Shule zote zilikuwa na bendi ya shule. Ambayo kila asubuhi ilipiga muziki wakati wa wanafunzi kukaguliwa kama wamekuja shuleni wasafi, moja ya ndoto za wanafunzi wengi ni kuwa katika bendi ya shule. Aidha kuwa mpiga ngoma au mpiga filimbi na kubwa kuliko yote ni kupata bahati kuwa mshika kifimbo. Shule zilishindana kwa kuzivalisha bendi mavazi bora na upigaji kuwa makini na hivyo siku za sikukuu kila shule ilijitahidi bendi yake ndio iwe bora. Hakika nakumbuka raha iliyokuwepo wakati shule mbalimbali zilipokutana siku ya siku kuu au kukiwa na maandamo na kisha kila bendi kupita mbele ya mgeni wa heshima, wanafunzi tulijitahidi kuwa wakakamavu wenye nidhamu ili shule yetu ishinde.
TANU Youth League (TYL) ilikuwa na matawi kila mahala. Kimuziki TYL ilichangia sana, kwani kila kwenye tawi la TYL lazima kulikuwa na kundi la muziki aidha kwaya au ngoma, na mara nyingi vyote na sehemu nyingi TYL pia ilinunua vyombo vya bendi na hivyo karibu kila wilaya ilikuwa na bendi. Hapa ndipo wanamuziki wengi maarufu wa miaka hiyo na ambao nyimbo zao bado maarufu mpaka leo walikotokea. Pale Iringa, vyombo vya TYL hatimae viliishia kuwa chini ya shule ya Sekondary ya Mkwawa na hivyo pale kulikuwa na bendi nzuri sana ambayo iliweza kuja kurekodi RTD, kati ya waliokuwa wanamuziki wa bendi hiyo, mpia solo ni mzazi wa producer mmoja maarufu wa Bongo fleva na hata yeye alikuja kuwa na bendi yake TZ Brothers, mpiga rythm kwa sasa ana chuo kikubwa cha muziki pale Tabata, wakati muimbaji mmoja wa bendi hiyo alianzisha bendi maarufu pale Arusha.

























