Friday, February 26, 2016

MAZISHI YA MZEE KASSIM MAPILI


IMG_20160222_184035 MZEE MAPILI JUMATATU TAREHE 22 FEBRUARI 2016, AKIWA KWENYE KABURI LA FRED MOSHA MARA BAADA YA MAZISHIIMG_20160226_145039 WANAMUZIKI KATIKA MSIBA WA MZEE MAPILIIMG_20160226_155519 MWILI WA MAREHEMU KASSIM MAPILI UKIFANYIWA DUAIMG_20160226_145045 IMG_20160226_145054 IMG_20160226_151729 IMG_20160226_151732 IMG_20160226_153038 IMG_20160226_153042 IMG_20160226_155527 IMG_20160226_165932 IMG-20160226-WA0124 IMG-20160226-WA0125 IMG-20160226-WA0136 IMG-20160226-WA0138 IMG-20160226-WA0141 IMG-20160226-WA0142 IMG-20160226-WA0146 IMG-20160226-WA0149

IJUE HISTORIA FUPI YA MZEE KASSIM MAPILI

Mzee mapiliHAKIKA miezi michache iliyopita Mzee Kassim Mapili alinambia huku anacheka kuwa siku akifariki, maiti yake iagwe katika uwanja wa Mnazi Mmoja na kisha jeneza lake libebwe na wapenzi wake bila kutumia gari hadi Kisutu ambapo ndipo azikwe. Haikuwezekana kufanya shughuli ya kwanza ya kuaga lakini hakika Mzee Mapili amezikwa makaburi ya Kisutu kama alivyowahi kusema mara kadhaa. Jambo lililofanya Mzee Mapili asiagwe ni kutokana na mazingira ya kifo chake. Siku ya Jumanne usiku alipotoka kuangalia mechi ya Arsenal na Barcelona aliingia chumbani kwake na ni kwa wakati huo alipofikwa na mauti. Bahati mbaya baada ya kufikwa na mauti ilifikia mpaka Alhamisi jioni, ndipo maiti yake ilipogundulika na taratibu za mazishi zilipoanza kufanyika. Bahati mbaya tayari mwili ulishanza kuharibika hivyo haikuwezekana kutimiza nia ya marehemu ya kuagwa Mnazi Mmoja.
 12742369_10153337239035143_6265583808634571896_nMzee Mapili alizaliwa katika kijiji cha Lipuyu, Tarafa ya Lionya, Wilaya Nachingwea mkoani Lindi mwaka 1937. Hivyo umauti umekuta Mzee Mapili akiwa na umri wa miaka 79. Alipata elimu ya msingi huko kwao Lipuyu, sambamba na kupata elimu ya dini na mwenyewe aliwahi kusema alianza kupata mapenzi ya kuimba wakati alipokuwa Madrasa akighani Kaswida. Mwaka 1958 alijiunga na White Jazz Band iliyokuwa na masikani Lindi. Mwaka mmoja baadae akahamia Mtwara na kujiunga na Mtwara Jazz Band, lakini mwaka 1962 akajiunga na Honolulu Jazz Band ambayo nayo ilikuwa hapo hapo Mtwara.   Mwaka 1963, Mzee Mapili akachukuliwa na TANU Youth League ya mjini Lindi, na kujiunga na bendi ya Jamhuri Jazz Band ya hapo Lindi. Mwaka 1964 Mzee Mapili akachaguliwa kuanzisha bendi ya TANU Youth League ya Tunduru. Mwaka mmoja baadae alihamia Kilwa Masoko na kujiunga na Lucky Star Jazz Band ya mji huo. Baada ya hapo ndipo Kassim Mapili akatua katika jiji la Dar es Salaam na kujiunga na Kilwa Jazz Band iliyokuwa ikiongozwa na Ahmed Kipande. Kama ilivyokuwa sera ya wakati ule ya kuanzisha vikundi vya sanaa katika sehemu za kazi, majeshi yetu pia yalianzisha bendi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) nalo likaanzisha bendi na Mzee Mapili alikuwa mmoja ya waanzilishi wa bendi ya JKT Kimbunga Stereo mwaka 1965. Polisi nao kama majeshi mengine nayo pia ikaanzisha bendi na Mzee Mapili akajiunga na Police Jazz Band, 15 Desemba 1965. Mzee Mapili ndie aliyekuwa mwalimu wa bendi ya kwanza ya wanawake nchini Women Jazz Band iliyoanzishwa mwishoni mwa mwaka 1965.
FIL17
Women Jazz band

 Ni katika bendi ya Polisi katika mtindo wao wa Vangavanga ndipo jina la Mzee Mapili lilikuja julikana na sana, na hasa kutokana na tungo zake kama Dunia ulioimbwa na Moshi William, na Hayati Mzee Diwani. Baada ya miaka 16 katika bendi ya Polisi, tarehe 5 Mei 1981, Mzee Kassim Mapili alistaafu jeshi la Polisi. Baada ya kustaafu Mzee Mapili alijiunga na bendi ya Tanzania Stars iliyokuwa na makao yake katika hoteli ya Margot. Hoteli na bendi zilikuwa zikimilikiwa na Jumuiya ya Ushirika iliyojulikana kama Washirika na hatimae bendi hiyo ilikuja julikana kama Washirika Tanzania Stars.189860_1941025764239_4048980_n
Wanamuziki na viongozi wa Tancut Almasi Orchestra wakisherehekea ushindi katika Top Ten Show
 Mwaka 1982 baada ya semina ya wanamuziki iliyofanyika Bagamoyo Mzee Mapili alikuwa mmoja wapo wa wanamuziki walioanzisha Chama Cha Muziki wa dansi Tanzania, na akachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa kwanza wa chama hicho. Akiwa Mwenyekiti wa chama hicho mwaka 1986, aliweza kukusanya kundi la wanamuziki 57 ambao walitengeneza kund lililoitwa Tanzania All Stars. Kundi hili lilirekodi muziki ambao mpaka leo umekuwa katika kipimo cha juu ambacho hakijafikiwa na wanamuziki wa sasa. Wakati wa uongozi wa Mzee mapili kwa kushirikiana na Umoja wa Vijana wa CCM, Radio Tanzania, BASATA na CHAMUDATA waliweza kufanya shindano la bendi ambalo aina yake haijawahi kurudiwa tena, shindano hili lililoitwa Top Ten Show lilishirikisha bendi kutoka karibu kila wilaya hapa nchini. Uongozi huu aliendelea mpaka mwaka 1990. Mwaka 1993 alikuwa mmoja wa waanzilishi wa Shikamoo Jazz Band na katika bendi hii alitunga wimbo wa Eva uliokuwemo katika album ya kwanza ya bendi hii. Alipoacha bendi hii Mzee mapili alipitia Super Matimila, Gold All Stars, na hata kujiunga na binti wa Mbaraka Mwinshehe katika bendi yake ya Volcano Stars, na kipindi cha karibuni alikuwa akishirikiana na Mrisho Mpoto na wasanii mbalimbali katika muziki. Mzee Mapili ameacha watoto watatu. Hakika Mzee Mapili alikuwa mtu wa watu.

Thursday, February 25, 2016

MZEE KASSIM MAPILI HATUNAE TENA


Mzee mapili
MZEE Kassim Mapili hatunae tena. Habari ilitufikia jioni hii kuwa Mzee aliingia chumbani kwake Jumanne usiku akitokea kuangalia mechi ya Arsenal na Barcelona, na toka alipoingia hakutoka tena, hivyo jioni ya leo majirani walilazimika kutoa taarifa ambapo polisi walivunja mlango wa chumba cha Mzee na kukuta amefariki. Kutokana na hali ya mwili inaonekana alifariki tangu juzi na hali ya mwili si nzuri. Mzee Mapili alilazwa miezi michache iliyopita Muhimbili kutokan na kuwa na tatizo la moyo, lakini alikusema mwenyewe hata wiki iliyopita kuwa kutokana na kusaidiwa na Salma Moshi, msanii mkongwe anaeishi Marekani kupata Bima ya Afya hali yake imeimarika kwani anapata dawa zote zinazohitajika bila ya matatizo. Siku ya Jumatatu Mzee mapili alishiriki kikamilifu katika kumzika mtangazaji Fred Mosha, na hata kumuimbia marehemu akisikitika kuondoka kwake mapema. MUNGU AMLAZE PEMA MZEE WETU MAPILI

Sunday, February 21, 2016

LEO NDIO SIKU YA MAZISHI YA RAFIKI YETU NA NDUGU YETU FRED CAMILLIUS MOSHA


FRED
RIP FRED MOSHA
  LEO NDIO SIKU YA MAZISHI YA RAFIKI YETU NA NDUGU YETU FRED CAMILLIUS MOSHA. FRED ALIKUWA MTANGAZAJI ALIYEKUWA NA MAPENZI MAKUBWA NA MUZIKI WA DANSI. MAPENZI YAKE YALIANZA TOKA AKIWA MDOGO KWANI NAMKUMBUKA AKIJA NA MAMA YAKE KATIKA MADANSI YA MCHANA AMBAYO BENDI YETU YA TANCUT ALMASI ILIKUWA IKIPIGA KWENYE UKUMBI WA OMAX KEKO. UPENZI HUU ULIFIKIA MPAKA KIPINDI ALITAKA KUACHA SHULE NA KUJIUNGA NA BENDI YA DDC MLIMANI PARK, BAHATI NZURI MAMA YAKE ALIIKAMATA BARUA YA MAOMBI YAKE YA KAZI, NA KUZUIA MPANGO HUO WA KUACHA SHULE. FRED HAKIKA ALIKUWA MTANGAZAJI BORA WA HABARI ZA WANAMUZIKI WA MUZIKI WA ZAMANI WA DANSI.
RATIBA YA MAZISHI NI KAMA IFUATAYO;
  • SAA 4-5 MWILI UTAPELEKWA NYUMBANI KWAKE CHAMAZI UKITOKEA MUHIMBILI
  • SAA 7 MWILI KUPELEKWA KANISA LA RC CHANG'OMBE KWA MISA YA MAZISHI
  • BAADA YA HAPO SAFARI ITAANZA YA KUELEKEA MAKABURI YA KINONDONI KWENYE MAKAZI YAKE YA MILELE
  • MUNGU MALAZE PEMA PEPONI FRED MOSHA

Monday, February 8, 2016

WAKONGWE WA DANSI TANZANIA KATIKA WIMBO WA PAMOJA- MIAKA 50 YA UHURU

VIDEO HII YA WIMBO HUU MIAKA 50 YA UHURU INA KUMBUKUMBU NYINGI. HAPA WAPO PAMOJA JUKWAANI, KASONGO MPINDA NA KABEYA BADU