Saturday, March 1, 2014

ASIA DARWESH DADA MPIGA KINANDA AMBAYE KAACHA REKODI YA PEKEE TOKA ALIPOFARIKI 1995


Asia Darwesh kwenye kinanda pembeni yake ni Johnny Rocks kwenye drums. Haba wakiwa Bandari Grill- New Africa Hotel-enzi za Ngoma za magorofani
MAKALA HII IMEANDIKWA NA MWANDISHI  FRED MOSHA
Jina Asia Daruwesh, sio jina geni kwa mashabiki wa muziki Tanzania na pengine Afrika mashariki kwa ujumla. Huyu Dada anaweza kutajwa kama mpiga kinanda wa kwanza kabisa mwanamke kuwahi kutokea kwenye rhumba letu la kitanzania ingawa siku za nyuma kuliwahi kuwa na bendi ya akinamama watupu ikiitwa Women Jazz ambayo kuanzia magitaa, masaxphones na kuimba walikuwa akinamama watupu. Asia Daruwesh alizaliwa mwaka 1964. Ingawa alikuwa na asili ya Zanzibar, maisha yake kwa kiasi kikubwa yalikuwa Zambia kuanzia utotoni hadi anakua na huko ndiko alikopata inspiration ya kuwa mwanamuziki. Kwa hapa kwetu Tanzania, jina la Asia Daruwesh lilisikika kwenye safu ya mwanzo kabisa ya King Kikii mwaka 1984 akiwa na Kikii mwenyewe, Mumba Kisi, Kapelembe Coco, Samba Wa Mikalay, Zahoro Bangwe, Mohamed Idd Control, Matei Joseph na wengine. Alishiriki kupiga kinanda kwenye nyimbo kadhaa za bendi hii iliyokuwa ikitumia mtindo wa Embalasasa Shika Break kama Kinyume, Dodoma Capital, Njimina, Mimi na we, Kibwanange, Malalamiko na nyingine kadhaa huku nyimbo kama Lamanda na Kitoto chaanza tambaa akimuachia Ally Hemed Star huyuhuyu ambaye leo anajulikana kama muimbaji na mtunzi mzuri wa Taarab. Hata hivyo mwaka 1986 mwishoni aliihama bendi hiyo na kujiunga kwenye safu ya mwanzoni ya MK Group wakati huo. Nyimbo karibu zote za kuanzia toleo la kwanza hadi la tatu la MK Group amepiga kinanda yeye. Hassan Rehani sijui anakumbuka nini ukimtajia MK Group!! Mwaka 1989 alikuwa miongoni mwa wanamuziki wanne walioihama MK Group na kwenda kuasisi Bicco Stars. Angekuwemo na Joseph Mulenga katika group hii lakini alirudi nyuma. Akiwa Bicco aliungana na akina Kinguti System, Fresh Jumbe, Athuman Cholilo Mashida, Seif Rengwe, Sid Morris, Mafumu Bilal, Andy Swebe Ambassadeur na wengine Katika bendi hii ndiko alikotunga wimbo wake wa kwanza wa Bwana Kingo na pia akashiriki kuimba na ameimbisha wimbo huo. Mwaka 1992 alianzisha bendi yake mwenyewe akiita Zanzibar Sound ikitumia mtindo wa Wesaka Dance akiwa na akina Bob Gad William, Hezron Ludala ama Bob Ludala, Fariala Mbutu, na baadaye akina Mohamed Idd Control na Shaban Lendi. Wimbo Banana ambao baadaye Bob Gad alikuja kuurudia akiwa na Twanga Pepeta ulirekodiwa kwa mara ya kwanza na bendi hii. Aidha wimbo Hadija ambao Fariala alikuja kuurudia na Kilimanjaro Connections ulirekodiwa nao huku Ludala akiwa muimbaji Kiongozi. Kufariki dunia kwa Asia Daruwesh ama kwa jina la utani Super Mama mwaka 1995 ndiko kulikohitimisha safari ya bendi hii. Ni hayo tu

Thursday, February 27, 2014

HISTORIA YA MANENO UVURUGE

Mawazo Hunja kwenye trumpet, Maneno Uvuruge kwenye gitaa
Maneno Uvuruge ni moja ya wanamuziki waliotoka katika familia ya wanamuziki ya ukoo wa Uvuruge. Kaka zake Jumanne, Stamili, na Huluka ni kati ya wapiga magitaa walioheshimika sana katika jamii ya wanamuziki wa bendi Tanzania.
Jumanne Uvuruge ambae alikuwa mkubwa wa akina Uvuruge wote, ndie aliyetunga kibao maarufu cha Georgina, kilichopigwa na Safari Trippers na kuimbwa na Marijani Rajabu. Siku zake za mwisho za maisha Jumanne alikuwa anajishughulisha na kupata riziki yake kwa kuzunguka katika mabaa mbalimbali na gitaa na kupiga maombi mbalimbali ya wanywaji, na kisha kuhama na kuelekea baa nyingine. Hayakuwa maisha rahisi.
Maneno Uvuruge hana kumbukumbu ya jinsi gani Jumanne alijifunza gitaa, lakini anajuwa kuwa Stamili alifundishwa na Jumanne. Anakumbuka zaidi jinsi Huluka alivyojifunza kwani ndie alikuwa kaka yake waliefuatana kuzaliwa. Huluka alijifunza gitaa kwa kuanza kuchonga gitaa lake mwenyewe, aliiba mishipi ya kuvulia ya baba yake na ndio zikawa nyuzi za gitaa lake, siku babake alipogundua wizi huo alivunja vunja gitaa na kumkataza asiguse mishipi yake tena, lakini akamwelekeza inakonunuliwa, Huluka alitafuta pesa na kwenda kununua mishipi na kuendelea na gitaa lake la kopo. Wakati huo Huluka alikuwa anasoma, naye Maneno akaanza hamu ya kutaka kujua kupiga gitaa akawa anaiba gitaa la kaka yake kila alipoenda shule, ilikuwa ni ugomvi kila alipokata nyuzi kwani alikuwa bado anajifunza. Jumanne na Stamili wakaanza rasmi kumfundisha gitaa Huluka nae akalijua vizuri sana. Si muda mrefu baadae nae akaanza rasmi kumfundisha mdogo wake. Maneno anasema wimbo wa kwanza kakake kumfundisha ni ile rhythm ya wimbo Novelle Geneation wa Orchestra Lipualipua, wimbo huu ulikuwa ni kipimo muhimu kwa wapiga rythm enzi hizo. Freddy Benjamin ndie aliyemshauri kujiunga na Bendi. Alimkaribisha UDA Jazz ambako alikuwa akiimbia na pamoja na kuweza kupiga gitaa alifanyiwa mizengwe na mpiga rhythm aliyekuweko na ambae pia alikuwa katibu wa bendi. Freddy alimuombea kazi Super Rainbow iliyokuwa na makao yake makuu pale Sunlight Bar Mwananyamala B. Na hapo akakutana na wanamuziki kama Hatibu Iteytey, Nuzi Ndoli, Rocky, Mzee Bebe, Akina Eddy Sheggy walikuwa bado hawajajiunga na bendi hii wakati huo.
 
Keppy Kiombile Bass, Maneno Uvuruge Rythm, Makuka Second solo, Juma Choka Drums, Lubaba Solo enzi ya Maquis

Katika kipindi ambapo Maneno Uvuruge alikuwa akipigia Super Rainbow ndipo Eddy Sheggy na Emma Mkello walipojiunga, hawa hukumbukwa sana kwenye bendi hii kwa ajili ya ule wimbo Milima Ya Kwetu, pia nae Banza Tax akajiunga kipindi hiki. Na kule Mabibo bendi ya Mambo Bado ilipata msukosuko na kuvunjika kwa mara ya kwanza na hivyo wanamuziki wake Juma Choka mpiga drums, Lodji Mselewa na Nana Njige pia wakajiunga na kundi na Super Rainbow, lakini hawakukaa sana Assossa aliweza kuifufua tena Mambo Bado na wote wakarudi wakifuatana na Maneno Uvuruge. Lakini tayari bendi ilikuwa iko katika hali mbaya kwani Assossa aliacha tena akiwa katika harakati ya kuunda bendi mpya na Mambo Bado ikafa rasmi. Juma Choka akamtaarifu Maneno kuwa Urafiki Jazz kuna nafasi ya kazi na hapo akenda na kusailiwa na Ngulimba wa Ngulimba, Marehemu Mzee Juma Mrisho, Urafiki nayo ilikuwa katika siku zake za mwisho lakini bado yule mpiga solo mahiri Michael Vicent alikuweko. Kipindi hiki pia waliingia Mohamed Gota gota na Hussein Jumbe. Maneno Uvuruge sasa alianza kufahamika kwa wanamuziki wengine kuwa ana uwezo mkubwa na bendi zikaanza kumsaka, na kuanzia hapo amekuwa hatafuti kazi bali anatafutwa. Bendi ya kwanza kumchukua ilikuwa ni Maquis, alichukuliwa ili awe mpiga gitaa la rhythm, aliwakuta wapiga rhythm wawili, huko, Mbwana Cox na Makuka. Akawa mwanamuziki wa Maquis wakati huo wapiga solo wa bendi hiyo walikuwa ni Nguza Viking, na Mzee Lubaba.
Mwanamuziki Belly Kankonde akakutana na Marehemu Mzee Mwendapole na kuamua kuipa uhai bendi ya Afrisongoma. Kankonde akawashawishi wanamuziki wenzie wanne wa Maquis, Maneno Uvuruge (guitar),Kiniki Kieto(mwimbaji), Comson Mkomwa(saxophone) na Keppy Kiombile(bass) wakahamia Afrisongoma. Maneno hakukaa muda mrefu kwani Nguza alimfuata yeye na Comson na kuwarudisha Maquis , na kwa kuwa walikuwa wamekwishapokea fedha za Mzee Mwendapole kesi ilifika polisi na ikalazimu Maquis warudishe fedha hiyo. Lovy Longomba alijiunga na Maquis nae hakukaa muda mrefu Mwendapole akamshawishi akaunde upya kundi la Afrisongoma ambalo katika awamu ya kwanza liliishia kurekodi mara moja na kutokuwa na maendeleo. Lovy pia tena akamuondoa Maneno na kuhamia nae Afrisongoma.
Wakati huo Mosesengo Fan Fan yule mpiga gitaa mahiri aliyetoka kwa Franco na kupigia Matimila na Makassy alikuwa amehamia Uingereza na akawa amemtaka Kiniki Kieto awashawishi Maneno Uvuruge, Keppy Kiombile, na Vivi Kapaya wamfuate,lakini mpango huo uliishia kwa Kiniki na Vivi kuendelea na Fanfan wakati Maneno na Keppy wakahamia Afrisongoma wakiwa na Lovy. Wanamuziki kadhaa walihamia Afriso wakati huo wakiwemo Kalamazoo, na Mzee Mponda ambae baada ya kutoka Msondo alikuwa kapita Sikinde na akatua Afrisongoma. Na hapo ndipo msondo wakamchukua Maneno kwa mara ya kwanza. Alikaa kwa muda na rafiki zake akina Benno Vila Anthony wakaweza kumshawishi ahamie Sikinde. Baada ya muda si mrefu Nguza akamfuata ili kumshawishi ajiunge na Orchestra Sambulumaa. Ilikuwa ni ushawishi wa Skassy Kasambula na Emmanuel Mpangala aliyekuwa mkurugenzi wa bendi ndio ulioweza kumfanya Maneno ahamie Sambulumaa

ORCHESTRE SANTA FE ILIKUWA BENDI YA KWANZA YA WAKONGO WATUPU NCHINI?

Kati ya maswali amabayo yamewahi kuulizwa humu ni kuhusu bendi hii Orchestra Santa Fe. Hii ilikuwa mwanzo ni bendi yenye asilimia kubwa ya wanamuziki Wakongo. Kuna wakati Blogger Kiongozi Issa michuzi aliwahi kuuliza kama Je,Sante Fe ndio ilikuwa Bendi ya kwanza ya Kikongo? Sina jibu bado kuhusu hili. Wenye taarifa zaidi kuhusu Bendi hii karibuni. Bendi hii ilikuwa ikipiga pale Gateways Mnazi Mmoja maeneo ambayo kuna wakati yalikuwa maeneo muhimu katika shughuli za starehe jijini Dar es Salaam.Kuna maoni yaliwahi kutoleaa kuhusu mada hii katika blog iliyokuwa kabla ya kuzaliwa hii na haya ndio yalikuwa maelezo yao:

      1. BLACKMANNEN said...
Orchestra Santa Fe, haikuwa ya Wakongo. Bendi za Fouvette na akina "Papa Mikey" ndiyo waliokuwa Wakongo wa mwanzo Tanzania.

Orchestra Santa Fe, Tanzania Jazz Band, King Africa Jazz Band na Orchestra Quilado zote zilikuwa za Kitanzania, ila habari zake wengi hatuzijui.

It's Great To Be Black=Blackmannen
2. 
Anonymous said...
TP SANTA FE ILIKUWA NI BENDI YA WAKONGO ILINGIA NCHINI IKITOKEA ZAMBIA NA BAADHI YA WANAMUZIKI WA ZAMBIA MMOJA WAPO NI MPIGA BASS JOSEPH MULENGA,WAKATI TP SANTA FE INAPIGA GOROFA YA TANO GATE WAYS SAFARI TRIPPES ILIKUA ATUA CHACHE PRINCESS BAR KUNA SIKU MPIGA BASS WA TRIPPERS MAREHEMU CHRISTIAN KAZINDUKI ALIPATA AJALI YA PIKIKI PALE KONA YA CENTRAL POLICE KUKAWA HAKUNA MPIGA BASS ILIBIDI MASHABIKI TUTOKE KWENDA KUMUZIMA MULENGA ILI DANSI LETU LIPIGWE NANDIO UKAWA MWANZO WA NYOTA YAKE KUNG'AA ALIJIUNGA NA TRIPPERS NA NYIMBO YAKE YA KWANZA KUREKODI MATESO DHIKI NA MATESO AKIPIGA RIDHIM GITAA ,ABDALA GAMA SOLO,BENNY PETTY SECOND SOLO,KAZINDUKI BASS,KABLA YA KUHAMIA DAR INTERNATIONAL NA KUKUTANA NA MZAMBIA MWENZI MKUBWA WAKE MICHAEL ENOCK ALIE MTRAIN KUWA MPIGA SOLO SIKILIZA NYERERE BABA MLEZI NYERERE MWANA MAPINDUZI THEN AKAENDA SIKINDE.

Thursday, February 13, 2014

ULALE PEMA KING KESTER EMENEYA


 Jean Emeneya Mubiala Kwamambu, maarufu kama King Kester Emeneya amefariki leo 13 February 2014 alfajiri saa kumi na moja na nusu katika hospitali ya  Marie Lannelongue katika jiji la  Paris akiwa na umri wa miaka 57.

Mwanamuziki huyu kiongozi na  mlezi wa kundi la Victoria Eleison. King alipata mshtuko wa moyo mara ya kwanza aliposikia kifo cha Tabu Ley mwezi November 2013 na akatibiwa katika hospitali hiyo ya Marie Lannelongue. Inaonekana  Kester Emeneya alishtushwa sana na kifo cha Tabu Ley ambaye alimuiga kwa mambo mengi. Rafiki wa Kester ambaye ni mwandishi wa habari Deck Mbutanganga alisema kuwa tangu kifo cha Tabu Ley, Kester hakurudia katika hali yake ya kiafya, alizidi kudhoufika mpaka alipofikia mauti yake..
King Kester alizaliwa mji wa Kikwit katika jimbo la Bandundu, magharibi mwa Jamhuri ya Kongo, alipofikia umri wa miaka 17 alianzisha kundi la muziki la Les Anges Noir, Malaika Weusi, akiwa na Lidjo Kwempa ambaye waliendelea kushirikiana katika muziki miaka mingi baadaye. Akiwa mwanachuo anaetafuta digrii ya Political Science katika Chuo Kikuu cha Lumbumbashi,  hamu ya kuwa mwanamuziki ikamzidia, mwaka 1977 akiwa na umri wa miaka 21 akaacha Chuo na kujiunga na kundi la Viva La Musica la Papa Wemba, akapata umaarufu mkubwa sana kama muimbaji, wakati mwingi ambapo Papa Wemba hakuwepo kwenye kundi hili Kester ndie aliyekuwa kiongozi. Hatimae tarehe 24 Desemba 1982 akazindua kundi lake la Victoria Eleison , kundi lililoleta ladha mpya katika muziki wa Kongo. Kester hutajwa kuwa mwanamuziki wa kwanza wa Afrika ya Kati kuingiza synthesizer kwenye muziki wake na album yake ya Zinzi, ambao wimbo huo ulitengenezwa studio tu, iliuza zaidi ya nakala milioni moja. Hakika alikuwa ndie mwanamuziki maarufu katika Afrika ya Kati katika miaka 1980-1990. Katika maisha yake Kester alipata Tuzo nyingi sana, kitaifa na kimataifa. Werrason na JB Mpiana walitumia nyimbo zake nyingi na mikongosio yake kutengeneza Wenge Musica. Amekwisha fanya maonyesho katika mabara yote matano duniani. Alijulikana kama Entertainer of the Year na magazeti mengi ya Kongo, katika onyesho lake moja Switzerland watu zaidi ya 12,000 walihudhuria, kitu ambacho kilitokea kwa mara ya kwanza kwa mwanamuziki kutoka Afrika kufanya katika nchi ile. Mwaka 1991 alihamia Paris na mwaka  1997 aliporudi Kongo kwa mara ya kwanza  baada ya miaka 6, onyesho alilolifanya Stade des Martyrs  lilihudhuriwa na watu 80,000.  Kester anasemekana alikuwa na nyimbo zaidi ya 1000.
 Marais wote wa Kongo waliwahi kumkaribisha katika Ikulu, Mobutu Sese Seko, Rais Laurent Kabila alimkaribisha ikulu mara tatu, na alishakaribishwa mara mbili na Rais wa sasa Joseph Kabila.
King Kester Emeneya amekuwa anaishi Ufaransa toka 1991 japo alikuwa na nyumba mbili Kinshasa katika eneo la watu wenye uwezo wa kifedha
Emeneya amekwenda lakini alichokiasisi kinaendelea katika jamii ya wapiga rumba Afrika
Mungu Mlaze Pema peponi.
Tumkumbuke kwa wimbo wa Zinzi hapa katika video hii;

Tuesday, January 14, 2014

FRANKLIN BOUKAKA WA LE BUCHERON AFRIKA


FRANKLIN  alikuwa mtoto wa mwanamuziki Aubin Boukaka wa kundi la "The Gaiety ", na mkewe Yvonne Ntsatouabaka aliyekuwa MC maarufu  kwenye misiba na pia alikuwa mwanamuziki muimbaji.  François Boukaka aliyekuja julikana kama Franklin alizaliwa tarehe  10 Oktoba, 1940. Yeye ndie alikuwa mtoto wa kwanza katika familia ya watoto wanane wavulana watatu na wasichana watano. Elimu yake yote aliipata katika shule mbalimbali nchini kwake Congo Brazzaville. Franklin  alianza mambo ya muziki 1955 katika kundi lililojiita Sexy Jazz lililoongozwa na Miguel Samba, baadae akaanzisha kundi la Negro Band. Hatimae katika safari yake ya muziki akaungana na wakali wengine kama  Edo Clary Lutula, Jeannot Bombenga, Tabu Ley , Mutshipile "Casino", André Kambite " Damoiseau ",  Papa Bouanga, Charles Kibongue katika lile kundi maarufu la African Jazz, sauti ya Franklin imo katika nyimbo kama  Mwana mawa , Catalina cha cha na Marie José zilizotungwa na Tabu Ley. Mwaka 1959 kundi la African Jazz lilimeguka baada ya wanamuziki wengine walipohamia Brussels wakifuatana na wanasiasa wa Kongo kwenye mazungumzo ya awali ya uhuru wa Kongo. Wanamuziki wote waliobaki akiwemo Jeannot Bombenga,  kasoro Tabu Ley wakajiunga na kuanzisha kundi jingine lililotingisha Africa lililoitwa Vox Africa, Franklin Boukaka na Jeannot Bombenga wakiimba. Baada ya hapo Franklin akaaliacha kundi hili na kurudi kwao Brazzaville ambako  1962 akawa mmoja wa wanamuziki wa Cercul Jazz, band iliyoanza miaka ya 50 ikiwa chini ya chama cha vijana kilichokuwa kikipata ufadhili wa serikali ya Ufaransa, chama hicho kiliitwa Cercule Culturel de Bacongo.  Hatimae Boukaka alikuja kuwa kiongozi wa chama hiki na kikawa na umaarufu wa mkubwa. Wimbo wa bendi hiyo "Pont Sur le Congo" (Daraja juu ya Mto Congo), wimbo ambao ulikuwa una hamasisha kuunganika kwa Congo Kinshasa na  Kongo Brazzaville baada ya nchi hizo kupata uhuru. Wimbo uliopata umaarufu kuliko nyimbo zote za bendi hiyo. Baadaye Franklin akiwa na gitaa lake kavu akaanzisha kikundi ambacho kilikuwa na wapiga marimba wawili akaweza kufanya ziara kadhaa hata nje ya nchi yake na kundi hili. Mwaka 1970 ndipo Boukaka  alipo rekodi nyimbo 12 zilizopangwa vyombo na Manu Dibango na hapo ndipo nyimbo Nakoki na Le Bucheron zilipopatikana. Baada ya hapo Franklin alijiunga na wenzie waliotaka kuipindua serikali ya Congo Brazzaville wakati huo ikiwa chini ya Rais Marien Ngouabi(aliyetuletea suti za Ngwabi). Jaribio hilo lililofanyika tarehe 22 February 1972 lilishindwa na siku chache baadae kifo cha Boukaka kilitangazwa.

Saturday, January 11, 2014

WAKUMBUKE ORCHESTRA MAQUIS ORIGINAL MAY 1996 -VIDEO

June 1, 1996 Jumamosi kulifanyika Tamasha kubwa la muziki katika viwanja vya Mnazi Mmoja, ilikuwa ni kuhamasisha utunzaji wa mazingira. Huu ulikuwa wimbo mmoja wa Maquis katika matayarisho ya siku hiyo.