, kumbe haikuwa ndoto ya kawaida bali ni maisha halisi chini ya bahari ambako majini yaliishi.

“Shauri yako.” Zamaradi aliongea akiukunja uso wake na kunisababishia hofu zaidi, hakika alinitisha kugundua kwamba alikuwa ni jini.

Nilipoamka na kurejea kwenye ulimwengu wa kawaida asubuhi ilikuwa ni furaha tupu kwa kila mtu kituoni, Mustapha aliandaa sherehe ya kunipongeza ambayo ilifanyika mchana bwaloni, kwani mimi ni pekee niliyekuwa nimechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kutoka kwenye kituo hicho.

Siku iliyofuata maandalizi yalianza, Mustapha akaninunulia vitu vyote muhimu vilivyohitajika na wiki tatu baadaye nilipelekwa shuleni na kuanza masomo nikiwa nimemwahidi mfadhili wangu kufanya kila nilichoweza ili nisimwangushe, nikiweka wazi kabisa kuwa katika Tanzania nzima lazima ningekuwemo kati ya kumi bora ambao wangefanya vizuri.

Haukuwa uongo, Shule ya Sekondari ya Mwanza ilikuwa miongoni mwa shule zenye wasichana wazuri sana nchini Tanzania, uwepo wa wakazi wengi wenye asili ya nchi jirani ya Rwanda na Ethiopia ulifanya mabinti wengi waliosoma katika shule hiyo iliyopo katikati ya Jiji la Mwanza barabara ielekeayo Hospitali ya Bugando, wawe wenye sura za kuvutia.

Jambo ambalo sikulitarajia ni kwamba ningeweza kuwavutia wasichana wengi shuleni hapo, hata siku moja maishani mwangu sikuwahi kudhani nami nilikuwa miongoni mwa watu wenye sura ya kuvutia. Hata siku moja sikuwahi kumsikia mtu akiniambia hivyo, lakini nilipoingia Mwanza Sekondari wasichana walianza kunifuata wakijaribu kunishawishi nijiingize kwenye uhusiano wa kimapenzi.

Mara zote niliisikia sauti ya Zamaradi ikinipa onyo kupitia masikioni mwangu. Hofu ya kuuliwa na jini ikanitawala, nikaogopa kufa, haukuwa utani Zamaradi alikuwa na uwezo wa kuondoa maisha yangu kama ningekwenda kinyume na ahadi niliyoiweka. Nikaamua kujiheshimu kwa sababu nilikuwa mume wa mtu mwenye mtoto mmoja kwenye ulimwengu usioonekana kwa macho ya kawaida.

Tabia yangu ya kutopenda ngono, jambo ambalo lilifanywa sana na wanafunzi shuleni ilinifanya nionekane tofauti na wengine wote, ikanijengea sifa kubwa mpaka uongozi wa shule ukanichagua kuwa kiranja mkuu ili niweze kuwasimamia wenzangu nilipokuwa kidato cha pili. Hakuna aliyeelewa siri ya mimi kuwa na msimamo huo, haukuwa bure, ulitokana na hofu ya kifo iliyonitawala.

Nikaendelea hivyo mpaka kumaliza kidato cha nne, matokeo yalipotoka nilikuwa nimechaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya kutwa ya Azania iliyopo jijini Dar es Salaam kwa masomo ya kidato cha tano na cha sita, Mustapha alifurahi mno na kwa sababu shule hiyo ilikuwa ya kutwa alilazimika kuwasiliana na kituo cha kulea watoto yatima cha Dogodogo ili waweze kunipokea na kunipa hifadhi kwa miaka miwili nitakayoishi jijini Dar es Salaam.

Hapakuwa na tatizo lolote kwani uongozi wa kituo hicho ulikubali kunipokea, ndipo kwa mara ya kwanza shule ilipofunguliwa, nilipanda ndege nikiwa na Mustapha na kusafiri hadi Dar es Salaam, jiji ambalo siku zote nililisikia midomoni mwa watu au kusoma kwenye magazeti.

Sasa nilitakiwa kuishi ndani yake kwa miaka miwili na pengine minne zaidi kama ningefanya vizuri kidato cha sita na kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hiyo ndiyo ilikuwa ndoto yangu. Tulipokelewa vizuri kituoni na nikatambulishwa kwa uongozi na wanafunzi wengine ambao pia walikuwa yatima na walitunzwa kwenye kituo hicho, taarifa zangu zilishatangulia kwamba nilikuwa mwanafunzi niliyeshika namba tatu Tanzania nzima kwa mtihani wa kidato cha nne, hii ilinipa heshima kubwa miongoni mwa watoto wenzangu.

Kwa mara ya kwanza nililala kwenye kituo hicho, Zamaradi akaniijia usingizini akiwa na mtoto wangu Mina, nilishangaa aliwezaje kunifuata mpaka Dar es Salaam kwa umbali wote uliokuwepo, akaniambia yeye na mtoto walikuwa ni roho, popote wanaweza kupatikana. Zamaradi aliendelea kunionya juu ya mafanikio niliyokuwa nikiyapata na tamaa ambazo zingenifuata kama nisingekuwa makini.

“Kumbuka umeoa.’
“Najua mke wangu.”
“Usinisaliti.”
“Siwezi.”
“Ukinisaliti nitakunyonya damu Samir.”
“Sitakusaliti mke wangu.”

Hayo ndiyo yalikuwa maneno yake kila siku alipokuja ndotoni, yalinitia hofu sana na kunifanya niendelee kuwa mwaminifu kwake nikiogopa kufa. Kwenye kituo cha Dogodogo, kila siku asubuhi niliamka na kutembea na wenzangu hadi shuleni ambako tulisoma mpaka saa nane mchana ndipo tukapanda basi kuturejesha maeneo ya Posta ambako kituo kilikuwa, hatukuweza kutembea kwa miguu mchana sababu ya njaa.

“Simamisha gari! Konda simamisha gari!” Nilipiga kelele nikiwa nimekaa kiti cha nyuma.
“Vipi tena dogo?”
“Nimemuona mtu.”
“Hapa siyo kwenye kituo.”

“Simama tu.”
Tulikuwa tumefika kwenye mnara wa askari na macho yangu hayakuwa yamenidanganya, nilimwona Zamaradi akiwa na mtoto mgongoni! Hiyo haikuwa ndoto ni kweli nilimwona Zamaradi. Nikaendelea kusisitiza dereva asimamishe gari lakini hakuna aliyenisikiliza hatimaye likafika kwenye kituo cha Posta ya Zamani na kusimama, hapo ndipo palikuwa mwisho wa safari.

Sikutaka kusubiri kupita mlangoni kama abiria wengine, nikaruka dirishani na kuanza kukimbia kurudi basi lilikotokea ili nimuwahi Zamaradi na mwanangu Mina, sikumuona kwenye Mnara wa Askari, nikaanza kuuliza walinzi kwenye maduka kama walimuona binti mwenye mtoto akipita maeneo hayo.

“Yule mwenye kitoto kizuri kabisa?”
“Ndiyo.” Niliitikia, mlinzi hakuwa amekosea, Mina alikuwa mtoto mzuri mno.
“Ameelekea upande huu wa baharini.”
“Asante.”

Nikaanza kukimbia kuelekea baharini, mita chache kabla sijayafikia maji nilimuona binti huyo akiwa amenitega mgongo, mtoto wake akiwa mikononi, akitembea kwa haraka kuelekea majini, nikaongeza kasi nikimfuata. Lengo langu lilikuwa ni kumshika ili nimbakize duniani, nikashuhudia akiyakanyaga maji na kuanza kuingia ndani, tayari nilishafika na kumshika mkono kwa nguvu nikimvuta atoke majini.

Alipogeuka kuniangalia kweli alikuwa Zamaradi.
“Niachie.”
“Huwezi kwenda.”
“Kwanini?”
“Nataka ubaki.”
“Siwezi.”

Tukaanza kuvutana, watu wengi wakaja wakikimbia ili kujua kilichokuwa kikiendelea mahali pale.
 MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.10.


Tulianza kuvutana nikitumia nguvu zangu zote nilizojaliwa na Mwenyezi Mungu kuhakikisha Zamaradi na mwanangu Mina hawarejei tena chini ya bahari, nilimpenda sana mke wangu na sikutaka kabisa arejee tena kwenye ulimwengu usioonekana. Vurugu ilikuwa kubwa, watu wakazidi kujaa na kutuzunguka wakishuhudia ugomvi wetu bila kufanya chochote.

“Lakini huyu ni mwanafunzi wa Azania, si mnaona sare zake?” Mwanamke mmoja alisikika akisema, tayari nilishamtoa Zamaradi ndani ya maji na kumlaza kwenye mchanga akiwa na Mina aliyekuwa akilia kwa nguvu mikononi mwake, nikaketi juu yake nikimgandamiza ili asiondoke.
“We kijana mwachie bibi wa watu.”

“Bibi gani, niacheni huyu ni mke wa...,” nilisema kwa sauti ya juu lakini kabla sijamalizia sentensi yangu nilikumbuka kuwa jambo nililotaka kulisema halikuwa la ulimwengu huu bali la ulimwengu wa ndotoni, ilikuwa siri yangu, sikutakiwa kumwambia mtu yeyote hivyo nikakomea hapo hapo lakini watu wote wakacheka kwa sauti ya juu, nikahisi waliona nimechanganyikiwa.

“Mkeo? Huyu bibi? We mtoto unaumwa?”
“Bibi yuko wapi? Naomba mniache.”
Tayari polisi walishafika na kuanza kuwapangua watu kwa kutumia virungu vyao mpaka wakanifikia nilipokuwa nimemlalia Zamaradi kwa juu, mtoto akiendelea kulia, wakanishika na kuanza kunivuta. Kwa kuwa walikuwa polisi sikuwa na sababu yoyote ya kuendelea kulumbana nao, nikamuachia Zamaradi na kusimama kando huku nikimwangalia kwa jicho la upendo.

“Vipi kijana? Mbona unamkaba bibi wa watu?” Mmoja wa wale askari aliuliza, nilipotupa macho kumwangalia mtu aliyekuwa amesimama mbele yangu, nilishangaa, nikaelewa ni kwa nini watu walikuwa wakicheka.

“Mh!” Nikaguna, hakuwa Zamaradi bali mwanamke mzee mwenye umri usiopungua miaka sitini mikononi akiwa amembeba mtoto aliyeonekana ni mjukuu wake.
“Huyu ndiyo unasema mkeo?”

Nikaanza kulia nikawa nimeinamisha kichwa changu chini kwa sababu ya aibu, nilishindwa kuelewa ni jambo gani lilitokea kwani kwa asilimia mia moja mtu niliyemuona alikuwa ni Zamaradi akiwa na mwanangu Mina, iweje tena awe bibi kizee mwenye sura mbaya kiasi hicho? Sikupata jibu, nilipokumbuka maneno ya mtu aliyenielekeza kule ambako Zamaradi alielekea nikawa na uhakika kabisa sikukosea.

“Yule mwenye kitoto kizuri?” Maneno ya mwanaume huyo yaliendelea kujirudia kichwani mwangu na kunifanya nishindwe kuelewa ni jambo gani lilitokea, sikuwa nimechanganyikiwa kama ambavyo watu wote walionizunguka walidhani.
“Unaishi wapi?” Mmoja wa wale askari aliuliza.
“Dogodogo.”
“Twende.”

Wakidhani nimechanganyikiwa, askari walinipakia ndani ya gari lao na tukaondoka moja kwa moja tukipitia Barabara ya Sokoine na baadaye kupita mitaa ya katikati ambayo siikumbuki jina mpaka tukafika kituoni ambako nilikabidhiwa kwa mkuu wa kituo baada ya kupewa historia nzima ya tukio.

“Eti Phillip kimetokea nini?” Aliuliza mkuu wa kituo akionesha mshangao.
“Sijui mama.”
“Unaumwa?”
“Hapana.”

Mkuu wa kituo akawashukuru askari kwa msaada wao kisha wakaagana, hapo ndipo akanichukua hadi ofisini kwake na kuanza kunidadisi. Sikudiriki kufungua mdomo wangu kumwambia kitu chochote juu ya Zamaradi, muda wote akizungumza nilikuwa nikilia. Akajitahidi kunifariji kwa uwezo wake wote, mwisho nilipotulia alinichukua hadi chumbani kwangu, nikapanda juu ya kitanda na kujilaza, haukupita muda mrefu sana usingizi ukanipitia na ndoto ikaanza.

“Samahani sana Samir, ni kweli nilikuja kwenye ulimwengu uonekanao kwa macho, nilitamani kukuona baada ya kukukumbuka sana. Lakini kama ujuavyo mimi na Mina si viumbe wenye miili, ni roho. Baada ya kutoka majini tuliwaingia bibi kizee mmoja na mjukuu wake tuliowakuta kando ya bahari, tukaitumia miili yao kuzunguka huku na kule tukikutafuta, tukaja hadi shuleni kwenu na kukuta unaondoka ndipo tukaanza kulifuatilia basi ulilopanda hadi ulipotuona.”

“Zamaradi.”
“Bee!”
“Ni kweli unayoyasema?”
“Ni kweli kabisa, ndiyo maana nimekuja kukuomba msamaha.”
“Ni kwa nini hukukubali kubaki kwenye ulimwengu unaoonekana nilipokuwa nakuvuta pale kando ya bahari?”

“Tusingeweza kuishi huko pamoja na wewe, tungetumia miili ya nani maana baada ya muda si mrefu wenye miili yao wangeihitaji na sisi tungekufa. Ikabidi turudi hadi ufukweni ambako tuliiacha miili hiyo na kuingia majini, ndiyo maana ukakutana na sura halisi ya bibi na mjukuu wake, nakupenda sana Samir.”
“Nakupenda sana Zamaradi, unanitesa, tutaishi maisha haya hadi lini?”

“Nisamehe mume wangu, hakuna maisha mengine tutakayoishi zaidi ya haya.”
“Lazima siku moja utoke huko Zamaradi.”
“Haiwezekani Samir.”
“Mrudishe mtoto, uje peke yako.”

Zamaradi aliondoka kwa sekunde chache tu na kurejea akiwa peke yake, akanikumbatia na wote tukalala juu ya mchanga kando ya bahari na kuanza kupapasana. Muda mrefu haukupita tulikuwa katikati ya tendo la ndoa kuthibitisha upendo wa mke na mume. Maumivu yote niliyokuwa nayo moyoni yakaisha, Zamaradi akanibusu usoni kisha akaniaga.

“Oyaa! Vipi tena? Unanifanya mimi demu wako mshikaji?” Ilikuwa ni sauti ya Zakaria, mmoja wa watoto kwenye kituo hicho ambaye nililala naye kitanda kimoja.

“Kwani vipi?” Nilimuuliza baada ya kuketi na kuwa na uhakika kabisa nilikuwa nimeota ndoto nikiwa na Zamaradi tena tukifanya mapenzi.
“Umenikumbatia halafu unanifanyia vitu vya ajabu, au wewe ni ba…?”
“Acha utani basi Zakaria, hiyo ni ndoto tu kwani wewe hujawahi kuota unafanya mapenzi?”

“Siyo leo tu, tangu uje huwa hupitishi siku mbili na unaita jina hilo hilo la Zamaradi, huyu Zamaradi unampenda sana bila shaka.”
“Ni ndoto tu.”

Je, nini kitaendelea maishani mwa Phillip? Nani alitega bomu kwenye basi na kuua watoto wote? TUKUTANE KESHO JIONI....USIKU MWEMA!!

MSICHANA NDOTONI MWANGU.....EP.10.


Tulianza kuvutana nikitumia nguvu zangu zote nilizojaliwa na Mwenyezi Mungu kuhakikisha Zamaradi na mwanangu Mina hawarejei tena chini ya bahari, nilimpenda sana mke wangu na sikutaka kabisa arejee tena kwenye ulimwengu usioonekana. Vurugu ilikuwa kubwa, watu wakazidi kujaa na kutuzunguka wakishuhudia ugomvi wetu bila kufanya chochote.

“Lakini huyu ni mwanafunzi wa Azania, si mnaona sare zake?” Mwanamke mmoja alisikika akisema, tayari nilishamtoa Zamaradi ndani ya maji na kumlaza kwenye mchanga akiwa na Mina aliyekuwa akilia kwa nguvu mikononi mwake, nikaketi juu yake nikimgandamiza ili asiondoke.
“We kijana mwachie bibi wa watu.”

“Bibi gani, niacheni huyu ni mke wa...,” nilisema kwa sauti ya juu lakini kabla sijamalizia sentensi yangu nilikumbuka kuwa jambo nililotaka kulisema halikuwa la ulimwengu huu bali la ulimwengu wa ndotoni, ilikuwa siri yangu, sikutakiwa kumwambia mtu yeyote hivyo nikakomea hapo hapo lakini watu wote wakacheka kwa sauti ya juu, nikahisi waliona nimechanganyikiwa.

“Mkeo? Huyu bibi? We mtoto unaumwa?”
“Bibi yuko wapi? Naomba mniache.”
Tayari polisi walishafika na kuanza kuwapangua watu kwa kutumia virungu vyao mpaka wakanifikia nilipokuwa nimemlalia Zamaradi kwa juu, mtoto akiendelea kulia, wakanishika na kuanza kunivuta. Kwa kuwa walikuwa polisi sikuwa na sababu yoyote ya kuendelea kulumbana nao, nikamuachia Zamaradi na kusimama kando huku nikimwangalia kwa jicho la upendo.

“Vipi kijana? Mbona unamkaba bibi wa watu?” Mmoja wa wale askari aliuliza, nilipotupa macho kumwangalia mtu aliyekuwa amesimama mbele yangu, nilishangaa, nikaelewa ni kwa nini watu walikuwa wakicheka.

“Mh!” Nikaguna, hakuwa Zamaradi bali mwanamke mzee mwenye umri usiopungua miaka sitini mikononi akiwa amembeba mtoto aliyeonekana ni mjukuu wake.
“Huyu ndiyo unasema mkeo?”

Nikaanza kulia nikawa nimeinamisha kichwa changu chini kwa sababu ya aibu, nilishindwa kuelewa ni jambo gani lilitokea kwani kwa asilimia mia moja mtu niliyemuona alikuwa ni Zamaradi akiwa na mwanangu Mina, iweje tena awe bibi kizee mwenye sura mbaya kiasi hicho? Sikupata jibu, nilipokumbuka maneno ya mtu aliyenielekeza kule ambako Zamaradi alielekea nikawa na uhakika kabisa sikukosea.

“Yule mwenye kitoto kizuri?” Maneno ya mwanaume huyo yaliendelea kujirudia kichwani mwangu na kunifanya nishindwe kuelewa ni jambo gani lilitokea, sikuwa nimechanganyikiwa kama ambavyo watu wote walionizunguka walidhani.
“Unaishi wapi?” Mmoja wa wale askari aliuliza.
“Dogodogo.”
“Twende.”

Wakidhani nimechanganyikiwa, askari walinipakia ndani ya gari lao na tukaondoka moja kwa moja tukipitia Barabara ya Sokoine na baadaye kupita mitaa ya katikati ambayo siikumbuki jina mpaka tukafika kituoni ambako nilikabidhiwa kwa mkuu wa kituo baada ya kupewa historia nzima ya tukio.

“Eti Phillip kimetokea nini?” Aliuliza mkuu wa kituo akionesha mshangao.
“Sijui mama.”
“Unaumwa?”
“Hapana.”

Mkuu wa kituo akawashukuru askari kwa msaada wao kisha wakaagana, hapo ndipo akanichukua hadi ofisini kwake na kuanza kunidadisi. Sikudiriki kufungua mdomo wangu kumwambia kitu chochote juu ya Zamaradi, muda wote akizungumza nilikuwa nikilia. Akajitahidi kunifariji kwa uwezo wake wote, mwisho nilipotulia alinichukua hadi chumbani kwangu, nikapanda juu ya kitanda na kujilaza, haukupita muda mrefu sana usingizi ukanipitia na ndoto ikaanza.

“Samahani sana Samir, ni kweli nilikuja kwenye ulimwengu uonekanao kwa macho, nilitamani kukuona baada ya kukukumbuka sana. Lakini kama ujuavyo mimi na Mina si viumbe wenye miili, ni roho. Baada ya kutoka majini tuliwaingia bibi kizee mmoja na mjukuu wake tuliowakuta kando ya bahari, tukaitumia miili yao kuzunguka huku na kule tukikutafuta, tukaja hadi shuleni kwenu na kukuta unaondoka ndipo tukaanza kulifuatilia basi ulilopanda hadi ulipotuona.”

“Zamaradi.”
“Bee!”
“Ni kweli unayoyasema?”
“Ni kweli kabisa, ndiyo maana nimekuja kukuomba msamaha.”
“Ni kwa nini hukukubali kubaki kwenye ulimwengu unaoonekana nilipokuwa nakuvuta pale kando ya bahari?”

“Tusingeweza kuishi huko pamoja na wewe, tungetumia miili ya nani maana baada ya muda si mrefu wenye miili yao wangeihitaji na sisi tungekufa. Ikabidi turudi hadi ufukweni ambako tuliiacha miili hiyo na kuingia majini, ndiyo maana ukakutana na sura halisi ya bibi na mjukuu wake, nakupenda sana Samir.”
“Nakupenda sana Zamaradi, unanitesa, tutaishi maisha haya hadi lini?”

“Nisamehe mume wangu, hakuna maisha mengine tutakayoishi zaidi ya haya.”
“Lazima siku moja utoke huko Zamaradi.”
“Haiwezekani Samir.”
“Mrudishe mtoto, uje peke yako.”

Zamaradi aliondoka kwa sekunde chache tu na kurejea akiwa peke yake, akanikumbatia na wote tukalala juu ya mchanga kando ya bahari na kuanza kupapasana. Muda mrefu haukupita tulikuwa katikati ya tendo la ndoa kuthibitisha upendo wa mke na mume. Maumivu yote niliyokuwa nayo moyoni yakaisha, Zamaradi akanibusu usoni kisha akaniaga.

“Oyaa! Vipi tena? Unanifanya mimi demu wako mshikaji?” Ilikuwa ni sauti ya Zakaria, mmoja wa watoto kwenye kituo hicho ambaye nililala naye kitanda kimoja.

“Kwani vipi?” Nilimuuliza baada ya kuketi na kuwa na uhakika kabisa nilikuwa nimeota ndoto nikiwa na Zamaradi tena tukifanya mapenzi.
“Umenikumbatia halafu unanifanyia vitu vya ajabu, au wewe ni ba…?”
“Acha utani basi Zakaria, hiyo ni ndoto tu kwani wewe hujawahi kuota unafanya mapenzi?”

“Siyo leo tu, tangu uje huwa hupitishi siku mbili na unaita jina hilo hilo la Zamaradi, huyu Zamaradi unampenda sana bila shaka.”
“Ni ndoto tu.”

Je, nini kitaendelea maishani mwa Phillip? Nani alitega bomu kwenye basi na kuua watoto wote? TUKUTANE KESHO JIONI....USIKU MWEMA!!

No comments: