Friday, October 11, 2013

VIDEO YA ONYESHO LA MWISHO LA FRANCO LWAMBO MAKIADI,,22 SEPTEMBA 1989



Ijumaa , Septemba 22, 1989 Franco Luambo Luanzo Makiadi alifanya onyesho lake la mwisho maishani mwake katika ukumbi wa De Melkweg jijini Amsterdam Uholanzi. Alipoingia tu katika ukumbi siku hiyo watu wote waliona kuwa Franco alikuwa katika hali mbaya kiafya, ilikuwa wazi siku hiyo kuwa wapenzi wa Franco walianza kukata tama kuhusu afya yake. Siku hiyo onyesho lilianza na kuendelea kwa karibu masaa mawili kabla Franco kuweza kupanda jukwaani. Siku hiyo kama ilivyokuwa kawaida MC alikuwa mpiga saxaphone wa OK Jazz Isaac Musekiwa, ambaye alikuwa na Franco toka 1957, na ndiye aliyemsaidia Franco kupanda jukwaani na kumuketisha kwenye kiti, lile jitu la miraba minne lilikuwa limepungua sana, hata kusimama ilikuwa ni mtihani.  Wimbo ambao ulikuwa upigwe ulikuwa ni Chacun Pour Soi, uliokuwa umetungwa na Josky Kiambukuta ambaye siku hiyo hakuweko. Alipoanza tu kupiga ikajulikana wazi alikuwa mgonjwa kiasi cha kushindwa hata kupiga gitaa. Ukisikiliza kwenye video hii utasikia jinsi anavyokosea kupiga utadhani anajifunza wimbo ambao alipiga mwenyewe, inasikitisha. Alijitahidi kuimba  sehemu zake na kujaribu kusimama kilipofikia kipande chake cha kucharaza solo hali ilikuwa mbaya wanamuziki wake walijaribu kumsaidia kusimama, lakini hakuweza kuendelea kupiga tena kwani alikuwa anakosea kosea hakuwa tena Franco yule. Ikalazimu kuacha jukwaa akiwaacha wanamuziki wake na wapenzi wake wakiwa wamechanganyikiwa kwa majonzi. Machozi yalikuwa yametanda ukumbi mzima. Siku 20 baada ya onyesho hilo tarehe 12 Oktoba 1989 L’Okanga Lwa Ndjo Pene Luambo Makiadi akiwa na umri wa miaka 51 tu alifariki katika hospitali mjini Namur Ubelgiji. 
MUNGU AMLAZE PEMA PEPONI AMEN


No comments: