Sunday, March 30, 2014

UNAWAKUMBUKA BLACK BLOOD...WAONE HAPA KATIKA VIDEO YA WIMBO WAO A.I.E MAMA

Sunday, March 9, 2014

URAFIKI JAZZ BAND 2

Urafiki Jazz Band
Bendi ya Urafiki ikiwa katika hali yake ya uchanga mwaka 1970 ilipata ajali ya gari, wakati kundi zima likitoka katika onyesho huko Chang’ombe, gari lao aina ya Volkswagon Kombi liligonga mti maeneo kona ya Kigogo na Msimbazi Mission.
Baadhi ya wanamuziki waliumia sana na gari lao, likawa halifai kabisa.
Wapigaji walioumia walikuwa ni Hamisi Mashala – Drummer Boy - alivunjika mguu, Mohamed Bakari Churchil aliumia kichwani na kushonwa nyuzi kadhaa, na pia Ayoub Iddi Dhahabu na Maarifa Ramadhani walipata maumivu makali kwa ndani mwilini.

Bendi ilisimamisha maonyesho yake kwa muda hadi  wanamuziki wake walipopata nafuu na kuanza maonyesho tena. Hali ya ajali ile ilileta fikra mbaya kwa wanamuziki hao na wapenzi wao na ilionekana kana kwamba kulikuwa na mkono wa mtu katika ajali ile.  Juma Mrisho ‘Ngulimba’ alitunga wimbo ‘Nimekosa Nini Jama’, wimbo ulioelezea kadhia hiyo. Katika kipindi hiki dhana ya ushirikina ilitawala sana katika bendi mbalimbali. Vifo vya wanamuziki mara nyingi vilihusishwa na upinzani katika bendi. 
Kufikia miaka ya ‘80’ kati bendi ya Urafiki ikawa inasua sua kutokana na uchakavu wa vyombo na Menejimenti iliyokuwepo wakati huo haikuwa tayari kutoa pesa kununulia vyombo vipya. Bendi ya Urafiki ilifikia tamati katika miaka ya ‘80’ kati kati na bendi hiyo ikatoweka katika anga za muziki na kubaki historia.

URAFIKI JAZZ BAND 1



                                                                  
Pichani toka kushoto waliosimama-Hamis Nguru-mwimbaji, Marifa Ramadhani-Tumba, Juma Saidi- Maracas, Abas Lulela-Bass, Abasi Said -Saxophone, Fida Said-Saxophone, Mohamed Bakari (Churchill)-rythm, Juma Mrisho(Ngulimba wa Ngulimba)-Mwimbaji na Kiongozi wa Bendi.Waliokaa Michael Vicent-Solo gitaa, Ezekiel Mazando-Rythm, Juma Ramadhani Lidenge-second solo na Ayub Iddi- Bass
Bendi ya Urafiki (Urafiki Jazz Band), ilianzishwa mwaka 1970 na kiwanda cha nguo cha Urafiki kilichopo Ubungo. Jina rasmi la kiwanda lilikuwa ni FRIENDSHIP TEXTILE MILL. Kiwanda kilijengwa kwa msaada wa watu wa Jamhuri ya China na kwa urafiki huo kilipewa jina la Friendship Textile. Bendi ilianzishwa ili kutangaza bidhaa hasa Khanga na Vitenge za kiwanda hiki kwani wakati huo kulikuwa na viwanda vingine kadhaa vya nguo nchini kama vile Mwatex, Mutex, Kilitex, na kadhalika


Meneja Mkuu wa kiwanda cha Urafiki Bw. Joseph Rwegasira aliubariki mpango huo wa kuanzishwa bendi ya dansi ya kiwanda na hivyo aliidhinisha malipo ya hundi ya Shs. 50,000/= kununulia seti ya vyombo vya muziki kutoka katika duka la Dar Es Salaam Music House ambalo mpaka leo lipo katika mtaa wa Samora Avenue – Dar Es Salaam.

Ili kupata kundi lililo bora, Menejimenti ya kiwanda cha Nguo cha Urafiki ilimuajiri Juma Mrisho Feruzi maarufu kwa jina la Ngulimba wa Ngulimba na kumuagiza atafute wapigaji kutoka popote ili kuunda kundi imara.. Katika kuhakikisha bendi hiyo mpya inasimama, Ngulimba alichukua wapigaji watano kutoka Orchestre African Qwillado, bendi ambayo aliipigia kabla ya kuanza Urafiki. Na hii ndio maana nyimbo za mwanzoni za Urafiki Jazz Band zilionekana kama zina mahadhi ya Orch. Qwillado.

Wanamuziki aliowachukua Ngulimba kutoka Orch. Qwillado walikuwa ni Michael Vincent Semgumi, mpiga gitaa la Solo, Ayoub Iddi Dhahabu – Besi, Abassi Saidi Nyanga – Tenor Saxophone na Fida Saidi, Alto Saxophone. Ngulimba yeye akawa Muimbaji na pia Kiongozi wa Bendi.

Wanamuziki wengine wa mwanzo ambao waliungana na hao watano waliotoka Orch. Qwillado ambao tayari walikwisha ajiriwa kiwandani Urafiki, walikuwa – Juma Ramadhani Lidenge – Second Solo, Mohamed Bakari Churchil – gitaa la kati (rhythm), Ezekiel Mazanda – rhythm, Abassi Lulela – Besi, Hamisi Nguru – Muimbaji, Mussa Kitumbo – Muimbaji, Cleaver Ulanda – Muimbaji, Maarifa Ramadhani – Tumba, Juma Saidi – Manyanga (maraccass) na Hamisi Mashala – mpiga drums.

Mtindo walioanza nao Urafiki ulijulikana ‘Mchaka Mchaka’ na baadae ukabadilika na kuwa ‘Chaka Chua’ na hatimae mwisho mwisho bendi inaelekea ukingoni walipiga mtindo wa ‘Pasua’ na ‘Patashika’

Mwaka 1971 Gidion Banda, mwanamuziki kutoka bendi ya Morogoro Jazz alijiunga na kundi akiwa mpigaji wa Saxophone.

Aidha, Bendi ya Urafiki ilipitiwa na wanamuziki wengi baadhi wakiwemo Gideon Banda mpuliza saxophone kutoka Morogoro Jazz wengine wakiwemo Thobias Cosmas Chidumule na Frank Mahulu – Waimbaji waliotokea Western Jazz (Saboso) mwaka 1973 na kuongeza nguvu katika safu ya uimbaji. Waimbaji hao walishiriki nyimbo nyingi baadhi zikiwa Tausi Karuka, Jembe na Panga (Geza Ulole), Kosa la Nani, Mauaji ya Soweto, Rukia Hukusikia, Maonyesho ya Mtu Mweusi n.k.

Pia waliongezeka Mkali na Hidaya kutoka Morogoro wakipuliza matarumbeta, hao walikuja 1973 na Ali Saidi alietokea Cuban Marimba akipiga gitaa la kati (rhythm) na baadae mwaka 1975, Mganga Hemedi kutoka Tanga, akitokea Atomic Jazz, nae alijiunga na kuwa upande wa solo na rhythm.

Urafiki Jazz imetunga nyimbo nyingi, zaidi ya mia tatu zinazoelekeza kwenye siasa, mapenzi, nasaha na mafundisho na pia kukosoa. Baadhi ya nyimbo zake za siasa zilizopata umaarufu ni kama zile Mwenyekiti Nyerere, Mauaji ya Soweto, Jembe na Panga n.k..

Mwaka 1975 Bendi ilishiriki katika mashindano ya bendi za muziki wa dansi yaliyofanyika Mnazi Mmoja – D’Salaam na kushika nafasi ya tatu na Mzee Ngulimba, kama Kiongozi wa Urafiki aliiwakilisha Tanzania pamoja na bendi ya Afro 70 iliyopata nafasi ya kwanza na baadhi ya vikundi vya utamaduni kutoka Tanzania Bara na Zanzibar nchini Nigeria katika maonyesho ya mtu mweusi yaliyofanyika huko.

Saturday, March 1, 2014

ASIA DARWESH DADA MPIGA KINANDA AMBAYE KAACHA REKODI YA PEKEE TOKA ALIPOFARIKI 1995


Asia Darwesh kwenye kinanda pembeni yake ni Johnny Rocks kwenye drums. Haba wakiwa Bandari Grill- New Africa Hotel-enzi za Ngoma za magorofani
MAKALA HII IMEANDIKWA NA MWANDISHI  FRED MOSHA
Jina Asia Daruwesh, sio jina geni kwa mashabiki wa muziki Tanzania na pengine Afrika mashariki kwa ujumla. Huyu Dada anaweza kutajwa kama mpiga kinanda wa kwanza kabisa mwanamke kuwahi kutokea kwenye rhumba letu la kitanzania ingawa siku za nyuma kuliwahi kuwa na bendi ya akinamama watupu ikiitwa Women Jazz ambayo kuanzia magitaa, masaxphones na kuimba walikuwa akinamama watupu. Asia Daruwesh alizaliwa mwaka 1964. Ingawa alikuwa na asili ya Zanzibar, maisha yake kwa kiasi kikubwa yalikuwa Zambia kuanzia utotoni hadi anakua na huko ndiko alikopata inspiration ya kuwa mwanamuziki. Kwa hapa kwetu Tanzania, jina la Asia Daruwesh lilisikika kwenye safu ya mwanzo kabisa ya King Kikii mwaka 1984 akiwa na Kikii mwenyewe, Mumba Kisi, Kapelembe Coco, Samba Wa Mikalay, Zahoro Bangwe, Mohamed Idd Control, Matei Joseph na wengine. Alishiriki kupiga kinanda kwenye nyimbo kadhaa za bendi hii iliyokuwa ikitumia mtindo wa Embalasasa Shika Break kama Kinyume, Dodoma Capital, Njimina, Mimi na we, Kibwanange, Malalamiko na nyingine kadhaa huku nyimbo kama Lamanda na Kitoto chaanza tambaa akimuachia Ally Hemed Star huyuhuyu ambaye leo anajulikana kama muimbaji na mtunzi mzuri wa Taarab. Hata hivyo mwaka 1986 mwishoni aliihama bendi hiyo na kujiunga kwenye safu ya mwanzoni ya MK Group wakati huo. Nyimbo karibu zote za kuanzia toleo la kwanza hadi la tatu la MK Group amepiga kinanda yeye. Hassan Rehani sijui anakumbuka nini ukimtajia MK Group!! Mwaka 1989 alikuwa miongoni mwa wanamuziki wanne walioihama MK Group na kwenda kuasisi Bicco Stars. Angekuwemo na Joseph Mulenga katika group hii lakini alirudi nyuma. Akiwa Bicco aliungana na akina Kinguti System, Fresh Jumbe, Athuman Cholilo Mashida, Seif Rengwe, Sid Morris, Mafumu Bilal, Andy Swebe Ambassadeur na wengine Katika bendi hii ndiko alikotunga wimbo wake wa kwanza wa Bwana Kingo na pia akashiriki kuimba na ameimbisha wimbo huo. Mwaka 1992 alianzisha bendi yake mwenyewe akiita Zanzibar Sound ikitumia mtindo wa Wesaka Dance akiwa na akina Bob Gad William, Hezron Ludala ama Bob Ludala, Fariala Mbutu, na baadaye akina Mohamed Idd Control na Shaban Lendi. Wimbo Banana ambao baadaye Bob Gad alikuja kuurudia akiwa na Twanga Pepeta ulirekodiwa kwa mara ya kwanza na bendi hii. Aidha wimbo Hadija ambao Fariala alikuja kuurudia na Kilimanjaro Connections ulirekodiwa nao huku Ludala akiwa muimbaji Kiongozi. Kufariki dunia kwa Asia Daruwesh ama kwa jina la utani Super Mama mwaka 1995 ndiko kulikohitimisha safari ya bendi hii. Ni hayo tu

Thursday, February 27, 2014

HISTORIA YA MANENO UVURUGE

Mawazo Hunja kwenye trumpet, Maneno Uvuruge kwenye gitaa
Maneno Uvuruge ni moja ya wanamuziki waliotoka katika familia ya wanamuziki ya ukoo wa Uvuruge. Kaka zake Jumanne, Stamili, na Huluka ni kati ya wapiga magitaa walioheshimika sana katika jamii ya wanamuziki wa bendi Tanzania.
Jumanne Uvuruge ambae alikuwa mkubwa wa akina Uvuruge wote, ndie aliyetunga kibao maarufu cha Georgina, kilichopigwa na Safari Trippers na kuimbwa na Marijani Rajabu. Siku zake za mwisho za maisha Jumanne alikuwa anajishughulisha na kupata riziki yake kwa kuzunguka katika mabaa mbalimbali na gitaa na kupiga maombi mbalimbali ya wanywaji, na kisha kuhama na kuelekea baa nyingine. Hayakuwa maisha rahisi.
Maneno Uvuruge hana kumbukumbu ya jinsi gani Jumanne alijifunza gitaa, lakini anajuwa kuwa Stamili alifundishwa na Jumanne. Anakumbuka zaidi jinsi Huluka alivyojifunza kwani ndie alikuwa kaka yake waliefuatana kuzaliwa. Huluka alijifunza gitaa kwa kuanza kuchonga gitaa lake mwenyewe, aliiba mishipi ya kuvulia ya baba yake na ndio zikawa nyuzi za gitaa lake, siku babake alipogundua wizi huo alivunja vunja gitaa na kumkataza asiguse mishipi yake tena, lakini akamwelekeza inakonunuliwa, Huluka alitafuta pesa na kwenda kununua mishipi na kuendelea na gitaa lake la kopo. Wakati huo Huluka alikuwa anasoma, naye Maneno akaanza hamu ya kutaka kujua kupiga gitaa akawa anaiba gitaa la kaka yake kila alipoenda shule, ilikuwa ni ugomvi kila alipokata nyuzi kwani alikuwa bado anajifunza. Jumanne na Stamili wakaanza rasmi kumfundisha gitaa Huluka nae akalijua vizuri sana. Si muda mrefu baadae nae akaanza rasmi kumfundisha mdogo wake. Maneno anasema wimbo wa kwanza kakake kumfundisha ni ile rhythm ya wimbo Novelle Geneation wa Orchestra Lipualipua, wimbo huu ulikuwa ni kipimo muhimu kwa wapiga rythm enzi hizo. Freddy Benjamin ndie aliyemshauri kujiunga na Bendi. Alimkaribisha UDA Jazz ambako alikuwa akiimbia na pamoja na kuweza kupiga gitaa alifanyiwa mizengwe na mpiga rhythm aliyekuweko na ambae pia alikuwa katibu wa bendi. Freddy alimuombea kazi Super Rainbow iliyokuwa na makao yake makuu pale Sunlight Bar Mwananyamala B. Na hapo akakutana na wanamuziki kama Hatibu Iteytey, Nuzi Ndoli, Rocky, Mzee Bebe, Akina Eddy Sheggy walikuwa bado hawajajiunga na bendi hii wakati huo.
 
Keppy Kiombile Bass, Maneno Uvuruge Rythm, Makuka Second solo, Juma Choka Drums, Lubaba Solo enzi ya Maquis

Katika kipindi ambapo Maneno Uvuruge alikuwa akipigia Super Rainbow ndipo Eddy Sheggy na Emma Mkello walipojiunga, hawa hukumbukwa sana kwenye bendi hii kwa ajili ya ule wimbo Milima Ya Kwetu, pia nae Banza Tax akajiunga kipindi hiki. Na kule Mabibo bendi ya Mambo Bado ilipata msukosuko na kuvunjika kwa mara ya kwanza na hivyo wanamuziki wake Juma Choka mpiga drums, Lodji Mselewa na Nana Njige pia wakajiunga na kundi na Super Rainbow, lakini hawakukaa sana Assossa aliweza kuifufua tena Mambo Bado na wote wakarudi wakifuatana na Maneno Uvuruge. Lakini tayari bendi ilikuwa iko katika hali mbaya kwani Assossa aliacha tena akiwa katika harakati ya kuunda bendi mpya na Mambo Bado ikafa rasmi. Juma Choka akamtaarifu Maneno kuwa Urafiki Jazz kuna nafasi ya kazi na hapo akenda na kusailiwa na Ngulimba wa Ngulimba, Marehemu Mzee Juma Mrisho, Urafiki nayo ilikuwa katika siku zake za mwisho lakini bado yule mpiga solo mahiri Michael Vicent alikuweko. Kipindi hiki pia waliingia Mohamed Gota gota na Hussein Jumbe. Maneno Uvuruge sasa alianza kufahamika kwa wanamuziki wengine kuwa ana uwezo mkubwa na bendi zikaanza kumsaka, na kuanzia hapo amekuwa hatafuti kazi bali anatafutwa. Bendi ya kwanza kumchukua ilikuwa ni Maquis, alichukuliwa ili awe mpiga gitaa la rhythm, aliwakuta wapiga rhythm wawili, huko, Mbwana Cox na Makuka. Akawa mwanamuziki wa Maquis wakati huo wapiga solo wa bendi hiyo walikuwa ni Nguza Viking, na Mzee Lubaba.
Mwanamuziki Belly Kankonde akakutana na Marehemu Mzee Mwendapole na kuamua kuipa uhai bendi ya Afrisongoma. Kankonde akawashawishi wanamuziki wenzie wanne wa Maquis, Maneno Uvuruge (guitar),Kiniki Kieto(mwimbaji), Comson Mkomwa(saxophone) na Keppy Kiombile(bass) wakahamia Afrisongoma. Maneno hakukaa muda mrefu kwani Nguza alimfuata yeye na Comson na kuwarudisha Maquis , na kwa kuwa walikuwa wamekwishapokea fedha za Mzee Mwendapole kesi ilifika polisi na ikalazimu Maquis warudishe fedha hiyo. Lovy Longomba alijiunga na Maquis nae hakukaa muda mrefu Mwendapole akamshawishi akaunde upya kundi la Afrisongoma ambalo katika awamu ya kwanza liliishia kurekodi mara moja na kutokuwa na maendeleo. Lovy pia tena akamuondoa Maneno na kuhamia nae Afrisongoma.
Wakati huo Mosesengo Fan Fan yule mpiga gitaa mahiri aliyetoka kwa Franco na kupigia Matimila na Makassy alikuwa amehamia Uingereza na akawa amemtaka Kiniki Kieto awashawishi Maneno Uvuruge, Keppy Kiombile, na Vivi Kapaya wamfuate,lakini mpango huo uliishia kwa Kiniki na Vivi kuendelea na Fanfan wakati Maneno na Keppy wakahamia Afrisongoma wakiwa na Lovy. Wanamuziki kadhaa walihamia Afriso wakati huo wakiwemo Kalamazoo, na Mzee Mponda ambae baada ya kutoka Msondo alikuwa kapita Sikinde na akatua Afrisongoma. Na hapo ndipo msondo wakamchukua Maneno kwa mara ya kwanza. Alikaa kwa muda na rafiki zake akina Benno Vila Anthony wakaweza kumshawishi ahamie Sikinde. Baada ya muda si mrefu Nguza akamfuata ili kumshawishi ajiunge na Orchestra Sambulumaa. Ilikuwa ni ushawishi wa Skassy Kasambula na Emmanuel Mpangala aliyekuwa mkurugenzi wa bendi ndio ulioweza kumfanya Maneno ahamie Sambulumaa

ORCHESTRE SANTA FE ILIKUWA BENDI YA KWANZA YA WAKONGO WATUPU NCHINI?

Kati ya maswali amabayo yamewahi kuulizwa humu ni kuhusu bendi hii Orchestra Santa Fe. Hii ilikuwa mwanzo ni bendi yenye asilimia kubwa ya wanamuziki Wakongo. Kuna wakati Blogger Kiongozi Issa michuzi aliwahi kuuliza kama Je,Sante Fe ndio ilikuwa Bendi ya kwanza ya Kikongo? Sina jibu bado kuhusu hili. Wenye taarifa zaidi kuhusu Bendi hii karibuni. Bendi hii ilikuwa ikipiga pale Gateways Mnazi Mmoja maeneo ambayo kuna wakati yalikuwa maeneo muhimu katika shughuli za starehe jijini Dar es Salaam.Kuna maoni yaliwahi kutoleaa kuhusu mada hii katika blog iliyokuwa kabla ya kuzaliwa hii na haya ndio yalikuwa maelezo yao:

      1. BLACKMANNEN said...
Orchestra Santa Fe, haikuwa ya Wakongo. Bendi za Fouvette na akina "Papa Mikey" ndiyo waliokuwa Wakongo wa mwanzo Tanzania.

Orchestra Santa Fe, Tanzania Jazz Band, King Africa Jazz Band na Orchestra Quilado zote zilikuwa za Kitanzania, ila habari zake wengi hatuzijui.

It's Great To Be Black=Blackmannen
2. 
Anonymous said...
TP SANTA FE ILIKUWA NI BENDI YA WAKONGO ILINGIA NCHINI IKITOKEA ZAMBIA NA BAADHI YA WANAMUZIKI WA ZAMBIA MMOJA WAPO NI MPIGA BASS JOSEPH MULENGA,WAKATI TP SANTA FE INAPIGA GOROFA YA TANO GATE WAYS SAFARI TRIPPES ILIKUA ATUA CHACHE PRINCESS BAR KUNA SIKU MPIGA BASS WA TRIPPERS MAREHEMU CHRISTIAN KAZINDUKI ALIPATA AJALI YA PIKIKI PALE KONA YA CENTRAL POLICE KUKAWA HAKUNA MPIGA BASS ILIBIDI MASHABIKI TUTOKE KWENDA KUMUZIMA MULENGA ILI DANSI LETU LIPIGWE NANDIO UKAWA MWANZO WA NYOTA YAKE KUNG'AA ALIJIUNGA NA TRIPPERS NA NYIMBO YAKE YA KWANZA KUREKODI MATESO DHIKI NA MATESO AKIPIGA RIDHIM GITAA ,ABDALA GAMA SOLO,BENNY PETTY SECOND SOLO,KAZINDUKI BASS,KABLA YA KUHAMIA DAR INTERNATIONAL NA KUKUTANA NA MZAMBIA MWENZI MKUBWA WAKE MICHAEL ENOCK ALIE MTRAIN KUWA MPIGA SOLO SIKILIZA NYERERE BABA MLEZI NYERERE MWANA MAPINDUZI THEN AKAENDA SIKINDE.