Thursday, December 21, 2017

SANAA KATIKA MIKAKATI YA KUWA NCHI YA VIWANDA

Sanaa ni pana sana. Ukiangalia kila kinachokuzunguka, kina usanii ndani yake. Mpangilio wa habari katika gazeti hili, mpangilio wa lugha, mpangilio wa picha, halafu ukinyanyua macho na kuangalia vitu vilivyokuzunguka, majengo, mavazi, samani, vyombo vya usafiri, mpangilio wa rangi wa vitu hivyo au ukisikia sauti za muziki  vyote ni kazi za aina mbalimbali za sanaa. Katika zama hizi za kauli mbiu ya ‘nchi ya viwanda’, inashangaza kuwa matayarisho ya wasanii wa kuambatana na nchi ya viwanda haitiliwi mkazo, lakini bidhaa zote za viwanda zinahitaji usanii, kama ni kuchora nembo nzuri au kuweka tangazo zuri la mali au hata kutengeneza sura nzuri ya bidhaa zitakazozalishwa katika ‘nchi ya viwanda’ ni kazi ya sanaa. Bila matayarisho ya wasanii bora tutakuwa na mali nzuri zisizo na sura ya kumvutia mlaji. Hakika mpaka leo naamini kuwa kama wasanii wangehusishwa katika kukamilisha lile gari lililotengenezwa Tanzania na kupewa jina ‘nyumbu’, mambo kadhaa yangekuwa tofauti, kwanza lingepatikana jina la kuvutia zaidi na pili gari lile lingebuniwa  sura ya kuvutia zaidi. Watu wengi hununua magari kutokana na muonekano wa gari, bila hata kujiuliza mambo mengine ya kiufundi kuhusu gari husika.
 Kama nilivyosema sanaa ni pana sana leo nizungumzie sanaa ya kutumia mdomo. Binadamu wote kwa kawaida tuna midomo na pia kwa kawaida wote tunaweza kutoa sauti mbalimbali na mdomo huo. Mungu kawapa watu mbalimbali vipaji vya kuweza kutumia mdomo huo, kuna waimbaji wa staili mbalimbali, wako watambaji, waghani wa mashahiri, wasimuliaji wa hadithi, watangazaji, wachekeshaji, wahubiri, wanasiasa, na wengine wengi wa aina yao, wote hawa wanafanya sanaa zao kwa kutumia mdomo, japokuwa katika hawa hawa wengine hujiona sanaa yao ni bora kuliko ya wengine na mara nyingi hukataa katakata kuitwa wasanii.  Jambo moja lisilo pingika ni kuwa kila msanii hupenda kupata jukwaa la kuonyesha sanaa yake, na ndio maana kulibuniwa majukwaa, na hatimae majumba makubwa ya kuonyesha sanaa ambayo nayo huwa na majukwaa makubwa ya kupendeza. Wasanii hutayarisha shughuli zao  na kisha hualika watazamaji au wasilikizaji. Msanii aliyetayarisha au kutayarishiwa shughuli ni wazi ndie anayestahili kuweko jukwaa kuu kwani hata wanaokuja kumtazama wangetaka iwe hivyo ili wamuome na kumsikia vizuri. Kwenye shughuli za wasanii ambao hutumia midomo yao kuhubiri siasa, mara nyingi huweza ikaonekana ni vizuri kualika wasanii wengine, kama vile wanamuziki au wacheza ngoma au wanamuziki wa bongofleva na kadhalika ili waje wafanye sanaa zao kuleta burudani au kutoa ujumbe wa siku hiyo, kabla msanii aliyetayarisha shughuli hajapanda jukwaani na kuhubiri siasa. Katika shughuli za namna hii huwa hakuna utata sana kwani jukwaa kuu huanza kutumika na wanasiasa bila ya kuingilia. Lakini kuna tabia moja ambayo imejijenga hapa kwetu wakati shughuli inafanywa na wasanii wasio wanasiasa, ambao ili kufanikisha shughuli yao hualikwa wanasiasa, ni kawaida sana katika shughuli za namna hii ukakuta wanasiasa wamepangiwa viti kwenye jukwaa kuu na wenye shughuli kulazimika kujengewa jukwaa dogo pembeni, au kulazimika kufanya shughuli zao za sanaa kwenye sehemu ambayo hawaonekani. Nitoe mfano, siku chache zilizopita kulikuwa na shughuli kubwa ambayo ilihusu wasanii kuhamasisha uzalendo, wasanii kutoka sehemu mbalimbali nchini walikusanyika Dodoma kwa ajili ya shughuli hiyo. Shughuli ilipangwa kufanyika katika ukumbi mzuri uliojengwa kitaalamu kwa shughuli kama hizi. Na shughuli hiyo ilikuwa ikionyeshwa mubashara nchi nzima, hii iliwezesha ambao hawakuweza kuja Dodoma wafaidi na kuelewa yanayofanyika Dodoma bila wasiwasi. Siku hiyo ukumbi huu ‘ukaboreshwa’ kwa ajli ya shughuli, na  jukwaa dogo lilitengenezwa pembeni, na hapo ndipo wasanii walipopangiwa kufanya shughuli zao, katika jukwaa kubwa vikapangwa viti vya kukalia viongozi watazamaji wa maonyesho ya sanaa. Jengo hili lenye sehemu ya kukaa yenye zaidi ya viti mia tano, ikaachwa na viti vikapangwa kwenye jukwaa ambapo ndipo sehemu sahihi ya kuonyeshea kazi za sanaa. Ni nini kinasababisha ukumbi mzuri ule usitumike inavyotakiwa? Kwani viongozi wakikaa viti vya mbele na kuangalia sanaa zikiendelea jukwaani itakuwa wamedharauliwa? Mkao huo unaleta utata mwingine mkubwa kwa wasanii wanaofanya onyesho, wanakuwa katika utata, je wanafanya onyesho kwa ajili ya hadhira hivyo wawape mgongo viongozi au wanafanya onyesho kwa ajili ya viongozi hivyo waipe hadhira mgongo? Kwa aliye angalia kupitia onyesho lile kupitia luninga, onyesho lilionekana ni la hovyohovyo tu, wasanii wakionekana hawajui wanataka kufanya nini.
Baada ya viongozi kumaliza kilichowaleta wakaondoka, viti viliendelea kuwa jukwaani hivyo wasanii wakawa wanafanya maonyesho yao   chini ya jukwaa, na hivyo kutokuonekana vizuri kazi yao na watazamaji kuamua kuondoka mmoja mmoja. Matayarisho yote yamekuwa bure. Hata ule moto wa uzalendo uliotegemewa kuwashwa umegeuka cheche tu. Ushauri tu kwa wasanii wote niliyowataja hapo juu, itapendeza kila moja akiheshimu kazi ya mwenzie na kuruhusu ifanyike katika sehemu stahili, na si kujali tu kiongozi atakuwa wapi na kutokujali mamia ya hadhira yatawezaje kufaidi sanaa iliyopo ambayo imetayarishwa kwa muda mrefu na gharama kubwa..


PAKUA ANKO KITIME APP


PAKUA APP YA ANKO KITIME KWENYE SIMU YAKO UPATE TAARIFA ZOTE ZITAKAZOTUNDIKWA KWENYE www.theiringa.blogspot.com 
HABARI vichekesho PICHA video

Wednesday, November 15, 2017

HISTORIA FUPI YA DEKULA KAHANGA VUMBI


Vumbi Dekula Kahanga





Orch. Maquis Original 1987 Wapiwapi Chang'ombe Bar,kutoka kulia ni:
Mbuya Makonga "Adios",Dekula Kahanga"Vumbi",Mpoyo Kalenga na William Maselenge.
Alie chuchumaa ni Juma Choka

Kwa wapenzi wa muziki wa dansi Tanzania, jina la mpiga gitaa Dekula Kahanga Vumbi si geni, wengi hasa humfahamu kama mwanamuziki wa Maquis Original, na wanakumbuka mlio wa gitaa lake katika nyimbo kama Makumbele na Ngalula hasa pale ambapo Assossa anamhamasisha aongeze utamu kwa kutaja jina' Vumbi Vumbi'. Lakini Je, alianzia wapi? Kwanza kabisa  baba yake hakupenda kabisa apige gitaa, ulikuwa ugomvi mkubwa lakini bahati nzuri alikulia kwa bibi yake katika mji wa Uvira, mkoa wa Kivu, Jamhuri ya Kongo. Kwa bibi kama walivyo wabibi wengi, alikuwa na uhuru zaidi na akaanza kwa kutengeneza magitaa yake, ambalo yalikuwa yakivunjwa kila baba yake alipokuwa akija kumtembelea bibi yake. Jirani na alipokuwa akiishi kulikuweko na bar inaitwa Sikiya sosi ambapo palikuweko  na bendi ikiitwa Gramick Jazz, bendi iliyopitiwa na wanamuziki wengi ambao baadae walikuja Tanzania akiwemo Dr RemmyOngala. Vumbi alikuwa akisikiliza muziki ukipigwa ndani ya  hiyo bar na yeye akawa anafuatisha kwenye gitaa la kutengeza mwenyewe la nyuzi tatu, hatimae bibi yake akamnunulia gitaa dogo la nyuzi nne ambalo alikuwa anaenda nalo mpaka shule, ambapo mwalimu wake siku nyingine alikuwa akimwita awatumbuize wanafunzi wenzie. Hatimae akakutana na jamaa aliyekuwa akipiga katika bendi iliyokuwa ikimilikiwa na mapadri, akawa anamnunulia sigara huyu jamaa nae akaanza kumfundisha chords mbalimbali za kupiga gitaa. Aliendelea vizuri hatimae akajiunga na bendi hiyo ya mapadri iliyoitwa Kyalalo Band akiwa mpiga rhythm. Wanamuziki wa Kyalalo hawakuruhusiwa kujiunga na bendi zilizo kuwa zinapiga muziki kwenye bar, wala bendi yenyewe  haikuruhusiwa kwenda kupiga kwenye bar, kulikuweko na ukumbi mkubwa wa kanisa na hapo ndipo walipofanya mazoezi na maonyesho, lakini baadae Vumbi akajiunga na bendi Bavy National tena kama mpiga rhythm, 
Bavy National  Orchestre, kutoka kulia mstari wa nyuma ni Dekula (Rythm),Packot(Solo na Kiongozi),Maboko(Besi),
Merry-Djo (Drums).
Kutoka kulia mstari wa mbele,Waimbaji ni Djo-Mali,Issa Nundu na Simplice Mofeza.
Mwaka wa 1983  katika "Sikia Sosi Bar" Mjini  Uvira Mkoani Kivu Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
na hapo akakutana na mwimbaji Issa Nundu ambae alikuwa anafanya hospitali na jioni kujiunga na bendi, hatimae Kyanga Songa ambaye kazi yake ilikuwa Bwana Shamba nae alijiunga nao.
Katika kipindi hicho wakazi wa Kongo ya Mashariki, ambako kunazungumzwa Kiswahili, walikuwa wakisikiliza na kuzijua bendi nyingi kutoka Afrika ya Mashariki, bendi kama Tabora Jazz, Mangelepa, Simba wa Nyika, Mlimani Park zilisikilizwa sana, na nyimbo kama Kassim ilikuwa moja ya nyimbo maarufu wakati huo na hivyo ikawa ndoto ya Vumbi na wenzie kuwa lazima siku moja waende huko unakotoka muziki mtamu huo ili nao waweze kushiriki. Katika kipindi hicho Kyanga Songa na Issa Nundu waliondoka  kwenye bendi yao ya Bavi National na kuelekea Tanzania. Bendi ikatetereka sana, lakini nae wakati huo akawa anahamu sana ya kuja  Afrika Mashariki. Bahati nzuri mtu mmoja Alida Shanga akamjia akiwa ametumwa na Marehemu Mzee John Luanda aliyekuwa anamiliki Chamwino Jazz kuja kutafuta wanamuziki toka Kongo, nae akawachukua wanamuziki kadhaa akiwemo Vumbi na kituo chao cha kwanza kilikuwa Tandale jijini Dar es Salaam. Na siku waliofika tu na wakaanza mazoezi siku hiyo hiyo. Wakiwa vijana bado yeye na wenzie watatu walikuja wakiwa na staili ya  kuimba na kucheza steji show ambayo wakati huo iliitwa sarakasi, na pia wao ndo kilikuwa kikundi cha kwanza kuanza kurap katikati ya nyimbo. Waimbaji wakiwa ni   Sisko Lunanga, Fanfan Bwami, na mwenzao mmoja Baposta Kilosho ambae hatimae alirudi Kongo. Recording ya kwanza ilimuacha Julius Nyaisanga akishangaa vituko vya vijana hawa. Katika bendi ya Chamwino wakati huo wapiga magitaa walikuwa Vumbi Dekula, Kazembe wa Kazembe (huyu alikuwa Msukuma ambaye aliishi kwa muda Kongo na alikuwa mpiga gitaa hodari sana), na Mzee Albert, na hatimae wakamchukua Muhidin ambae alikuwa mpiga bezi wa Dr Remmy. Siku moja walienda kuomba kupiga na Maquis Original(lift), wakati huo wakipiga nyimbo za kopi, nyimbo kama Mario, Maze na kadhalika, hivyo wakazipiga hizo na watu wakafurahi sana na kuwatuza  fedha nyingi, wakachanganyikiwa maana bendi yao ya Chamwino ilikuwa haina mshahara na si mara moja walitembea kwa miguu kutoka Buguruni hadi Tandale kwa kukosa hata nauli. Japo wakati huo walikuwa wadogo kwa umri na hata umbo walifika mahala marehemu Kasheba alikuwa anawaita ‘Vimario’, upigaji wao ulikuwa mzuri sana. Nguza aliwashauri wawe wanakuja kupiga kabla Maquis hawajaanza kupiga. Hivyo wakaamua kuacha Chamwino, na wakawa wanasindikizana na Maquis, hili lilimuudhi aliyewaleta na siku moja wakiwa Silent Inn, maafisa wa Uhamiaji walikuja kuwachukua wakalazwa Central Police na kisha kupelekwa gereza la Keko. Wakiwa huko walimwandikia Mzee Luanda kuwa wanarudi Chamwino, basi wakaachiwa na kurudi kusuka upya Chamwino Jazz. Lakini hawakukaa muda mrefu Mzee Makassy akaja kuwaomba waingie katika bendi yake, wenzake waimbaji  wakaenda  yeye akabaki Chamwino, lakini muda si mrefu Nguza akamwambia aandike barua ajiunge na Maquis. Nae akafanya hivyo na ndio kujiunga rasmi na Maquis kama mpiga gitaa la second solo. Aliwakuta wanamuziki kama Maneno Uvuruge, Omari Makuka, Keppy kiombile, Ilunga Lubaba, William Maselenge na wengine wengi.  Aliendelea kupiga second solo hadi siku moja bendi ilikuwa inapiga maeneo ya Ukonga, kwa kawaida Mzee Lubaba alikuwa anapiga kuanzia saa tatu mpaka saa sita, na  kisha Nguza Viking akiingia na kuendelea .
Maquis wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma,  wa pili toka kulia na shati jeusi Vumbi, wapili toka kushoto na suruali nyeusi Issa Nundu
Siku hiyo Nguza hakuonekana Vumbi  akaweza kupiga nyimbo zote za Nguza, na kesho yake  akaambiwa afike ofisini akasainishwa rasmi mkataba wa kuwa mwanamuziki wa Maquis.  Baada ya muda mfupi Nguza akaacha bendi.
Muda mfupi baada ya hapo walirekodi ule wimbo maarufu wa Makumbele, solo ya wimbo huu ilikuwa awali ikipigwa na Mzee Lubaba, lakini afya ya mzee Lubaba ilianza kuzorota nae akawa anawafundisha nyimbo zake wanamuziki wengine, wimbo wa Makumbele alifundishwa  Omari Makuka na akawa anaupiga katika maonyesho mbalimbali, lakini wakati wa kutaka kurekodi kamati ya uongozi ya Maquis iliamua Vumbi aufanyie mazoezi  na aurekodi. Kurekodi kwa album ya Makumbele ilitokana na safari ndefu ya bendi ambayo ilichukua miezi mitatu katika mikoa ya Ziwa, hivyo bendi iliporudi Dar  ilikuta sifa ya bendi imepungua, hivyo walirekodi album ya Makumbele iliyokuwa na nyimbo kama Tipwatipwa, Ngalula na Makumbele, sifa ya bendi ikarudi juu tena kwa mara nyingine. Na ni wakati huo ambapo bendi ilihamia katika ukumbi wa Lang’ata Kinondoni. Vumbi aliedelea kupiga katika bedi hii mpaka alipoamua kuhamia Sweden ambako yuko mpaka leo akiendelea kupiga muziki.




Sunday, November 12, 2017

JE UTAMU WA GITAA LA RYTHM UTAWEZA KURUDI TENA?

Harrison Siwale (Satchmo) mpiga rythm, Mbaraka Mwinyishehe mpiga solo, Abdul Mketema mpuliza saksafoni
Katika mfumo wa awali kuanzia miaka ya 50,  bendi zilikuwa  na mfumo wa kutumia magitaa matatu, Solo, rythm na Bass. Gitaa la solo lilikuwa na sauti ya juu, huku rythm ikiwa na sauti nzito kidogo ya kati, na mwisho Bass likiwa na sauti nzito kuliko magitaa mengine. Kimuundo gitaa la rythm na la solo hakuna tofauti. Yote yana nyuzi 6,lakini katika kutyuni kwenye amplifier, gitaa la rythm hunyimwa treble (ukali) kiasi na kuongeza bass zaidi kuliko gitaa la solo ambalo huwa na treble zaidi ya magitaa mengine. Mwanzoni mwa miaka ya 60 likaanza kutumika gitaa la nne lililojulikana kama 'second solo' au Wakongo waliliita 'mi solo'. Inasemekana kaka yake mpiga solo maarufu wa Kongo wa enzi hizo Dr Nico, ndie aliyeanzisha mtindo wa kuongeza gitaa hilo la nne. Hili lilikuwa likipigwa kwa mifumo mbalimbali katika bendi mbali mbali. Bendi nyingine zilitumia second solo kama gitaa lililokuwa linajibizana na solo, na bendi nyingine lilikuwa linajibizana na rythm,na hata kulikuweko mfumo ambapo gitaa hilo aidha lilikuwa likipiga 'harmony ya gitaa la solo au ya gitaa la rythm. Bendi nyingine , mfano  Cuban Marimba chini ya Juma Kilaza liliongeza ubunifu na kuongeza gitaa la 5 na kuliita 'chord guitar'. Ubunifu huu uliongeza sana uzito wa muziki na hata kuleta ladha mbalimbali za muziki wa dansi. Na uamuzi wa aina ya mpangilio wa magitaa uliweza kuleta tofauti kubwa kati yabendi moja na nyingine.
Lakini katika makala ya leo tuzungumzie gitaa la rythm. Chombo hiki bado kinapigwa katika bendi nyingi lakini umuhimu wake umeshuka sana. Katika kipindi cha miaka ya 60 na 70, gitaa hili lilikuwa na umuhimu mkubwa na wapigaji wake waliweza kubuni staili zao wenyewe. N kujijengea sifa kubwa. Kati ya wapiga rythm maarufu alikuweko Satchmo, hilo ndio lilikuwa jina la kisanii la Harrison Siwale, huyu alikuwa Mzambia aliyekuja weka masikani yake katika mji wa Tanga. Alipitia bendi kubwa za Tanga ikiwemo Atomic Jazz Band na hatimae Jamhuri Jazz Band. Satchmo alikuwa na staili peke yake ya kupiga rythm, sikumbuki kusikia mtu mwingine akipiga rythm ya aina yake kabla ya hapo, lakini hakika wapiga rythm wengi walichukua mtindo wake na kubuni vionjo vya aina yao. Rythm yake ilitawala nyimbo za Jamhuri Jazz Band wakati huo. Ufundi wake unaonekana sana katika nyimbo kama Mganga no 1 na 2, au Blandina. Kule Tabora  Mzee Kasim Kaluwona nae alikuwa na staili tofauti ya upigaji wa gitaa la rythm uliyoifanya Tabora Jazz kuwa na staili yake peke yake, kumbuka gitaa lake katika wimbo Asha, au Dada Lemmy. Charles Kazembe akiwa na Morogoro Jazz anakumbukwa katika upigaji wa rythm kwenye nyimbo kama Wajomba Wamechacha. Hao ni wachache tu kulikoweko na wengi marufu. Katika kipindi hiki huko Zaire kulikuwa na mipigo mbalimbali ya gitaa la rythm, ila kitu kipya kikaanzishwa ambapo katika ufungaji wa nyuzi ,wapiga rythm wakauondoa uzi namba nne katika gitaa hilo na kuweka uzi namba moja, hivyo kukawa na nyuzi namba moja 2 katika gitaa moja, hapo ndipo akina Vata Mombasa wakaweza kuleta utamu mpya katika upigaji wa rythm, ufungaji wa aina hii wa nyuzi za gitaa ulifahamika kama 'double string'. Wakati huo Orchestra Kiam wakawa wanajivunia kupiga rythm kwa spidi kali sana,vibao kama Kamiki, Bomoto ni ushahidi wa kazi hizo. Utamu wa ufungaji wa nyuzi kwa staili hii uliweza kusikika vizuri katika gitaa lililopigwa mwanzo kabisa wa wimbo Andoya. Umuhimu wa gitaa la rythm ulikuwa ukionekana kwa bendi nyingi kuwa na mtindo wa 'kuachia rythm', huo ulikuwa ni mpangilio ambapo gitaa la rythm liliachwa lipige peke yake wakati magitaa mengine yakiwa kimya. Hapo mpiga rythm aliachiwa kucheza na gitaa alivyotaka na  kuonyesha umahiri wake wote. Mtindo huu ulipendwa sana na wapenzi wa muziki. Utaratibu huu umerudi kwa njia ya ajabu sana, bendi nyingi za  taarab vimeanza 'kuachia rythm' lakini kwa kuwa bendi hizo hazitumii tena gitaa la rythm , jukumu hili linafanywa na mpiga solo, tena vipande vingi vinavyopigwa ni vile vilivyopigwa na bendi za zamani!!  matokeo ni yaleyale, wapenzi wa muziki hupanda mzuka na kucheza sana wakati wa kipindi hicho. 
Kwa ujumla bendi nyingi za dansi hazitilii umuhimu tena gitaa la rythm. Kinanda kimechukua nafasi ya gitaa hili. Kuna bendi ambazo zinalo gitaa la rythm lakini kwa mfumo wa sasa wa muimbaji kuchukua nafasi kubwa ya wimbo gitaa hilo limerudishwa nyuma sana. Lakini kwenye muziki kila kitu kina utamu wake kamwe chombo kimoja hakiwezi kuziba pengo la chombo kingine.

Friday, October 13, 2017

MUZIKI ENZI ZA NYERERE

LEO ni miaka 18 toka Kifo cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mungu amlaze pema Mwalimu. Vyombo vya habari vinaeleza mengi kuhusu hali ya maisha ilivyokuwa zama za Enzi ya Nyerere, kwa tuliekuweko enzi hizo tunaona mengi yanayosemwa ni ya kweli na mengi si sahihi, mengine yanatungwa ili kufanikisha azma fulani, mengine si kweli kwa kuwa mtoa habari hakuweko au alihadithiwa na mtu ambaye hakuwa mkweli au pengine hakumbuki vizuri, lakini hiyo ndio hali halisi kutokana na kuwa mengi yaliyokuwa yakitendeka wakati ule hayakuwekwa katika maandishi kutokana na uwoga wa kusema ukweli enzi hizo, uchache wa vyombo huru vya mawasiliano, na kutokana na ukweli kuwa hata sasa ni vizuri uchunge unachosema kuhusu Mwalimu hasa kama ni mwanasiasa unaweza ukajikuta unatengwa na jamii ukionekana unakinzana na Mwalimu!!!!. Lakini mimi si mwanasiasa ni mwanamuziki, na leo nitasimulia ilikuwaje kuwa mwanamuziki enzi za Mwalimu. Mimi ni mzaliwa wa Iringa, nilipata bahati kuzaliwa katika nyumba ambayo muziki ulikuwa sehemu kubwa ya maisha. Moja ya starehe kubwa ya wazazi wangu ilikuwa muziki, baba yangu alikuwa mpiga gitaa mzuri aliyerekodi nyimbo zake kwa mara ya kwanza Tanganyika Broadcasting Services (TBC) mwaka 1960 na nyimbo hizo kupigwa kwa mara ya kwanza katika kipindi cha Jimbo Letu, 16 May 1960. baba alilipwa shilingi 40. Hili ni ushahidi kuwa kabla ya Uhuru wanamuziki walilipwa mirabaha kila nyimbo zao zilipopigwa katika redio miaka hiyo. Niliwahi kumuona baba pia akipiga accordeon, trumpet na saxophone, ila chombo chake haswa kilikuwa gitaa lisilotumia umeme, acoustic guitar, ambalo alikuwa akipiga katika  mtindo wa Folk Music, au mtindo wa kupiga gitaa kwa kutumia vionjo vya utamaduni asili wa mpigaji, nae tungo zake zilitokana na utamaduni wa kabila lake la Kihehe. Hivyo nilipokuwa mdogo nilishirikishwa kuimba wakati akipiga gitaa na kuupenda muziki toka nikiwa na umri mdogo. Pia nyumbani tulikuwa na radio na gramaphone iliyokuwa na santuri za muziki aina mbalimbali,muziki wa Kiswahili, Kihindi, Kiingereza na muziki toka Afrika ya Kusini na Kongo, hivyo muziki ulikuwa masikioni muda mwingi wa maisha yangu ya awali.  Nilianza shule mwaka uleule ambapo Tanganyika ilipata Uhuru, nakumbuka tulifagia barabara za jirani na shule yetu kisha kuzimwagia maji siku moja kabla ya Uhuru, ili siku ya Uhuru kusiwe na vumbi.
Shuleni kulikuwa na kipindi kilichoitwa ‘Kuimba’, mwalimu alihakikisha anafundisha japo wimbo mmoja kwa wiki, vitabu maalumu vilikuwepo vikiwa na nyimbo zilizokuwa na mafunzo ya maisha, kuheshimu wazazi, wakubwa, kupenda shule na kadhalika. Somo hili lilikuweko katika ngazi zote za shule za msingi, na kulikuweko waalimu wengi waliokuwa wakijua kusoma na kuandika muziki kwa nota hivyo wanafunzi kupewa elimu ya muziki zaidi ya kuimba nyimbo. Shule zote zilikuwa na bendi ya shule. Ambayo kila asubuhi bendi  ilipiga muziki wakati wanafunzi wakikaguliwa kama wamekuja shuleni wasafi, moja ya ndoto zangu ilikuwakuja kuwa mmoja wa wana bendi ya shule. Nilitamani aidha kuwa mpiga ngoma au mpiga filimbi na kubwa kuliko yote ni kupata bahati kuwa mshika kifimbo. Shule zilishindana kwa kuzivalisha bendi mavazi bora na upigaji kuwa makini na hivyo siku za sikukuu kila shule ilijitahidi bendi yake ndio iwe bora. Hakika nakumbuka raha iliyokuwepo wakati shule mbalimbali zilipokutana siku ya siku kuu au kukiwa na maandamo na kisha kila bendi kupita mbele ya mgeni wa heshima, wanafunzi tulijitahidi kuwa wasafi, wakakamavu na wenye nidhamu ili shule yetu ishinde.  

Kila shule ilikuwa na vikundi vya kwaya, ngoma za asili na nyingine kuwa na bendi za muziki wa kisasa. Nilisoma shule iliyokuwa na wahindi wengi, Iringa Aga Khan Primary School, bila kujali kabila wote tulicheza ngoma za asili. Hakika kulikuwa na wahindi wanajua kucheza sindimba kuliko waswahili. Siasa ya Ujamaa iliingia wakati niko darasa la saba. Mambo mengi yalibadilika, nyimbo, ngoma ngonjera, mashahiri yakanza kuwa ni ya kisiasa, nyimbo nyingi za kiasili zikapewa maneno ya kisiasa, maafisa utamaduni ndio walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha hili, kwa kuzunguka kuhamasisha na hata kutoa adhabu kwa vikundi vilivyoonekana havitaki kuimba nyimbo za siasa. Mashuleni tulianza kuimba nyimbo za siasa kwa uwingi zaidi, somo la kuimba lilikuwa likifundisha nyimbo za siasa tu. Kwaya zilizokuwa na nyimbo mbalimbali za siasa kutoka kila upande wa nchi, zilirekodiwa na Radio ya Taifa ambayo kwa wakati huu iliitwa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD). Uzalendo ulikuwa ndio ‘habari ya mjini’. Kila mwisho wa onyesho la muziki bendi zililazimika kupiga ule wimbo wa ‘Chama cha Mapinduzi chajenga nchi’. TANU Youth League (TYL) ilikuwa na matawi kila mahala. Kimuziki TYL ilichangia sana, kwani kila kwenye tawi la TYL lazima kulikuwa na kundi la muziki aidha kwaya au ngoma, na mara nyingi vyote na sehemu nyingi TYL pia ilinunua vyombo vya bendi na hivyo karibu kila wilaya ilikuwa na bendi. Hapa ndipo wanamuziki wengi maarufu wa miaka hiyo na ambao nyimbo zao bado maarufu mpaka leo walikotokea. Pale Iringa, vyombo vya TYL hatimae viliishia kuwa chini ya shule ya Sekondari ya Mkwawa na hivyo pale kulikuwa na bendi nzuri sana ambayo iliweza kuja kurekodi RTD ikiwa na mtindo wao wa Ligija, kati ya waliokuwa wanamuziki wa bendi hiyo, mpia solo ni mzazi wa producer mmoja maarufu wa Bongo fleva na hata yeye alikuja kuwa na bendi yake TZ Brothers, mpiga rythmambaye  kwa sasa ana chuo kikubwa cha muziki pale Tabata, wakati muimbaji mmoja wa bendi hiyo alianzisha bendi maarufu pale Arusha.  Mashirika ya umma, taasisi mbalimbali za kiserikali zilihamasishwa kuwa na vikundi vya utamaduni ambavyo ndani yake kulikuwa na kwaya, bendi na ngoma za asili. Vingi vilikuja kuwa maarufu nchi nzima, kama vile BIMA, vikundi vya majeshi yote, DDC, TANCUT, UDA, URAFIKI ana kadhalika. Pamoja na kutoa burudani vikundi hivi vilijenga uzalendo kwa vijana wa wakati ule. Hakika uzalendo kwa sasa si moja ya vipaumbele na matokeo ya hili ni janga kubwa kwa Taifa .

Miaka 28 bila Franco Luambo Luanzo Makiadi

Franco Luambo Luanzo
François Luambo Luanzo Makiadi  alizaliwa 6 July 1938, katika kijiji cha Soni Bata magharibi mwa jimbo la Bas Zaire huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Wakati akiwa bado mchanga wazazi wake walihamia jiji la Leopodville ambalo sasa linaitwa Kinshasa. Baba yake aliitwa Joseph Emongo alikuwa mfanyakazi wa shirika la reli, wakati huo mama yake alikuwa akiuza maandazi sokoni. Alipofikia umri wa miaka saba alitengeza gitaa lake akawa analipiga kwenye genge la mama yake ili kuita wateja. Mwanamuziki maarufu Paul Ebengo Dewayon ndie aliyegundua kipaji cha mtoto huyu na kuanza kumfundisha rasmi namna ya kupiga gitaa. Mwaka 1950 akiwa na umri mdogo wa miaka 12 alichukuliwa rasmi kama mwanamuziki wa bendi ya Watam iliyokuwa inaongozwa na Dewayon. Kipaji chake kiliwashangaza wengi hasa kwa vile alikuwa akionekana umbo lake likilingana na ukubwa wa gitaa analolipiga, lakini akiwa analipiga kwa umakini mkubwa. Akiwa na miaka 15 alirekodi wimbo wake wa kwanza ulioitwa Bolingo na ngai na Beatrice (Mapenzi yangu kwa Beatrice). Wimbo huu aliutunga alipojiunga na bendi iliyokuwa inamilikiwa na Studio za Loningisa. Kiongozi wa bendi hiyo Henri Bowane ndie aliyeanza kufupisha jina la mwanamuziki huyu na kumuita Franco, jina alilokuja kujulikana nalo maisha yake yote. Mwaka 1955 alianzisha bendi akishirikiana na Jean Serge Essous, bendi ilizinduliwa katika ukumbi wa OK Bar, hatimae bendi ilichukua jina la OK Jazz kwa heshima ya bar ambapo ilizinduliwa.Katika muda mfupi ikiwa na mwimbaji Vicky Longomba(Baba yake Lovy Longomba) walianza kuwa bendi pinzani ya bendi kongwe ya African Jazz iliyokuwa inaongozwa na Joseph Kabasele maarufu kwa sifa ya Grand Kalle. Mwaka 1958 Franco aliteuliwa kuwa kiongozi na mtunzi mkuu wa Ok Jazz,  kundi alilokuja kulijenga kwa kuanzia watu 6 hadi kufikia  watu 30 kwenye mwaka 1980. Franco mwenyewe alikuwa anasema OK Jazz iliweza kutoa album 150 katika miaka 30 ya bendi hiyo.Mwaka 1958 Franco alifungwa kwa mara ya kwanza kwa kosa la uendeshaji mbaya wa gari, lakini siku ya kutoka kwake jela ilikuwa kama shujaa katoka vitani, inasemekana sababu ya kufungwa ilikuwa ya kisiasa zaidi kwani alikuwa katunga wimbo ambao haukupendeza wakoloni wakati ule. 1960 Vicky Longomba aliacha bendi. Lakini wakati huo Kongo ilikuwa kwenye vuguvugu za kutafuta uhuru na nchi ilikuwa si shwari Franco akahamia Ubelgiji. Baada ya Mobutu Sese Seko kushika nchi na kukawa na amani katika nchi iliyoitwa sasa Zaire,  Franco akarudi kwao mwaka 1966. Akashiriki katika Tamasha la Sanaa Za Afrika lililofanyika Kinshasa 1966 na Franco akawa kipenzi cha serikali ya Mobutu.
Franco hakuwa tu mwanamuziki mzuri bali pia aliendesha vizuri sana biashara zake za kurekodi na kampuni alizozianzisha wakati huo. Alikuwa na lebo kama (Surboum OK Jazz, Epanza Makita, Boma Bango and Éditions Populaires). Katika miaka ya 70 muziki wa Kongo ulishika kasi sana Afrika na Franco akiongoza jahazi kwa nyimbo kama Infidelité Mado,  na akaendeleza kupiga mitindo mbalimbali kama Bolelo na muziki uliotokana na ngoma za asili toka Kongo zikichanganywa na mapigo kutoka Cuba na kuanza upigaji wa gitaa uliokuja itwa Sebene.
 
Bavon  Marie Marie
Mwaka 1970 Franco alimpoteza mdogo wake ambaye nae alikuwa mpiga gitaa mashuhuri Bavon Marie-Marie Siongo ambaye alifariki katika ajali ya gari. Lilikuwa pigo kubwa kwa Franco kwa miezi kadhaa aliaacha hata kupiga muziki. Baada ya hapo OK Jazz ilibadili jina na sasa kuitwa TP OK Jazz na mwaka 1973 kutoa kibao kingine kilichotikisa Afrika, AZDA.  Wimbo huu kwanza ulirekodiwa kama tangazo kwa ajili ya  kampuni ya Volkswagen VW. Mahusiano yake na Mobutu yalikuwa na mawimbi mara wakipatana mara wakikosana kutokana na Franco kuwa anatumia nyimbo zake kukosoa serikali ya Mobutu. 1970 Franco alikuwa ni Rais wa wanamuziki wa Kongo na pia kuajiliwa na kampuni ya kugawa mirabaha ya wanamuziki. Aliendelea kutajirika kwa kuweza hata kunua ardhi nchini Ufaransa, Ubergiji na Kongo, na kuwa na nightclub 4 kubwa kuliko zote Kinshasa kwa wakati huo na kufanya club mojawapo
kuwa ndio makao makuu yake. Hapo ilijengwa studio kubwa, office na apartment za kuishi kadhaa. Mwaka 1978 alitiwa mbaroni  tena baada ya kugundulika kuwa alikuwa anasambaza nyimbo zenye matusi ambazo hakuzipitisha katika  kamati ya kuchunguza mashairi kama ilivyokuwa kawaida wakati ule. Kufikia kipindi hiki TPOK Jazz  ilikuwa kubwa kiasi iliweza kumeguka kuwa mbili moja ikifanya kazi Afrika wakati nyingine ikiwa inafanya maonyesho Ulaya. !983 Franco alifanya maonyesho kadhaa Marekani lakini hayakufanikiwa haijajulikana mpaka leo sababu za kushindikana huko. Katikati ya miaka ya 70 Franco alibadili dini na kuwa Muislam na kupewa jina la Abubakkar Siddiki, japo hakuonekana kufuata taratibu zozote za Kiislamu na akaendelea kuitwa Franco. 1980, Franco alitajwa kama ndie Grand Master wa muziki wa Kongo na serikali ya nchi hiyo, nyimbo zake nyingi zikaanza kuwa zinasifia utawala ulikuweko madarakani. 1985 Franco alitoa wimbo ambao uliuza kuliko nyimbo zake zote, wimbo ulioitwa Mario,  wimbo ambao ulikuwa ni hadithi ya mwanaume kijana  ambae alikuwa anategemea akina mama watu wazima wamlee.
Franco
1987 zilianza habari kuwa Franco anaumwa sana, na kwa mwaka ule alitoa wimbo mmoja Attention Na SIDA
 (Jihadhari na UKIMWI), wimbo huu ukaanzisha maneno kuwa pengine Franco amekwisha pata ugonjwa huu. Franco akawa taratibu anakosekana kwenye shughuli za bendi nayo ikaanza kumeguka kutokana na kutokuwa na uongozi thabiti. Franco tena akarudi kwenye dini yake ya awali ya Roman Catholic. Tarehe 12 Oktoba 1989, Franco alifariki katika hospitali moja Ubelgiji. Mwili wake ukarudishwa Kongo, sanduku likiwa limefunikwa bendera ya Taifa lake na kupitishwa katika mitaa ya Kinshasa na kuagwa na maelfu ya wapenzi wake. Serikali ikatangaza siku 4 za maombolezo ambapo redio ya serikali ilipiga nyimbo za Franco tu. Franco alizikwa tarehe17 Oktoba 1989. Alifariki akiwa na miaka 51. Mungu amlaze pema peponi


Thursday, October 12, 2017

PICHA ZA ZIADA ZA MAZISHI YA SHABANI YOHANA WANTED

 JITIHADA ZA WANAMUZIKI HAWA WAKONGWE ZILIFANIKISHA MAZISHI YA MWANAMUZIKI MWENZAO.






 HATIMAE SAFARI YA KWENDA MICHUNGWANI KWA MAZISHI ILIANZA


  KWAMGWE KIJIJI ALIKOZIKWA SHABANI YOHANA WANTED






 WANAMUZIKI WALIKUTANA NA MZEE MASONGI











 IBADA  YA MAZISHI NYUMBANI









 KANISANI










 MAZISHI









































 PICHA BAADA YA MAZISHI














 KURUDI NYUMBANI