Wednesday, December 14, 2016
MWISHO WA LUTUMBA SIMARO KATIKA TP OK JAZZ
BANNING EYRE ni mwandishi Mmarekani aliyefanya mazungumzo na mwanamuziki Lutumba Simaro mpiga gitaa wa kundi la OK Jazz, kuna mengi ya kujifunza kwa wanamuziki wa Tanzania
SWALI: Nini kinaendelea katika muziki wa Kongo siku hizi?
SIMARO: Kinachoendelea sasa sikipingi, mi ndio baba yao, hawa vijana kuna kitu walichoingiza katika muziki. Wameleta damu mpya na ujana kweli lakini,kuna monotony mno, Huwezi kutofautisha bendi moja na nyingine. Wanavyoimba, wanavyocheza na wanavyopiga mgitaa katika kile wanachoita seben. Kuna mtangazaji mmoja anaitwa Gaspar wa Studio Maximum, ana kipindi kimoja ambapo nilikuwa nasikia wimbo wa Werrason lakini alikuwa JB anecheza na wimbo wa JB ukichezwa show na Werra, kwa kweli huwezi kuona tofauti ya muziki wa hawa wawili.
Enzi za OK Jazz, Franco alikuwa mtunzi mzuri sana, mimi nikajiunga nikaleta style yangu, Josky alipokuja nae akaleta staili yake. Ndombe nae pia akaja na staili yake. Wote tulikuwa OK Jazz, gitaa la Franco ndilo lilitawala na kuweka nembo ya staili zetu mbalimbali. Papa Wemba akiimba najua ni Papa Wemba ana staili yake. Mdogo wangu Kofi nae anastaili yake, Zaiko ya Nyoka Longo pia wana staili yao
Kama wangeweza kunisikiliza ningewaambia hivi hawa vijana wanajitoa Wenge na kuanzisha makundi yao, ni muhimu kuja na utofauti, wana waimbaji wazuri sana, watunzi wazuri na wamepata bahati kuweza kurekodi katika studio za kisasa wana jukumu la kuendeleza ubunifu. Wakati wetu wa enzi za Vicky Longomba, Mujos na Kabasele, kama we ni mwimbaji ulilazimika kuimba aina mbalimbali za muziki. Muziki wa Ulaya au Marekan na kwa staili mbalimbali. Mtu akiomba Tango, unapiga Tango , ukitakiwa kuimba Waltz uliimba style hiyo, lakini waimbaji wetu wa sasa, hakuna kitu. Na wapiga magitaa pia, tulikuwa na wapiga magitaa wakali kama Papa Noel, na Tino Baroza, na hata Franco. Wapiga magitaa siku hizi ukiwauliza unamfahamu Nico Kasanda? Tuno Baroza? Kimya kinatawala. Muhimu kujua staili zao ili kujitafutia stail mpya. Nina mpiga gitaa ana miaka 20, wiki iliyopita nilimpa sanduku zima la santuri akafanye mazoezi, nashukuru ameanza kuniuliza maswali mengi kuhusu upigaji mbalimbali. Utunzi nao unapwaya pia utakuta wimbo unataja majina ya watu 200, wanaita “mabanga”, nawauliza majina mengi ya nini wananiambia hawa huwa wanawalipa vizuri.
Vijana wana bahati wana teknolojia nzuri, wana TV nyingi na nzuri za kuweza kuwafanyia promotion, Wakati wetu tulikuwa na radio moja tu, hivyo ililazimu kufanya kazi nzuri ili ujulikane. Nawakumbuka Soki Dianzenza na Soki Vangu walikuja na kitu kipya, Nyboma, Pepe Kalle wote watakumbukwa kwa aina yao ya uimbaji.
Nimeitafsiri kwa ruksa ya Banning Eyre. Kwa habari nyingi zaidi angalia <www.afropop.org>
Monday, December 5, 2016
SITI BINTI SADI SUPER STAR WA KWELI
Kwa akina mama wanamuziki katika Taarabu, alikuwa ndio ufunguo ya mfumo uliopo ambao taarab inaongozwa na waimbaji wa kike.
Alikuwa ndie mwasisi wa kuimba taarab kwa Kiswahili.
Kwa wanamuziki wote kwa ujumla Siti Binti Sadi ni super star wa kweli.
- Alirekodi santuri zaidi ya 150
- Alikuwa wa kwanza kwenda kurekodi nyimbo zake India May 1928
- Umaarufu wake ulisababisha Columbia Records ya India kujenga studio Zanzibar katika enzi yake ili tu kumrekodi.
Oktoba 1936 aliwahi kufanya onyesho moja huko Pangani na kupata shilingi 1200/-. Kwa thamani ya pesa wakati ule, mtu aliweza kupanga chumba kwa shilingi 1 kwa mwezi. Na Pangani ilikuwa na wastani wa watu 1500. Si rahisi msanii yoyote wa leo hapa nchini kuweza kufikia Usuper Star huo.Kufanya onyesho na kuteka mji mzima.
Siti alizaliwa mnamo mwaka 1880 na kufariki 1950.
Tuesday, November 29, 2016
NI MIAKA MITATU TOKA KIFO CHA NGULI TABU LEY
Mokolo mosusu ngai nakanisi
Naloti lokola ngai nakolala aah mama
Mokolo nakokufa
Mokolo nakokufa, nani akolela ngai ?
Nakoyeba te o tika namilela.
Liwa ya zamba soki mpe liwa ya mboka
Liwa ya mpasi soki mpe liwa ya mai O mama
Mokolo nakokufa
Kwa kifupi maana ya maneno haya ni;
Siku moja niliona kama nimeota siku yangu ya kufa,
Siku ya kufa nani atanililia? Sijui labda nitabiri.
Ntafia porini au nyumbani?
Kifo changu kitakuwa cha maumivu au kuzama majini?
Ahh siku yangu ya kufa.
Tabu Ley maarufu kwa jina na Rochereau, alizaliwa mwaka 1940 huko Bandundu katika Jamhuri ya Demokrasi ya Kongo. Alianza maisha akiitwa Pascal Emmanuel Sinamoyi Tabu, jina la Rocherau lilikuwa ni jina la utani toka shuleni na ndilo alilolitumia alipopeleka nyimbo zake za kwanza kwa Joseph Kabasele wakati akiomba kujiunga na bendi ya African Jazz. . Tabu Ley alianza maisha yake ya muziki mapema sana na 1954 akiwa na umri wa miaka 14 tu aliandika wimbo wake wa kwanza Bessama Muchacha, ambao akaurekodi na kundi maarufu la African Jazz lililokuwa chini ya Joseph ‘Grande Kalle’ Kasebele, (asichanganywe na Pepe Kalle). Aliendelea na shule na hatimae alipomaliza High School 1959, ndipo alipojiunga rasmi na African Jazz. Alikuwa mmoj awapo wa walioimba ule wimbo utunzi wa Grande Kalle, na uliotikisa anga la Afrika miaka ya 60, Independence Cha Cha. Uliogeuka na kuwa wimbo rasmi wa kusherehekea uhuru wa kongo.
Baada ya kiasi kama miaka minne alijiengua bendi hii na akiwa na mpiga gitaa mahiri Nicholaus Kassanda aka Dr Nico, wakaanzisha African Fiesta, ambapo alikuweko hadi 1965, wakati Kongo imewaka moto kimuziki na ushindani kuwa mkali sana, akaachana na Dr Nico na kuanzisha African Fiesta National au mara nyingine ikiitwa Africa Fiesta Flash, Wanamuziki kama Papa Wemba na Sam Mangwana ni kati ya wakongwe waliowahi kupitia katika kundi hili tishio.
Kufikia mwaka wa 70, Tabu Ley alianzisha Orchestre Afrisa International wakati huo Afrisa na TPOK Jazz ndizo zilikuwa bendi maarufu zaidi Afrika. Afrisa waliteremsha vibao kama Sorozo, Kaful Mayay, Aon Aon, na Mose Konzo na Tabu Ley aliweza hata kupata tuzo toka serikali za nchi kama Chad iliyompa heshima ya Officer of The National Order, wakati Senegal ilimpa heshima ya Knight of Senegal, na akawa sasa anaitwa Siegneur Rochereau. Katikati ya miaka ya 80 Tabu Ley aligundua kipaji cha mwanamama aliyekuja kutikisa anga za Afrika naye si mwingine ila Mbilia Bel, baadae Tabu alimuoa Mbilia a wakapata mtoto mmoja. Nyimbo kama Nadina, Nakei Nairobi zinaonyesha kipaji gani alikuwa nacho binti huyu aliyekuwa mzuri kwa sura, aliyejua pia kucheza na kutawala jukwaa vizuri. 1988 Tabu akamgundua muimbaji wa kike mwingine Faya Tess. Hapo Mbilia akaacha bendi na kuendelea na maisha yake ya muziki peke yake.
Kipindi hiki, mtindo wa Soukus uliokuwa na mapigo yenye mwendokasi zaidi ya lile rumba la Afrisa na TPOK Jazz ulianza kuzishika nyoyo za vijana, bendi hizi kubwa zikaanza kufifia.
Mwanzoni mwa miaka ya 90 Tabu Ley alihamia Marekani akaishi Kusini mwa California, akabadili muziki wake katika kujaribu kujikita zaidi katika soko la ‘Kimataifa’, akatunga nyimbo kama Muzina, Exil Ley, Babeti Soukous. 1996 Tabu Ley alishiriki katika album ya kundi la Africando na kushiriki katika wimbo Paquita wimbo aliyokuwa ameurekodi miaka ya 60 akiwa na African Fiesta. Tabu alipata cheo cha Uwaziri katika utawala wa Laurent Kabila baada ya kuondolewa kwa Mobutu. Hata baada ya kifo cha Laurent Kabila November 2005 Tabu alipewa cheo cha Vice-Governor in charge of political, administrative, and socio-cultural questions, kwenye jiji la Kinshasa.
Mwaka 2006 Tabu Ley akashirikiana na rafiki yake wa muda mrefu Maika munah na kutoa album yake ya mwisho iliyoitwa Tempelo, katika album hiyo kuna wimbo ambao ni kama kumbukumbu ya kote alikopita na pia akaimba wimbo mmoja na binti yake Melodie.
Mwaka 2008 alipata mshtuko wa moya na hakika kuanzia hapo hali yake haikutengenemaa mpaka kifo kilipomchukua siku ya Jumamosi Nov 30 2013, katika hospital ya St Luc Bsusells Ubelgiji. Matatizo ya kisukari na moyo yalisababisha kifo cha mbuyu huu wa muziki wa rumba. Inasemekana tabu Ley alikuwa na watoto wengi sana, inasemekana walifikia 104. Hata mwenyewe alipokuwa hai akiulizwa ana watoto wangapi hakujua. Watoto wake wachache walifuata nyayo za baba yao, akiwemo Melodie, binti aliyezaa na Mbilia Bel ambae sauti yake imo katika album ya mwisho ya Tabu Ley ‘Tempelo’ aliyoitoa mwaka 2006. Wengine katika muziki ni
Pegguy Tabu, Abel Tabu, Philemon and Youssoupha Mabiki.
Youssoupha ni rapper anaeishi Paris, alizaliwa mwaka 1979 , mama yake alikuwa kutoka Senegal. Mwanae Marc Tabu ni mtangazaji kwenye TV moja huko Paris na ndie aliyetoa taarifa ya kwanza ya kifo cha baba yake kwenye ukurasa wake wa FACEBOO 2013.
Saturday, November 12, 2016
RAJABU OMARY KUNGUBAYA APATA MGUU WA BANDIA KUTOKA KWA WAPENZI WA MUZIKI WA ZAMANI
Marehemu Omary Kungubaya |
Rajabu Kungubaya |
Rajabu Omary Kungubaya, mtoto wa marehemu Omary Kungubaya, mwanamuziki ambaye alipata umaarufu kutokana na wimbo wake wa ‘ Salamu za wagonjwa’ uliokuwa wimbo wa kufungua na kufunga kipindi cha salamu za wagonjwa kilichokuwa kikirushwa na Radio Tanzania, leo amepokea mguu wa bandia ili kumsaidia kutokana na mguu wake wa kulia kuwa umekatwa kutokana na ajali ya bodaboda. Wanamuziki John Kitime na Mjusi Shemboza walimuona Rajabu kwa mara ya kwanza siku walipoenda kumzika Mzee Kungubaya na kuona umuhimu wa kumsaidia Rajabu kutokana na hali yake ya kutegemea magongo wakati wa kutembea. Kwa kutumia kundi a Whatsapp la ZAMA ZILE, (kundi la wapenzi wa muziki wa zamani wanaosikiliza kipindi cha ZAMA ZILE kinachoendeshwa na John Kitime kupitia EFM 93.7fm kila Jumapili kuanzia saa 2-5 usiku), wanakikundi waliweza kuchanga fedha zilizowezesha kijana huyu kupata mguu wa bandia.
Rajabu ni mchangamfu anaeonekana kupendwa na kila mtu, kutokana na majirani zake wote kumuunga mkono ikiwemo serikali ya mtaa wake. Mwenyekiti wa serikali ya mtaa akiwa na wajumbe wengine wa serikali ya mtaa wake wote walimsifu kwa tabia yake ambayo walisema ilikuwa ni mfano hasa kwa jitihada zake za kutunza familia yake. Mke wa marehemu Mzee Kungubaya, ambaye ni mama mzazi wa Rajabu alisema yeye alikuwa anategemea kuishi kwa kufanya kazi za kibarua katika sehemu ambazo kuna ujenzi unaendelea, hufanya kazi kama kubeba maji na zege kuwasaidia wajenzi. Marehemu Kungubaya ameacha watoto wakiwemo wadogo ambao mmoja yuko shule ya chekechekea na mwingine darasa la 6, wote hawa wanamtegemea sasa kaka yao ambae ana mguu mmoja. Rajabu alikatika mguu kutokana na gari kuovertake na kumfuata upande wake na kumgonga wakati akiwa kwenye bodaboda, aliyemgonga, jina na namba ya simu ipo aliahidi kumsaidia lakini hajatimiza ahadi zake kwa kijaa huyu aliyempa ulemavu wa maisha.
Saturday, October 29, 2016
EXCLUSIVE- ANGALIA PAMBAMOTO LILIVYOKUWA LIKICHEZWA MIAKA YA 90 -VIDEO
VIJANA DAY kila Jumapili mchana Vijana Jazz Band walikuwa wakipiga katika ukumbi wa Vijana Social Hall Kinondoni na hii ilikuwa mojawapo ya raha ukumbini. Aina ya uchezaji hakika ni tofauti na leo.
Jukwaani wapiga magitaa
Miraji Shakashia- solo
John Kitime- Rythm
Manitu Musa - Bass
Drums- Juma Choka
Sax Rashid Pembe na Said Mohamed Ndula
Trumpet- Mawazo Hunja na Tuba
Uimbaji
Jerry Nashon, Mohamed Gotagota, na Abdallah Mgonahazelu
Jukwaani wapiga magitaa
Miraji Shakashia- solo
John Kitime- Rythm
Manitu Musa - Bass
Drums- Juma Choka
Sax Rashid Pembe na Said Mohamed Ndula
Trumpet- Mawazo Hunja na Tuba
Uimbaji
Jerry Nashon, Mohamed Gotagota, na Abdallah Mgonahazelu
TOA MAONI
Friday, October 21, 2016
MAZISHI YA MZEE KUNGUBAYA
MWANAMUZIKI mkongwe ambaye alipata umaarufu kutokana na wimbo wake Salam za Wagonjwa amezikwa leo katika makaburi ya kifamilia Njeteni Kwembe. Msiba huo ulihudhuria na watu wengi wakiwemo majirani, ndugu, wanamuziki na wapenzi wa muziki wa Mzee Kungubaya.Tatu itakuwa siku ya Jumamosi 22/10/2016.
Jeneza likiwa nje ya nyumba ya marehemu |
Mwanamuziki Mjusi Shemboza akiongea na mmoja wa watoto wa marehemu Mzee Kungubaya |
Mjusi Shemboza akiwa na Mtendaji Mkuu wa COSOTA wa zamani Mzee Mtetewaunga |
Msafara wa kuelekea makaburini |
Mazishi ya Mzee Kungubaya |
Thursday, October 20, 2016
BURIANI OMARY KUNGUBAYA
Mzee Omari Kungubaya akipiga gitaa siku ya mkesha wa msiba wa Dr. Remmy Ongala |
Friday, October 7, 2016
BURIANI SALOME KIWAYA
Picha iliyopigwa Uingereza wakati Salome alipoenda huko na Shikamoo Jazz Band. Toka Kushoto Marehemu Salome Kiwaya, Marehemu Papa Wemba, na Marehemu Bi Kidude Mungu awalaze pema. |
Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa za msiba wa Mama Salome Kiwaya, mwanamuziki mkongwe. Taarifa zilinifikia kuwa Salome amefariki katika ajali ya gari iliyotokea Dodoma sehemu za Meriwa. Nilimfahamu Salome kwa mara ya kwanza mwaka 1987, wakati nikiwa bendi ya Tancut Almasi Orchestra, tulipopiga kambi Dodoma Hotel kwa muda wa miezi mitatu, tukitoa burudani kwanza kwa wajumbe wa mkutano wa Kizota, kisha wenyeji wa mji wa Dodoma. Katika kufahamiana kipindi hicho, tuliweza hata kupiga wimbo wake mmoja ulioitwa Tuhina, uliokuwa ukiimbwa na Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa, ambao nao ni marehemu. Siku moja nilipita mtaani Dodoma na kununua kanda za muziki wa Salome, nilizipenda sana nyimbo zake na nikamuahidi kuwa ningejitahidi kuzipeleka kwa watu wenye uwezo wa kuendeleza kazi zile. Nilizipeleka kanda kwa Ronnie Graham, Mscotch mmoja mwenye upenzi na uelewa mkubwa wa muziki wa Kiafrika na hasa rumba, na huyu Mscotch ndie aliyewezesha kuanzishwa kwa bendi ya Shikamoo Jazz Band. Baada ya kuzisikia nyimbo zile akaamua kuwa Salome asindikizane na bendi ya Shikamoo kwenye ziara yao ya Uingereza kama muimbaji wa kike. Salome alienda Uingereza na aliporudi ndipo alipoanza kununa vyombo na kuunda kundi la Saki Stars, ikiwa ni kifupi cha Salome Kiwaya Stars. Mume wake Mzee Kiwaya nae ni msanii maarufu aliyekuwa kiongozi wa kikundi cha Utamaduni cha CDA miaka hiyo ya 80. Kuanzia hapo nimekuwa karibu sana na Salome, miaka ya 90 wakati nikiwa Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Salome ndie alikuwa mwenyekiti wa chama hicho katika mkoa wa Dodoma baada ya mkutano mkubwa wa wanamuziki uliofanyika mwezi June 1998, kule Bagamoyo, ambapo wanamuziki 265 waliweza kukusanyika pamoja na kukaa siku nne katika mji wa Bagamoyo wakifanya warsha za fani mbalimbali za muziki. Katika miaka ya karibuni Salome alishughulika na sanaa ya urembo akiwa wakala wa Miss Tanzania kwa kanda ya Kati na kuweza kutoa MIss Tanzania mmoja, baadae aliingia katika siasa na kufikia kuwa Mwenyekiti wa UWT wa Mkoa wa Dodoma, lakini aliendelea na muziki katika maisha yake yote.
Mungu Amlaze Pema Salome Kwaya. Ucheshi wako hatutausahau.
JOHN KITIME
JOHN KITIME
Thursday, September 22, 2016
TANGA MJI ULIKOANZA MUZIKI WA DANSI
Wiki hii nilipata bahati ya kutembelea mji wa Tanga, mji ambao sifa zake zilianza kusikika kuanzia enzi za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo shule ya kwanza ya serikali ilijengwa hapa enzi hizo hizo za utawala wa Wajerumani, jiji ambalo liliendelea kukua sana kutokana na kilimo cha katani na hivyo kukusanya vijana toka kila kona ya nchi kuja kutafuta kazi katika mashamba makubwa ya katani wakati huo. Tanga mji ambao kutokana na uwingi wa vijana wakati huo, shughuli za burudani ya muziki nazo zilifikia kiwango cha juu kuliko sehemu nyingi Tanzania.
Ukizungumzia historia ya muziki wa dansi, huwezi kukwepa kuzungumzia Tanga, kwani historia inatueleza kuwa kabla ya kuanza vikundi vya muziki wa dansi kulianzishwa klabu za kucheza dansi. Klabu hizo zikitumia muziki wa santuri, wanachama wake walicheza na hata kushindana kucheza muziki kwa mitindo mbali mbali ya kigeni ikiwemo waltz, tango, chacha, rumba na kadhalika. Klabu za kwanza nchini zilianzia Tanga. Kulikuwa na klabu kama Young Noverty miaka michache baada ya vita ya kwanza ya dunia, wakati huo nchi ya Tanganyika ikiwa bado changa kabisa. Mtindo huu wa vilabu vya dansi ulienea na baadae kuingia Dar es Salaam na miji mingine iliyokuwa imeshaanza wakati huo. Vilabu hivi ndivyo baadae vikaanzisha vikundi vya kwanza vya muziki wa dansi. Hata majina ya vikundi hivyo vya kwanza yalihusiana na klabu za burudani za wakati huo. Kulikuwa na vikundi kama Coast Social Orchestra, Dar es Salaam Social Orchestra na kadhalika. Hivyo mji wa Tanga ulikuwa katika ndoto za vijana enzi hizo. Kwa vile vijana wengi walikusanyika katika jiji hili nchi, kulianzishwa pia klabu ambazo zilikuwa kwa ajili ya vijana waliokuwa wakitoka kabila moja. Klabu hizo zikiwa na nia ya wananchama wao kusaidiana katika shida na raha, na vilabu hivi pia vilikuwa ni sehemu muhimu katika kutoa burudani kwa vijana waliotoka sehemu moja. Kati ya klabu hizi kulikuweko na klabu iliyoitwa Young Nyamwezi, kama jina lake lilivyo ilikuwa ni klabu ya vijana kutoka Unyamwezini. Hatimae mwaka 1955 klabu hii ilianzisha bendi yake iliyoitwa Young Nyamwezi Band, bendi hii ilikuja kukua na baada ya Uhuru ilibadili jina na kuitwa Jamhuri Jazz Band. Hakika kwa vijana waliokuwa wapenzi wa muziki miaka ya 60 na 70 ilikuwa lazima uifahamu Jamhuri Jazz Band, muziki wake, au kwa lugha ya enzi zile, ‘vibao’ vyake vilijulikana Afrika ya Mashariki nzima. Bendi hii ilikuwa ikibadili mitindo ya upigaji wake na kupiga katika mitindo ya ‘Toyota’ na hatimae ‘Dondola’. Aliyekuja kumiliki bendi hii, ambayo wapenzi wake pia waliita JJB alikuwa Joseph Bagabuje, kulikuwa hata maelezo wakati fulani kuwa JJB ilikuwa kifupi cha Joseph Jazz Band na si Jamhuri Jazz band. Kama ilivyokuwa kawaida ya bendi za wakati ule Jamhuri Jazz Band ilisafiri sana na kufanya maonyesho katika kila kona ya nchi yetu, jambo hilo pamoja na kuwa bendi hii ilirekodi na kutoa santuri kupitia kampuni za kurekodi za Kenya na pia kurekodi nyimbo zake katika radio ya Taifa uliifanya bendi hii kuwa maarufu sana. Upigaji wa aina ya pekee wa gitaa la rhythm wa bendi hii, ambao uligunduliwa na Harrison Siwale, maarufu kwa jina la Sachmo, uliigwa na wapiga magitaa ya rhythm wengi nchini. Uimbaji wa kutumia waimbaji wawili tu, uliopendelewa na bendi za Tanga wakati huo ikiwemo bendi nyingine maarufu wakati huo, Atomic jazz Band, ulikuwa ni wa aina yake pia. Jamhuri Jazz Band pia ndio kilikuwa chanzo cha bendi maarufu ya Simba wa Nyika na bendi zilizozaliwa baada ya hapo. Nilibahatika kukutana mtu aliyekuweko siku ya kwanza ya safari ya kuja kuzaliwa kwa Simba wa Nyika, hakika ni hadithi yake ilikuwa ya kusisimua. Inasemekana kuwa siku hiyo Jamhuri Jazz Band ilikuwa imekodishwa kwa ajili ya kupiga kwenye harusi kule Muheza. Wanamuziki walikuwa wakilazimika kukusanyika katika jengo la klabu lililokuwa Barabara ya 15 ili kupata usafiri wa kwenda Muheza. Siku hiyo wanamuziki wengine walikusanyika lakini George na Wilson Peter, Luza Elian a wengine wachache hawakuonekana, baada ya upelelezi mfupi ikajulikana kuwa wamejificha au wameondoka mjini Tanga, hivyo ikalazimika kutafuta wanamuziki viraka wa haraka haraka kuweza kufanikisha onyesho la siku hiyo, msimuliaji alinambia kuwa japo yeye hakuwa mwanamuziki bali shabiki tu wa bendi aliweza kupanda jukwaani na kuimba katika harusi hiyo, hali haikuwa mbaya kwani alijitokeza mteja mwingine akitaka bendi ikapige kwenye harusi yake pia, lakini ombi lake lilikataliwa kwani wanamuziki walijua kuwa hawakuwa kwenye kiwango chao. Na baada ya hapo kikaanza kipindi kigumu kwa Jamhuri Jazz Band kujitahidi kurudisha hadhi na ubora wa bendi, na pia ikaanza safari iliyokuja kubadili historia ya muziki wa dansi Afrika mashariki kwa vijana hawa waliotoroka kuelekea Arusha ambako walianzisha Arusha Jazz Band na hatimae kuvuka mpaka na kuingia Kenya ambako walianzisha Simba wa Nyika ambayo mafanikio yake yanatingisha hisia za wapenzi wa muziki wa dansi mpaka leo.
Tuesday, September 13, 2016
JAMHURI JAZZ BAND
Kwa mara ya kwanza niliwaona 'Live', Jamhuri Jazz Band wakipiga katika ukumbi wa Community Centre Iringa, ukumbi maarufu kwa wenyeji wakati huo kwa jina la Olofea senta (Welfare Centre). Ni vigumu kuelezea jinsi nilivyokuwa najisikia kwani nilikuwa sidhani kama kutakuja kuweko na wanamuziki wanapiga vizuri namna ile. Lakini katika wote mpiga rythm guitar Harison Siwale, aliyejulikana kwa jina la Satchmo, alikuwa na anabakia kuwa mpiga gitaa aliyenifurahisha kuliko wote. Kwanza alikuwa na staili ya peke yake, na mpaka leo nikisikiliza nyimbo zake kama vile Blandina, Mganga no 1, Maria bembeleza mwana au Ewe ndege, nabaki kusifia kuwa huyu bwana alikuwa na kipaji cha pekee. Kuna rafiki yangu aliwahi kumuuliza wakati ule huwa anapataje mawazo ya kupiga gitaa lake kwa staili ile? alijibu kuwa huwa anajaribu kupiga sauti za viumbe mbalimbali wa porini katika gitaa lake.
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School, Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni. Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School, Manji, Sewando, Danford Mpumilwa, Askofu Kakobe watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo lazima bendi kubwa ikija, wanamuziki wadogo huomba Kijiko, na kama unaweza kuimba au kupiga vizuri unaachiwa nafasi ili muhusika akatafute mpenzi. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni. Bendi hii ilianza kwenye miaka ya 50 ikiwa ikijulikana kama Yanga Nyamwezi Band, Kiukweli ilikuwa ni Young Nyamwezi Band, bendi iliyokuwa imetengenezwa kwa ajili ya Vijana toka Tabora waliokuja kukata mkonge katika mashamba ya mkonge yaliyokuweko Tanga miaka hiyo. Na baada ya Uhuru ikajulikana kama Jamhuri Jazz Band, kifupi JJB japo kifupi hicho baadae kilidaiwa kuwa kilikuwa kifupi cha jina mwenye bendi Joseph Bagabuje. Wakati wa uhai wa Jamhuri Jazz bendi Tanga kulikuwa kuna waka moto kwa vikundi maarufu katika Afrika ya Mashariki kuwa vyote katika mji huo. Atomic Jazz, Amboni Jazz, Lucky Star, Black Star. Kwa vyovyote Tanga ulikuwa mji wa starehe wakati huo, hasa ukikumbuka kuwa kulikuweko na bendi nyingine ambazo hazikuwa maarufu labda kutokana na aina ya muziki zilizokuwa zinapiga. Kama vile ile bendi ya Magoa The Love Bugs ambayo ndiyo hatimae ilikuja kuwa The Revolutions na sasa Kilimanjaro Band
Mbaruku Hamisi,Abdallah Hatibu, Zuheni Mhando |
Eliah John, Alloyce Kagila, Musa Mustafa |
Yusuf Mhando, Joseph Bagabuje, Rajabu Khalfani |
George Peter, Harrison Siwale, Wilson Peter |
Friday, September 9, 2016
HASSAN SHAW MPIGA KINANDA MKONGWE
Shaw Hassan Shaw |
Kwa wapenzi wa Vijana Jazz wanakumbuka vile vipande vya kinanda vilivyokuwa vikianzisha zile nyimbo mbili alizokuwa akiimba Kida Waziri, Penzi Haligawanyiki na Shingo feni, mpigaji wake alikuwa Shaw Hassan Shaw Rwamboh. Mwanamuziki huyu alizaliwa tarehe 25 September 1959, Dar Es Salaam. Alianza kujifunza kupiga gitaa na wenzie kando ya Ziwa Tanganyika huko Kigoma, wakitumia magitaa ya tajiri mmoja aliyekuwa na meli ya uvuvi. Alipokuja Dar es Salaam akakutana na mwanamuziki Zahir Ally Zorro, Zahir ndiye aliyeboresha upigaji wake wa gitaa kiasi cha kukubaliwa na Patrick Balisidya kupiga gitaa la rythm katika bendi yake ya pili PAMA Band, chini ya Afro70.
Hassan Shaw wa kwanza kulia aliyenyoosha mkono. Mwendeshaji wa blog hii John Kitime wa kwanza aliyesimama kushoto. Hapa wakiwa Stadium Morogoro. |
Ni chini ya malezi ya Patrick alipojifunza kupiga Keybords (Kinanda). Baada ya hapo aliacha muziki na kujiunga na Dar Technical College. Lakini 1980 alijiunga na Vijana Jazz kama mpiga Keyboards, alishirikiana na wanamuziki wengi lakini wengi kwa mapenzi ya Mungu, wametangulia mbele ya haki. Baadhi ya waliobaki kati ya aliyokuwa nao wakati huo ni John Kitime, Kida Waziri, Saad Ally Mnara, Hamisi Mirambo, Huluka Uvuruge, Hassan Dalali, Hamza Kalala na Rashid Pembe. Mwaka 1990 alijiunga na Orchestra Safari Sound, chini ya Maalim Muhidin Gurumo (MJOMBA), na Marehemu Abel Baltazar, hapa alikutana na wanamuziki kama Benno Villa Anthony na Mhina Panduka (Toto Tundu) .Aliacha bendi baada ya miezi sita tu, mwenyewe anasema, ‘….kutokana na muhusika kutozingatia mkataba wangu…’. Alihamia Zanzibar na kujiunga na bendi iliyokuwa ikipiga Mawimbini Hotel, hakukaa sana kwani Washirika Tanzania Stars walimwita. Hapa akakutana na mwalimu wake wa gitaa Zahir Ally, Ally Choki, Musemba wa Minyugu,Tofi Mvambe, Abdul Salvador na wengine, ilitokea kutoelewana baina ya wanamuziki na yeye kama kiongozi wa bendi ilibidi aachie ngazi kuepusha bendi kuzidi kujichanganya. Baada ya hapo Kanku Kelly ambaye ni mume wa dada wa mke wake alimuita ajiunge na Kilimanjaro Connection Band. Anasema Kanku alimvumilia sana kwa kuwa alikuwa hajawahi kufanya kazi ya kukopi nyimbo za wanamuziki wengine wakubwa duniani, hatimae akaweza kujiendeleza na kuweza kumudu kupiga vitu vikubwa, bendi hii ya Kanku ilikua inazunguka kwa kupiga muziki hotel mbalimbali katika nchi za Malaysia, Singapore, Indonesia, Thailand na Japan jambo ambalo lilifanya aone kila kitu ni kigeni kila alipokwenda. Katika bendi hiyo alishirikiana na akina Kanku Kelly, Mafumu Bilal, Maneno Uvuruge, Burhan Adinan, Shomari Fabrice, Bob Sija, Fally Mbutu, Raysure boy, Delphin Mununga na Kinguti System. Baadaye Shaw, Kinguti na Burhan Muba waliamua kuanzisha kundi dogo wakitumia sequencer keyboards na kumuaga Kanku Kelly. Group hili lilijiita Jambo Survivors Band, bendi ambayo itakumbukwa kwa ule wimbo Maprosoo ulioimbwa na MlasiFeruzi ambao uliokuwa katika album ya MAPROSOO.
Baada ya hapo bendi ikaanza kuzunguka nchi mbalimbali ikipiga katika mahotelini. Wameshapita Oman , Fujairah, U.A.E, Singapore, Malaysia na sasa wapo Thailand. Shaw anasema wanamuziki ambao hatawasahau kwa kuwa wamemfikisha alipo ni Zahir Ally Zorro, Marehem Patrick Balisdya, Waziri Ally, Kinguti System, Burhan Muba na Kanku Kelly. Kituko ambacho hawezi kusahau ni nchini Malasyia wakati akiwa na Kanku Kelly na ikiwa ni mara ya kwanza kwake kupiga muziki akiwa amezungukwa na watu weupe watupu. Anasema nyimbo zote zilipotea kichwani akawa hakumbuki hata nyimbo moja aliyokuwa kafanyia mazoezi
Mlasi feruzi |
Wednesday, September 7, 2016
WESTERN JAZZ BAND MOJA YA BENDI ILIYOKUWA MAARUFU TANZANIA
Mzee Iddi Nhende ndiye aliyepata wazo la kuanzisha bendi maarufu ya Western Jazz. Iddi Nhende alianza muziki akiwa bado mdogo katika bendi ya shule alipokuwa Primary huko Nzega, mwaka 1944 alijiunga na Tabora Boys Secondary na hapa akajiunga na Brass Band ya shule ambapo alikuwa mpigaji wa Cornet. Alimaliza shule na kuja Dar es Salaam kujiunga na Chuo cha Afya, Sewa Haji Medical Training Center. Baada ya kumaliza mafunzo akaajiriwa Bohari ya madawa na kisha mwaka 1957 alihamishiwa Muhimbili. Upenzi wake wa muziki ulimfanya mwaka huohuo ajiunge na Rufiji Jazz Band kama mpiga trumpet, bendi hii wakati huo ilikuwa ikifanya maonyesho yake Minazini Community Centre iliyokuwa eneo linaloitwa siku hizi Mchikichini na pia walikuwa wakipiga muziki katika ukumbi wa Arnatougro.
Kutokana na miji kuwa ndio ilikuwa inaanza, watu wengi kutoka maeneo mbalimbali walihamia mijini na kujaribu kutafuta wenzao waliotoka sehemu moja na kuwa na vikundi vya kusaidiana au kuwaunganisha, watu wa sehemu mbalimbali walianzisha bendi wakazipa majina ya wanakotoka, hivyo waanzilishi wa Rufiji Jazz walitoka Rufiji, na ndivyo ilivyokuwa kwa Kilwa Jazz, Ulanga jazz na kadhalika. Hivyo Iddi Nhende aliyekuwa ametoka Nzega akaamua kuanzisha bendi ya watu kutoka Magharibi, kwa kuwa nchi ilikuwa imegawanywa katika majimbo, yakiweko majimbo kama Northern Province, Southern Highlands Province, Western Province na kwa vile Nhende alitoka Western province akaanzisha Western Jazz Band 1959. Akanunua vyombo aina ya Grampian toka duka la Souza Junior duka la vyombo vya muziki lililokuwepo mtaa wa Mkwepu. Aliweza kupata fedha baada ya kuuza ng’ombe kadhaa wa mamake. Wakati huo katika bendi za aina yake ni Dar es Salaam Jazz Band peke yake waliokuwa na magitaa ya umeme, hivyo Nhende akawa na kazi ya kuwatafuta wapigaji ambapo alimfuata mpiga gitaa la umeme wa kwanza Haus Dibonde(Msukuma), aliyekuwa anapigia Dar es Salaam Jazz Band(hii ilikuwa chini ya Mzee Muba), baada ya hapo akawapata wanamuziki wengine kutoka Ulanga Jazz Band, wakati huo chombo cha banjo kilikuwa muhimu hivyo akamtafuta mpiga banjo toka Cuban Marimba tawi la Dar es Salaam. Cuban Marimba wakati huo ilikuwa na tawi Dar Es Salaam lililokuwa chini ya Mzee Mwaipungu. Mwaka mmoja baadae alipata transfer ya kwenda Morogoro, hivyo huku nyuma alilazimika kuongeza wasanii ili kuimarisha bendi wakati hayupo. Akampata David Makwaya mwimbaji, na Ally Rashid(huyu ameacha muziki karibuni akiwa Msondo), mpiga Saxaphone toka Zanzibar. Bahati mbaya yule mpiga gitaa Haus akapata kichaa katika mazingira yaliyohusishwa na ushirikina kutokana na ushindani wa bendi uliokuwepo. Hivyo basi walifuatwa wanamuziki watatu toka Tabora Jazz, wanamuziki hao walikuwa wametoka pamoja katika bendi iliyokuwa na makazi Mwanza ikiitwa Kimbo Twist Band na wakahamia Tabora Jazz, na kutoka hapo wakachukuliwa na Western Jazz. Wanamuziki hao walikuwa
Rashid Hanzuruni, Kassim Mponda na Omary Kayanda. Baada ya kazi nzuri sana, Hanzuruni Nae akarukwa na akili katika mazingira yale ya yule mpiga solo wa kwanza akalazimika kurudishwa Tabora ambako alikaa mpaka mauti yake. Wema Abdallah akachukua nafasi ya mpiga solo katika bendi ya Western. Tatizo la kinidhamu lilifanya Wema aondolewe Western, na mpigaji mwingine mzuri sana Shamba Abbdallah akachukua nafasi, solo la huyu bwana linasikika kwenye nyimbo ka Rosa na kadhalika.
Hall la nyumbani la Western Jazz lilikuwa Alexander Hall, ambalo lilikuja kuwa hall la DDC Kariakoo. Western walinunua drums baada ya Kilwa Jazz kununua drums na kuzipitisha kwao kuwaringia. Walinunua toka kwa bendi moja ya Wagoa iliyoitwa De Mello Brothers. Western walirekodi santuri kadhaa chini ya mkataba waliyousaini na lebo ya Phillips ya Kenya. Hatimae Western na mtindo wao wa Saboso walitoweka katika anga za muziki miaka ya mwisho ya sabini. Kati ya nyimbo zao nyingi ni hizi hapa; Rosa, Vigelegele, Jela ya Mapenzi, Helena no 1 na 2.
Friday, August 19, 2016
MAZISHI YA BI SHAKILA , YATAFANYIKA LEO MBAGALA CHARAMBE
Mazishi ya Bi Shakila yatakuwa leo Jumamosi 20 AGOSTI 2016. Mbagala Charambe, saa kumi alasiri Uwanja wa Ninja.
Namna ya kufika msibani nyumbani kwa marehemu kwa kutumia daladala. Unapanda magari ya Mbagala Rangi Tatu, ukifika mwisho unachukua basi la Nzasa na unashuka Mnara wa Voda hapo unauliza kwa Bi Shakila utaonyeshwa
Namna ya kufika msibani nyumbani kwa marehemu kwa kutumia daladala. Unapanda magari ya Mbagala Rangi Tatu, ukifika mwisho unachukua basi la Nzasa na unashuka Mnara wa Voda hapo unauliza kwa Bi Shakila utaonyeshwa
Sunday, August 7, 2016
LEO TUNATIMIZA MIAKA 12 TOKA KIFO CHA PATRICK BALISDYA
Jina Patrick Balisdya halitakuwa geni kabisa kwa wadau wa blog hii,lazima roho zimeanza kuwadunda kama inavyokuwa kwangu kila nikimkumbuka Blai. Patrick Pama Balisidya alizaliwa Mvumi Dodoma tarehe 18 April 1946. Kabila lake alikuwa Mgogo , kabila ambalo lina wanamuziki wengi maarufu kutokana na muziki kuwa sehemu muhimu ya maisha ya kabila hilo. Mama yake alikuwa anapiga kinanda kanisani na hivyo basi kutokana na asili ya kabila lake na pia kutokana na mama yake, hakika huyu angeweza kujisifu kuwa muziki uko katika damu yake. Mdau mmoja alitutaarifu kuwa Balisidya alikuwa kiongozi wa Bendi ya shuleni kwake Dodoma secondary School. Ambapo kutoka hapo alijiunga na Chuo cha Ufundi , na baada ya kumaliza mafunzo alifanya kazi hiyo kwa muda na 1967 akawa tayari anapiga muziki Dar Es Salaam Jazz B. Kufikia mwaka 1970 Patrick alikuwa ameanzisha kikosi chake mwenyewe Afro70, kikiwa na mtindo wake Afrosa. Alikuwa mbunifu katika muziki wake, na kwa muda mrefu alikwepa sana kuingia katika wimbi la kufuata mapigo ya Kikongo kitu ambacho hata wakati huo bendi nyingi zilikifanya, japokuwa kukutana na Franco wakati alipofanya moja ya ziara zake nchini humu kulimfanya abadili mtindo kwa kipindi kifupi na katika nyimbo moja wapo aliiga kabisa solo la Franco alilolipiga kwenye wimbo wake Georgette. Afro70 iliwakilisha wanamuziki wa Tanzania katika maonyesho ya mtu mweusi Lagos, Nigeria. (FESTAC festival 1977). Vyombo alivyotumia katika maonyesho haya vilimsumbua akili mpaka alipofariki, kwani muda mchache kabla ya Festac, wakati huo serikali ikiwa imeshamtaarifu kuwa ndie atakuwa mwakilishi wa Tanzania, vyombo vyake vyote vilihalibika katika ajali ya gari. Serikali ilikuwa imenunua vyombo vipya kwa ajili ya bendi yake ya Wizara ya Utamaduni wakati huo, ambavyo siku zote Balisdya alisema aliambiwa ni vyake baada ya maonyesho. Aliporudi kutoka Nigeria Kiongozi mwingine wa serikali aliamuliwa arudishe hivyo vyombo virudishwe serikalini na kwa kitendo kile kutangaza kifo cha Afro70. Vyombo hivyo vilitumika kuanzisha bendi ya Asilia Jazz ambayo ilikuwa Bendi ya Wizara ya Utamaduni na Vijana. Balisdya alitumia muda mwingi kujaribu kudai haki yake hiyo ambayo ilimkwepa mpaka mwisho wa maisha. Mwaka 1979, Balisidya alikwenda Sweden na kushirikiana na kikundi cha Archimedes akatoa album nzuri sana iliyoitwa Bado Kidogo. Kuna wakati Patrick alijiunga na Orchestre Safari Sound, (masantula) na kupiga piano katika ule wimbo maarufu, ‘Unambie siri’, Patrick pia alikuwa mpigaji mahiri wa keyboards. Kwa kweli nyimbo za Patrick zilizokuwa juu katika chati ni nyingi. Harusi, Dirishani, Weekend, Tausi, Pesa, Nakupenda kama Lulu, Ni mashaka na mahangaiko, Afrika. Patrick alifariki tarehe 7, Agosti 2004 na kuzikwa 12 Aug katika makaburi ya Buguruni Malapa. Daima tutakukumbuka Patrick Pama Balisidya, Mungu akulaze pema peponi
NI MIAKA 46 TOKA KIFO CHA BAVON MARIE MARIE
Bavon Marie Marie, mdogo wake Franco Luambo,alizaliwa May 27, 1944 katika jiji la Kinshasa na kupewa jina la Siango Bavon Marie Marie. Alipokuwa mdogo hakuwa mtukutu lakini alikuwa na akili sana, akajulikana sana kwenye eneo alilokulia wilaya ya Bosobolo. Kadri alivyokuwa akaanza kuishi maisha ya makeke zaidi kwa kuwa mlevi mzuri wa pombe na msafi aliyechichumbua kisawasawa kama ilivyokuwa desturi ya vijana wa Kinshasa wakati ule. Kama alivyokuwa kaka yake Franco Makiadi naye alikuwa mpiga gitaa mzuri sana. Alipigia bendi kama Cubana Jazz akiwa na mwanamuziki Bumba Massa, akapigia Orchestre Jamel kabla ya kuingia Negro Succes, bendi ambayo ilianzishwa 1960 za Vicky Longomba (Baba wa Awilo Longomba). Vicky aliwahi kuwa mmoja wa wanamuziki wa TP OK Jazz, sasa yeye pamoja na wenzie Leon’ Bholen’ Bombolo, na mwimbaji mwenzie Hubert ‘Djeskin’Dihunga, mpiga sax Andre Menga, rhythm Jean Dinos, mpiga bezi Alphonse ‘Le Brun’ Epayo, mpiga drum Sammy Kiadaka na mwimbaji mwingine Gaspard ‘Gaspy; Luwowo wakaanzisha hiyo bendi kali kabisa Negro Succes . Bavon akawa mpiga gitaa wa bendi hii baada ya mwaka 1965, yeye na mwenzie Bholen wakawa viongozi na masupastar wa wakati huo kwa vijana wa Kinshasa. Pamoja na kuwa kaka yake Franco ndie aliyekuwa akijulikana kama Mwalimu Mkuu wa Rhumba la Kongo yeye pia alikuwa kipenzi vijana kutokana na upigaji wa solo lake lililokuwa na uchangamfu zaidi .
Tarehe 5 Agost 1970 Bavon Marie alifariki katika ajali ya gari baada ya ugomvi uliotokana na mpenzi wa Bavon aliyeitwa Lucy, ambapo Bavon alimshutumu kaka yake kuwa kalala na mpenzi wake huyo. Ajali hiyo ilisababisha Lucy akatike miguu. Kuna watu wengine wanasema kisa kilikuwa ni ulevi tu wa Bavon ulisababisha bendi yake ishindwe kufanya show nae akawa kakasirika kwa hilo na kuendesha gari kwa fujo na kuishia chini ya uvungu wa roli kwenye njia panda. Pamoja na upigaji wa gitaa Bavon pia alikuwa mtunzi mzuri sana wa mashahiri ambayo yaliwagusa watu. Kwa mfano wimbo wake wa 'Mwana 15 Ans'…Mtoto wa miaka 15, Bavon aliongea kama binti wa miaka 15 ambae ana uchungu kwa kuwa familia yake inamtafutia mchumba japo yeye anataka kwenda shule. Hadithi ambayo wote tutakubali mpaka leo inamaana sana katika jamii za Kiafrika
Subscribe to:
Posts (Atom)